Featured Post

UMAKINI UNAOTAKIWA KATIKA UFUGAJI WA MBUZI WA MAZIWA




Na Daniel Mbega
KWA ufugaji wetu wa asili, tumezowea tu kuwalisha mifugo chochote ambacho wanaweza kukipata, hususan nyasi na majani ya miti. Huo ni ufugaji wa mazowea!
Naam. Tunawapeleka ng’ombe au mbuzi mbugani au vichakani ambako wanapata lishe bora ya asili, jambo ambalo ni jema kwa sababu kadiri mifugo inapopata chakula cha aina tofauti ndivyo inavyotengeneza mseto mzuri wa nyama au maziwa.

Hata hivyo, linapokuja suala la ufugaji wakibiashara ambao una malengo ya kutengeneza kipato badala ya kufuga kwa ufahari kama tulivyozowea, ni lazima kujua namna nzuri ya kuihudumia mifugo yetu.
Ni lazima tutambue kwamba tunafuga kwa kufuata program inayoendana uzalishaji na ili kuyafikia malengo yetu ni lazima tuzingatie umakini katika kutunza mifugo hiyo.
Ndani ya MaendeleoVijijini ninazungumzia mambo mengi ya namna ya kuwahudumia mbuzi – iwe wa maziwa au nyama – maelezo ambazo yatawafaa wafugaji wote wa mbuzi bila kujali kama wanafuga kwa ajili ya maziwa au nyama.
Humu ninaelezea kuhusu namna ya kuwapandisha mbuzi wako wanapokuwa kwenye joto, namna ya kuwatunza madume, namna ya kuwatunza mbuzi kabla hawajafikia umri wa kuzaa, ukamuaji wa maziwa, faida za ufugaji wa mbuzi, na mambo mengine mengi.
Kila kipengele kitafafanuliwa vyema ili kwa kila mfugaji wa mbuzi wa jamii mojawapo aweze kujua nini cha kufanya katika kuboresha ufugaji wake.

Ulishaji wa mbuzi
Lishe ni jambo muhimu kwa kiumbe yeyote – iwe mnyama, mdudu au mmea katika kujenga mwili na kuzaa matunda. Hivyo, ni vyema kabisa kutambua kwamba, chakula unachomlisha mbuzi wako ndicho kitakachotengeneza maziwa au nyama.
Kwa maana hiyo, ni vizuri kutambua kwamba kumpa mbuzi chakula mahali pasipo safi si jambo jema kwa sababu mbuzi hula kila aina ya chakula kwa hiyo usiwaruhusu kula chakula kilicho na mchanga. Kuwalisha chakula kilichochanganyika na mchanga kunawafanya wawe katika uwezekano mkubwa wa kupata minyoo wanaopatikana kwenye mchanga.
Unaweza kuwafungulia mbuzi wako ili wale nyasi shambani na majani ya miti vichakani, hilo ni jambo jema, hasa unapokuwa na eneo kubwa la shamba ama uko kijijini ambako maeneo ya malisho ni mengi.
Lakini mbuzi wa maziwa mara nyingi hufugiwa kwenye mabanda kwa mfumo wa ‘zero grazing’, kwa hiyo ni lazima kuwatengezea mahali pa kulia chakula na kunywea maji ambapo panahitajika kuwa juu na mbali na nyumba yao ya kulala ili wasikanyage au kuchafua chakula.
Kwa kawaida, mbuzi mwenye uzani wa wastani huhitaji takriban nusu tani au kilo 500 za chakula cha hali ya juu ama nyasi zilizokaushwa kwa mwaka huku kiwango cha kila siku kikiwa asilimia 5-7 ya uzito wake.
Kupanga chakula cha mbuzi wa maziwa ni tofauti na kupanga chakula cha paka, mbwa ama binadamu. Kama walivyo ng’ombe, mbuzi pia ni wanyama wanaocheua (ruminants). Matumbo yao yamegawanyika katika sehemu nne na wanakula nyakula vyenye asili ya mimea ambavyo vina wanga wa kutosha pamoja na maji.
Mbuzi pia wanategemea vijidudu ndani ya matumbo yao ili kumeng’enya vyakula. Hii ni sayansi ambayo kwa yeyote aliyepita darasani anaweza kuikumbuka. Wakati chakula kigumu kinapoingia kwenye sehemu ya utumbo mpana (rumen) na reticulum, wadudu jamii ya protozoa na bakteria hukimeng’enya na kukiweka katika mfumo mwingine ambao utamwezesha mbuzi kukitumia kwa ajili ya shibe, kukuza mifupa, misuli, manyoya pamoja na kutoa maziwa. Kwa namna nyingine, unawalisha wadudu, na wadudu wanamlisha mbuzi.
Hii maana yake ni kwamba mbuzi anaweza kutumia kiasi kikubwa cha chakula, hususan nyasi.
Mbuzi mzuri katika utoaji wa maziwa pia anahitaji uwezo mkubwa wa kula nyasi za kutosha. Nyasi aina ya alfalfa mara nyingi zinapendekezwa kwa ajili ya ulishaji wa mbuzi wa maziwa, kwa sababu zina wingi wa protini na madini ya kalsiumu. Hata hivyo, nyasi hizo hazipatikani kila mahali, hivyo unaweza kutumia nyasi nyingine mbadala ambazo ni laini.
Majani kama vile napier, majani ya mahindi au mtama, mboga zisizotumiwa na majani ya viazi yanapaswa kukakatwa ili kupunguza uharibifu. Pia nyasi kavu za ngano au mpunga ni chakula kizuri kwao.
Wakati wa masika unaweza kukata nyasi nyingi na kuzianika halafu uzihifadhi vizuri kwenye banda maalum ili ziwafae kwa ajili ya kiangazi ambapo nyasi huwa shida kupatikana.
Kama chakula ulichowalisha bandani kimebakia, hakikisha unakiondoa na kumbuka tu kwamba, kama mbuzi wako wanabakisha chakula kingi hii ni ishara kwamba chakula hicho ni duni, ama unawapa chakula kingi kupita kiasi, au mbuzi wako hawana hamu ya kula chakula kwa sababu wana tatizo kama vile kutojihisi vyema au minyoo.
Unaweza kuwapa mbuzi nafaka kama njia ya kubadilisha chakula tofauti na kile cha kawaida, lakini tahadhali, zoezi la kuwabadilishia chakula cha nyongeza lazima lifanyike polepole na siyo mara moja ili kuwaruhusu mbuzi kuzowea chakula kipya bila kuwadhuru. Kamwe usiwape mbuzi nafaka tupu kwa sababu zinaweza kusababisha matatizo ya tumbo.
Unaweza pia kuwalisha mbuzi wa maziwa vyakula vya maziwa vinavyolishwa na ng’ombe katika kiwango cha nusu kilo kwa mbuzi asiyekamwa, kilo moja kwa mbuzi wa kukama lita moja ya maziwa na nusu kilo kwa kila lita zaidi ya maziwa.
Hakikisha unawalisha mbuzi madini muhimu kulingana na kiwango cha maziwa wanachotoa.
Wafugaji wengi wa mbuzi hupendelea kutengeneza chakula cha nyongeza wao wenyewe ili kuokoa fedha, kukifanya chakula hicho kiwe cha asili, au kwa sababu wana nafaka nyumbani, jambo ambalo ni zuri.
Unaweza kuchanganya nafaka, lakini kamwe haiwezi kuwa gharama rahisi, na itakuwa kazi kubwa. Nafaka hizo zinatakiwa kupondwa au kusagwa katika mchanganyiko huo. Unatakiwa kuongeza kiasi cha madini na protini ili kuweka uwiano mzuri. Utakapopiga gharama ya mchanganyiko huo na muda uliotumia na vifaa itachukua muda kuviandaa, utaona bora ukanunue.
Kama unalima bustani, mabaki ya mboga mboga kama mchicha, karoti, kabichi, spinachi, sukuma wiki na nyinginezo ni muhimu kwa malisho ya mbuzi wako, lakini hakikisha umeyasafisha ili yasiwe na mchanga ambao unaweza kuwa na wadudu wengine watakaoleta madhara kwa mbuzi wako.
Jambo jingine muhimu ni kwamba, unapaswa kuwapa maji safi ya kunywa kwa wingi kama lita 5 kwa kila mbuzi wa maziwa kwa siku.

