Featured Post

WASI (WAALAGWA): KABILA LENYE UTATA WA UTAMBULISHO

Bibi wa Kialagwa katika maskani yake huko chini ya Mlima Wasi.


Na Innocent Nganyagwa
NDUGU zangu, nawakaribisheni kwenye safu yetu ya Asili na Fasili inayotuwezesha kutopea kwenye ujadi wa makabila yetu mbalimbali hapa nchini.
Basi leo tunawatembelea ndugu zetu Wasi, au kama wanavyofahamika kwa jina lingine, Waalagwa.

Kwa kupiga hodi kwa ndugu zetu hawa, na tuko Kondoa huko Dodoma tunapokutana na ndugu zetu hawa wanaozungumza lugha yao ya Chasi.
Utambulisho wa ndugu zetu hawa una utata kutokana na sababu kadhaa kama nitakavyoeleza.
Kwanza, huwa wanadhaniwa kuwa ni sehemu ya jamii ya makabila mengine wanayotangamana nayo kwenye eneo moja. Jambo hilo husababisha kupotoshwa kwa utambulisho wao halisi.
Sababu nyingine ni kutokana na kuhusishwa na mbari mbili tofauti za Uhamitiki na Ukushi.
Kwa kabila kuhusika na mbari mbili sio tatizo sana, maana kuna makabila yanatoka moja kwa moja kwenye zile mbari kuu tano za Afrika.
Lakini pia kuna makabila yanayotokana na mchanganyiko wa zaidi ya mbari moja, lakini kwa hawa Wasi tutaona kwa kina nini hasa kinachochanganya utambulisho wao.
Basi ili tuweze kufika huko tuanze kutazama mambo ya hawa Waalagwa.
Kwanza hawa ndugu zetu ni wachache na ni moja kati ya makabila madogo hapa nchini, wengi wao bado wanaishi kwenye eneo lao la nchi ya Ualagwa bila kuhama kutoka eneo hilo.
Majirani zao wa kihistoria walio mkabala nao ni pamoja na Wamaasai (Wanailotiki), Wasandawe (Wakhoisan), Wairaqw, Waburunge, Wasi na Wagorowa (Wakushi) na Wambugwe (Wabantu).
Ndugu yangu, kwenye mabano ndizo hizo mbari kuu tano za Afrika ambazo huwa narudia kuzitaja mara kwa mara, katika kupeana elimu ya kina kuhusu chanzo cha makabila.
Na tutakapowatembelea Warangi, tutaona baadhi ya athari za matamshi ya lugha zao kutokana na baadhi ya makabila majirani zao kugubikwa na lugha yao ya ‘Kilaangi’ (Kirangi).
Halafu lugha hiyo iliporudi tena ndani ya Kirangi ikawa na zile athari za kimatamshi, mojawapo ya makabila hayo ni Waburunge na hawa Wasi.
Hilo pia husababisha watu wengi kutatanishwa na utambulisho wa Waalagwa na kudhania kuwa nao ni sehemu ya jamii tanzu za Kirangi.
Kadiri tutakavyoendelea kuchambua mambo yao hawa Waalagwa, tutaona pia sababu nyingine inayosababishwa na mbari yao na Warangi inavyochangia pia utata huo.
Awali tulipotembelea kabila la Wairaqw ambao ni Wakushi, tuliona kuwa katika safari yao iliyowafikisha huko Manyara waliko, walipita mahali tulipo sasa, yaani Kondoa.
Walipoondoka Kondoa walipoishi kwa muda, Wairaqw waliohamahama ili kukwepa vita waliacha mabaki ya jamii zao kwenye eneo hilo.
Baadhi ya mabaki hayo yalijumuika na kuchangia kuwepo kwa makabila ya Waburunge na Wasi, na walipofika karibu na eneo walilokuwepo walisababisha kuwepo kwa kabila la Wagorowa.
Kwa hiyo, mpaka hapo utaona kuwa kule kutatanishwa utambulisho wa Wasi kwa kudhani kuwa ni Warangi au Wairaqw, kunachangiwa pia na hizo mbari mbili za Kikushi na Kihamitiki ambazo makabila ya Warangi na Wairaqw nayo pia yanatokea humo.
Lakini tukiwaangalia zaidi wao wenyewe, ni kwamba Wasi wanapatikana katika nchi yao ya Ualagwa yenye vilima vyenye miamba na mabonde yaliyo katikati ya vilima hivyo.
Vilima hivyo vyenye baadhi ya wanyama pori, ni chanzo cha nishati kwa matumizi yao ya kila siku kwa kuwapatia kuni.
Nchi ya Ualagwa ina udongo mgumu wenye asili ya miamba, kutokana na eneo lenyewe lilivyo kijografia.
Katikati ya nchi hiyo ndipo eneo lenye rutuba zaidi linapopatikana, kutokana na Mto Bubu wenye maji safi kukatiza eneo hilo.
