Featured Post

PROFESA NDALICHAKO ATAKA MAONYESHO YA SAYANSI KWA WANAFUNZI YAFANYIKE KILA WILAYA NA MKOA



 Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi ya Young Scientists Tanzania (YST), Dk. Gozbert Kamugisha, akimwelekeza jambo mgeni rasmi Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako, kabla ya kuanza kutembelea maonyesho ya sayansi ya wanafunzi ambayo yamefanyika kwa mwaka wa tano.

 Christina Godfrey Mongi (aliyetazama kamera), mwanafunzi wa kidato cha sita katika shule ya sekondari Bwiru Girls ya jijini Mwanza, akiwaelekeza watu mbalimbali kuhusu utafiti wao juu ya kuweka mazingira bora na salama ya kujifunzi kwa wanafunzi wenye albinism.
 Maonyesho yakiwa yanaendelea.
 Mbali ya maonyesho, wanafunzi pia walipata fursa ya kutengeneza marafiki wapya kama wanavyoonekana hapa wakijadiliana mambo mbalimbali.
 Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako, akisikiliza maelekezo kutoka kwa wanafunzi wakati alipofunga na kutoa zawadi kwa washindi katika maonyesho ya tano ya sayansi.
 Mkurugenzi Mtendaji wa YST, Dk. Gozbert Kamugisha (katikati) akimtambulisha Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako kwa Mwambata wa Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania, Moller Mathieu.
 Walimu wa shule mbalimbali zilizoshiriki maonyesho ya tano ya sayansi kwa wanafunzi wakifurahia jambo nje ya ukumbi wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam jana.
Wanafunzi wakiwa kwenye maonyesho hayo.

Na Daniel Mbega
WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako, amesema serikali itaandaa mazingira ya kuwaendeleza watoto na vijana wanajihusisha na ubunifu katika masomo ya sayansi na kushauri mashindano ya sayansi kwa wanafunzi yafanyike kila wilaya, mkoa na taifa.
Akizungumza wakati wa utoaji wa tuzo kwa wanafunzi waliofanya vizuri kwenye Mashindano ya Tano ya Young Scientists Tanzania 2016 katika Ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam jana, Profesa Ndalichako alisema hatma ya Tanzania iko mikononi mwa wanasayansi na kwamba vijana hao chipukizi ndio msingi mkubwa wa kuhimiza ushiriki wa wengi na kuibua vipaji vitakakvyolisaidia taifa.
“Huu ni ulimwengu wa sayansi na teknolojia, ili Tanzania iendelee ni lazima tujikite kwenye sayansi na kwa maana hiyo mimi kama waziri mwenye dhamana naahidi kwamba tutawajengea mazingira mazuri zaidi watoto wetu kwa ajili ya kujifunzia pamoja na kuendeleza vipaji vyao,” alisema.
Akaongeza: “Tunaomba wadhamini waliofanikisha maonyesho haya waendelee kudhamini lakini wajitokeze wengine ili kuhakikisha mashindano yanafanyika kuanzia ngazi ya wilaya, mikoa na hatimaye taifa na hapo ndipo tutakuwa tumejenga msingi imara wa kuibua wanasayansi wengi.”
Hata hivyo, aliwapongeza wanafunzi wote walioshiriki maonyesho ya mwaka huu na kuwataka waendelee na ubunifu huo kwa vile serikali imedhamiria kuwaendeleza.
“Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2025 inasisitiza, pamoja na mambo mengine, suala la sayansi na ubunifu, na Tume yetu ya Sayansi na Teknolojia (Costech) itasimamia kuhakikisha hawa watoto wanaendelezwa,” alisema.
Jumla ya shule 150 kutoka mikoa yote ya Tanzania zimeshiriki mwaka huu na kushuhudia wanafunzi 300 wakionyesha ubunifu wao, likiwa ni ongezeko la shule 30 kulinganisha na shule 120 zilizoshiriki mwaka 2015.
Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa YST, Dk. Gozbert Kamugisha, alisema kwamba maonyesho hayo yanazidi kupanuka tofauti na yalipoanza miaka mitano iliyopita, na sasa wanashukuru kuona shule nyingi zikishiriki zikiwemo za vijijini.
Alisema, hata hivyo kwamba, lengo lao ni kuhakikisha wanafanya mashindano hayo kuanzia ngazi ya wilaya hadi mkoa ili kuwapata washiriki wa kitaifa walio bora Zaidi.
“Hawa wote ni bora, lakini kama tukifanya mashindano haya kuanzia wilayani tutajenga misingi imara na kuwahasisha watoto wengi kuyapenda masomo ya sayansi na kujikita kwenye ubunifu,” alisema Dk. Gozbert.
Naye Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya YST, Profesa Yunus Mgaya, alisema kwamba, japokuwa si shule zote zenye maabara, lakini sayansi siyo lazima ifanywe ndani ya maabara bali hata katika masuala mengine ya kijamii.
Alisema kwamba, sayansi ni maisha ya kila siku na kwamba yako mambo mengi yanayoizunguka jamii ambayo kama wanasayansi watajikita kuyatafutia ufumbuzi yanaweza kuleta maendeleo.
“Siyo lazima kuingia maabara kufanya sayansi, kuna mambo mengi katika jamii ambayo yanaweza kufanywa na wanasayansi,” alisisitiza.
Kwa upande wake, Mwambata wa Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania ambao ndio wadhamini wakuu wa maonyesho ya YST, Mollar Mathieu, alisema kwamba kupitia shirika la misaada la Irish Aid, wataendelea kudhamini maonyesho hayo ili kuhakikisha vipaji vingi vinaibuliwa na watoto wa Tanzania wanajikita kwenye sayansi.
“Sisi kule Ireland maonyesho haya yamefanyika kwa mwaka wa 51 na yanaendelea kushika kasi huku tukipata wanasayansi wengi, naahidi kwamba tutaendelea kudhamini maonyesho haya ili hatimaye Tanzania ipate wanasayansi wengi ambao watasaidia kuleta mabadiliko,” alisema.
Katika maonyesho ya mwaka 2015, aliyekuwa mgeni rasmi, Rais mstaafu wa awamu ya pili, Alhaj Ali Hassan Mwinyi, aliwataka walimu katika shule za msingi na sekondari kutumia lugha ya Kiswahili kufundisha sayansi, kwani lugha hiyo inaeleweka vizuri.
Alhaj Mwinyi alisema Kiswahili ni lugha inayoeleweka vizuri, si kwa wanafunzi tu, bali hata kwa watu wengine, hivyo ni vyema walimu wakaweka mkazo katika kuitumia kwenye masomo ya sayansi.
“Nimepita kwenye maonyesho haya, baadhi ya wanafunzi walikuwa wananiuliza ‘tukueleze kwa Kiswahili au kwa Kiingereza’, nikasema tumieni lugha yoyote tu. Wengine wamenieleza Kiingereza na wengine Kiswahili.
“Lakini nataka niwaambie, walionieleza kwa Kiswahili, pamoja na utafiti wao kuwa katika lugha ya Kiingereza, walifafanua vizuri sana na nikasema ‘aah, kumbe Kiswahili kinaweza kutumika kufundisha vizuri sayansi,” alikaririwa akisema wakati huo.
Aliongeza kusema kwamba, yeye wakati anaingia darasa la tano, mwalimu wake wa sayansi alikuwa rais wa Scotland, lakini alimfundisha sayansi kwa Kiswahili na ndio msingi wake mkubwa wa kulifahamu vyema somo la sayansi.

