- Get link
- X
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- X
- Other Apps
HISTORIA kuhusu Chifu Mkwawa kuandikwa
upya baada ya watafiti wa mambo ya kale kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
kuvumbua ushahidi wa makasha ya risasi eneo la Lugalo wilayani Kilolo mkoani
Iringa.
Mtafiti wa mambo ya kale, Dkt.
Frank Masele, amesema katika utafiti wao wamegundua makasha ya risasi kwenye Kijiji
cha Lugalo kwenye maadhimisho ya miaka 127 ya Vita ya Mkwawa dhidi ya Wajerumani.
Katika vita hiyo iliyopiganwa Agosti
17, 1891 Mkwawa alifanikiwa kuwaua askari wapatao 300 pamoja na kiongozi
wao Emil Von Zelewisky ambapo baada ya kushindwa vita hiyo Wajerumani walikwenda
kujipanga upya namna ya kumkabili Mkwawa.
Dkt. Masele amesema kuwapo kwa
mabaki mengi ya maganda ya risasi katika eneo hilo la Lugalo kunaonesha
kulikuwa na mapambano makali ya kivita ambapo licha ya majeshi kutumia silaha
za jadi kama mikuki bado waliwashinda Wajerumani ambao walikuwa wakitumia
silaha kali za kivita.
Hili ndilo Kaburi maarufu la Nyundo walikozikwa makamanda wote wa Kijerumani waliouawa na Mkwawa mwaka 1891 Lugalo
“Leo tupo hapa kuendelea
na utafiti wetu eneo la Lugalo, tumekuja kutafuta ushahidi, na kwa bahati nzuri
tumepata maganda ya risasi zilizotumiwa na Mjerumani na huu ndio ushahidi
pekee, Mkwawa alitumia mkuki na Mjerumani alitumia silaha hizi kali na katika
harakati za kuikomboa nchi yetu hatuwezi kukwepa kijiji hiki cha Lugalo na ndio
maana nimekuja na wanafunzi wangu 49 ili wajifunze kwa vitendo zaidi,” alisema
Dkt. Masele.
Naye Fatuma Mkwawa ambaye ni
dada wa Chifu Mkwawa aliiomba serikali kuweka kumbukumbu nzuri kwa kujenga
mnara au sanamu ya Mkwawa mwenyewe jambo ambalo familia itapendezwa zaidi
kumuenzi kuliko hayo makaburi ambayo yanaonesha bado wanaendelea kuwatukuza Wajerumani.
Awali akizungumza, Mzee Alfred
Mnyagala ambaye alizaliwa mwaka 1910 kijijini hapo na kupigana Vita ya Pili ya Dunia,
alisema duniani hakuna sehemu Wajerumani walikopigwa kama Iringa na walivyorudi
kwa mara ya pili kwa lengo la kuteketeza ngome ya Mkwawa walipitia Kata ya
Lulanga, Nguluhe, Tosamaganga hadi Kalenga na walimkuta Mkwawa ameshajimaliza
mwenye kabla ya kukamatwa na Wajerumani.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya
ya Kilolo, Asia Abdallah, na Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Richard Kasesela, kwa
pamoja wamesema wamepokea maombi yaliyotolewa na mwanafamilia huyo kuhusu
kuendeleza eneo hilo kwa kuwa Mkoa wa Iringa uliteuliwa kuwa kitovu cha utalii.
Abdallah alisema kuwa katika
kukuza utalii wa Kusini mwa Tanzania ni lazima kuviibua na kuvitangaza vivutio
vyote vya kiutamaduni pamoja na hifadhi za taifa ili viweze kutangazwa kwa
lengo la kuwanufaisha wananchi, kuingizia taifa fedha za kigeni, kuongeza ajira
kwa vijana pamoja na kuwafundisha watoto historia ya vivutio hivyo kwa ajili ya
kizazi cha sasa na cha baadaye.
Katika maadhimisho hayo ambayo
yamefanyika kwa mara ya kwanza serikali za wilaya zote mbili zimepokea matokeo
ya awali ya watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Idara ya Ikiolojia na Taaluma
za Urithi wa Utamaduni na pia Abdallah alisisitiza dhamira ya serikali
kuboresha kaburi hilo linalofahamika kama Kaburi la Nyundo ili kuwavutia
watalii wengi zaidi na kuongeza pato la Mkoa wa Iringa.


Comments
Post a Comment