Maeneo ya mwinuko kwenye vile vilima, kwa kawaida yana uhaba mkubwa wa maji kutokana na ukame, hali hiyo pia huchangiwa na uhaba wa mvua.
Kwa kawaida msimu wa mvua za kuaminika kwenye nchi hiyo ya Ualagwa ni kati ya Desemba na Mei.
Kwa asili, Wasi ni watu kutoka jamii mchanganyiko za mbari za Kikushi na Kihamitiki.
Kuhusika kwao na mbari hizo mbili ni kutokana na kuwa na misafara iliyo tofauti na makabila mengi ambayo tutaendelea kuyachambua kwenye hii safu yetu ya kijadi.
Tofauti hiyo ninayoizungumzia, ni kuwa mengi ya makabila tutakayoyatembelea tutaona jinsi jamii zao zilivyolowea na kuweka makazi, baada ya kuzurura hasa kutokea upande wa kaskazini.
Hawakurudi nyuma walikotokea, bali walitawanyikia maeneo ya pembezoni na kusambaa sehemu mbalimbali baada ya kufika hapa nchini.
Lakini masalia ya jamii zilizozalisha kabila la Wasi, yalitoka Iramba-Singida kwenda Mashariki ya Kati miaka mingi iliyopita.
Kama unaifahamu vyema ramani ilivyo, utakumbuka kuwa ukipita mashariki ya kati unapoelekea Mashariki ya Mbali lakini kwa uelekeo wa upande wa Arabuni, huko Saudia, eneo hilo lina kiini cha chanzo cha mbari ya Kihamitiki. Safari hiyo ya Wasi kurudi kaskazini, ni kinyume na jamii nyingi zilizokuja huku kutoka kaskazini.
Maana wao walitoka huku kuelekea kaskazini, lakini walipofika huko hawakuweza kutangamana na wenyeji waliowakuta huko.
Sababu kubwa ni wao kutokuwa na imani kama za wenyeji waliowakuta, ambao kwa sehemu kubwa walishaukumbatia Uislamu.
Kwa hiyo ndugu zetu Wasi, wakati huo wakiwa katika zile jamii zao za awali walipofika huko waliendelea kuabudu mizimu ya mababu zao kwa imani za kijadi zilivyo.
Hilo ndilo lililowafanya wasitangamane na kuwiana na wale wenyeji wa Mecca, ambako kunafahamika kuwa kiini cha imani ya Uislamu.
Baadaye jamii hizo zikageuza na kuanza kurudi tena upande huu waliotoka. Katika njia yao wakapitia eneo la Uhabeshi huko Ethiopia ambako pia Wakushi wanapatikana kwa wingi.
Kukatokea mchanganyiko tena wa mbari, maana kumbuka kuwa kule walikoenda ni nchi ya Uhamitiki na hapa walipopita ni moja kati ya nchi za Kikushi.
Ndiyo maana niliwatahadharisha kuwa, kadiri tutakavyoendelea na mambo ya ndugu zetu hawa tutaona ule utata wa utambulisho wao kupitia mbari.
Ukiachilia pia kule kubanwa katikati ya jamii masalia za Warangi (Wahamitiki) na Wairaqw (Wakushi).
Katika kurudi tena hapa nchini, kama yalivyo makabila mengi yaliyoingia na kuja hadi uwanda wa kutoka kaskazini magharibi hadi mashariki.
Wakafika Halas’o katikati ya Mlima Hanang’ na Kondoa, wakaishi kwa muda kabla ya kuanza tena safari iliyowafikisha walipo sasa huko nchi ya Ualagwa-Kondoa.
Eneo hilo walilokaa kwa muda mara kadhaa hutoa viashirio vya mizimu yao, kwa kusikika sauti za ngoma zao zikipigwa nyakati za usiku huku watu wakiimba na kucheza bila hao wapigaji na wachezaji kuonekana. Ni eneo ambalo bado lina nguvu za mizimu yao.
Ndugu yangu, nikufahamishe kuwa hawa Waalagwa ambao pia huitwa Wasi wana mambo yao yanayotegemea nguvu za kijadi.
Mathalan, walikuwa na kawaida ya kufanya matambiko ya kuita mvua ukame unapokithiri.
Tambiko la aina hiyo hufanyika chini ya mti, ambapo majani ya mti husika huchumwa na kusagwa na kupondwa.
Kisha kondoo mweusi huchinjwa na damu yake hunyunyizwa kwenye yale majani yaliyotapakazwa kuuzunguka ule mti, hivyo damu ile pia hunyunyizwa kuuzunguka mti huo wa tambiko la kijadi la Kialagwa.
Naam, tumeshapiga hodi kwa ndugu zetu Wasi (Waalagwa), ambao tutaendelea kuchambua mambo yao kesho.


Makala haya yamehaririwa, yalichapishwa kwa mara ya kwanza katika gazeti la Tanzania Daima Juni 06, 2009.

Comments