Maonyesho ya mwaka yamechukua mpaka shule za vijijini, zikiwemo za Kata, na yametoa taswira halisi ya kitaifa.
Orodha ya shule zote zilizoshiriki maonyesho ya mwaka huu ni kama ifuatavyo:
Arusha (6): Trust St. Patrick, Edmund Rice, Ilboru, St. Jude, Suye, na Notre Dame.
Dar es Salaam (11): Debrabant, Kinyerezi, Manzese, Vingunguti, Loyola High, Mugabe, Jamhuri, Jangwani, Malamba Mawili, Makurumla na Aga Khan Mzizima.
Dodoma (4): Miyuji, Viwandani, Mpunguzi na Makutupora.
Geita (3): Geita, Buseresere na Geita Islamic Seminary.
Iringa (4): Mseke, Idetero, Kwakilosa na Mkwawa.
Kagera (6): Nyaishozi, Ihungo, St. Joseph Kolping, Rugambwa, Bulyakashaju na Kabanga.
Katavi (3): Mpanda Girls, Misunkulimo na Karema.
Kigoma (4): Masanga, Katubuka, Mwananchi na Gungu.
Kilimajaro (4): St. James’ Junior Seminary, Rau, St. Amadeus na Same.
Lindi (8): Lindi, Mtama, Mkonge, Ng’apa, Ngongo, Mingoyo, Angaza na Kilwa.
Manyara (4): Kwaraa, Chiefdodo, Endasak, na Bagara.
Mara (4): Mwisenge, Mara, Songe Girls, na Mwembeni.
Mbeya (6): Mbeya Sekondari, Iyunga Technical, Kalobe, Loleza, Mwakibete na Nzondahaki.
Morogoro (7): Mzumbe, Kilakala, Sumaye, Morogoro, Asodu Adrian Mkoba, Ifakara na Kibaoni.
Mtwara (10): Mtwara Technical, Mtwara Girls, Mtandi, Mahuta, Aquinas, Mayanga, Ndikwa, Chidya, Ndanda na Umoja.
Mwanza (7): Bwiru Girls, Bwiru Boys Technical, Mirongo, Butimba Day, Mkolani, Pamba na Mnarani.
Njombe (3): Mabatini, Luhololo na Mbeyela.
Pemba (4): Maendeleo, Utaani, Fidel Castro na Shamiani.
Pwani (7): Kibaha, Makurunge, Tumbi, Bagamoyo, Kibiti, Premier Girls, na Minaki.
Rukwa (5): Matai, Kipande, Miangalua, Kizwite na Uchile.
Ruvuma (3): Songea Boys, Kigonsera High, na Mbinga Girls.
Shinyanga (7): Ngokolo, Chamaguha, Uhuru, Buluba, Mwasele, St. Francis Of Assisi na Msekelo.
Simiyu (4): Nassa, Mwamanongu, Binza na Maswa Girls High.
Singida (4): Dk. Salmin Amour, Ilongero High, Kijota, na Mandewa.
Tabora (4): Tabora Girls, Tabora Boys, Puge na Ipuli.
Tanga (7): Old Tanga, Macechu, St. Christina, Popatlal, Mkwakwani, Mikanjuni na Tanga Technical.
Unguja (7): Lumbumba, Kiembe Samaki, SoS Hermann Gmeiner, Haile Selassie, Mpendae, Ben Bella na Mwanakwerekwe A.





Comments