Utunzaji wa kumbukumbu
Kuweka kumbukumbu za mifugo ni muhimu katika uzalishaji kwa ajili ya kutambua kosaafu, gharama za utunzaji na faida na humsadia mfugaji kufanya uamuzi katika kuendeleza ufugaji wake.
Ikiwezekana mtumie mtaalam wa mifugo ambaye atatumia kumbukumbu hizi ili kukusaidia kuboresha ufugaji wako.
Ni muhimu sana kuweka kumbukumbu hizi:
Kumbukumbu za idadi na ukuaji wa wanyama waliopo, jinsi zao, uzito wa kwa kila mwezi ili kufuatilia ukuaji wao, tarehe ya kuachishwa kunyonya na idadi ya waliouzwa.
Kumbukumbu za uzazi zinazoonyesha tarehe ya kuzaliwa, namba yake, jinsi yake, aina (breed), namba ya dume/jike, na uzito wa kuzaliwa.
Kumbukumbu za upandishaji zinazoonyesha namba ya mbuzi anayepandwa, tarehe ya joto na ya kupandwa, namba ya dume lililotumika kupanda, tarehe ya joto la pili kama atarudia na tarehe ya kuzaa.
Kumbukumbu za chanjo na matibabu zinazoonyesha namba ya mbuzi, tarehe ya matibabu, aina ya chanjo au ugonjwa, dawa iliyotumika, idadi ya waliokufa na waliopona na jina la mtaalam aliyetibu.
Kumbukumbu za maziwa zinazoonyesha namba ya mbuzi, tarehe ya kuzaa, kiasi cha maziwa kwa siku, na kiasi cha maziwa kwa kipindi chote cha kukamuliwa, tarehe ya kuacha kukamua na idadi ya siku alizokamuliwa.
Kumbukumbu za mapato na matumizi zinazoonyesha mapato na matumizi, vitu vilivyouzwa au kununuliwa kwa siku, kiasi cha fedha unachokuwa nacho kila wakati, kiasi cha fedha unachodai na kudaiwa.

Kwa maoni na ushauri, usisite kunipigia ama kuwasiliana name kwa whatsapp kupitia namba 0656-331974. Au barua-pepe: maendeleovijijini@gmail.com.




Comments