Featured Post

MISAADA NI KUTAFUNA KIVULI CHA MPOKEAJI




NA ALOYCE NDELEIO
Miongoni mwa nchi zinazoendelea zimeshajengeka fikra kwamba bila misaada haziwezi kupiga hatua na hilo kushabikiwa na walio wengi imekuwa ni jambo la kusikitisha.
Inasikitisha kwa sababu hali hiyo ni kujikana na hata kujilemaza na kuwa tegemezi ilhali zinaweza kujinasua katika mkondo huo.

Wanaoona kujinasua wamekuwa wakidhihakiwa kwamba si rahisi kwao kujitegemea kwa kuwa ubavu wa kufanya hivyo hawana, lakini hali ni tofauti kwani ubavu wa kufanya hivyo upo.
Walio katika mkondo huo hususani miongoni mwa nchi za Afrika wanatambua kuwa zipo rasilimali nyingi ambazo zinaweza kutumika  badala ya kutegemea misaada.
Kilichojitokeza katika mkondo huo ni kwamba nchi zilizoendelea na ambacho  zinategemewa kwa misaada zinatambua kuwa misaada zinayotoa haisaidii kuzinyanyua nchi zinazoendelea, lakini haziweki hilo wazi.
Hilo linawekwa wazi na baadhi ya watu kutoka katika nchi hizo hizo zilizoendelea ambao wanasikitishwa na matendo au unafiki uliomo katika utoaji wa misaada.
Uthibitisho huo umo katika  Kitabu kilichoandikwa na William Easterly, na kuchapishwa na kampuni ya Penguin  Press mwaka 2006  katika ukurasa wa nne, ambacho kwa Kiingereza kinafahamika,  “The White Man’s Burden; Why the West’s Efforts to Aid the Rest have Done So Much Ill and so Little Good.”
Kwa tafsiri isiyo rasmi; “Mzigo wa watu weupe; Kwanini juhudi za msaada za Magharibi Mingi Imeleta Maumivu Makubwa na Neema Kidogo Sana.”
Anasema, “Janga linalowakabili maskini linatokana na kwamba nchi za Magharibi zimeshatumia dola trilioni 2.3 kwa ajili ya misaada inayotoa nje katika kipindi cha miaka miongo mitano na hata hivyo hazijaweza  kutoa senti 12 za dawa kwa ajili ya watoto ili kuwaokoa nusu yao na vifo vinavyotokana na malaria.
“Nchi hizo zimetumia dola trilioni 2.3 lakini zimeshindwa kutoa dola nne kwa ajili ya vyandarua kwa familia maskini.
“Zimeshatumia dola trilioni 2.3 na bado zimeshindwa kutumia dola tatu kwa ajili ya mama anayejifungua kwa mara ya kwanza ili kuzuia vifo milioni tano vya watoto.
“…Inavunja moyo kwamba jamii duniani zimeibua njia zenye ufanisi wa hali ya juu kwa ajili ya kutoa burudani kwa matajiri, watoto na watu wazima, wakati haiwezi kutoa senti 12 kutibu watoto maskini wanaofariki.”
Nukuu hiyo haina ubishi wa aina yoyote kwamba aliyoyaelezea mwandishi huyo ni ukweli kuwa kile wanachokitoa nchi tajiri ni sawa na tone la maji kutoka baharini na kwamba hiyo haiwezi kuwa ni misaada bali ni sawa na makapi tu.
Kauli hiyo haijatoa kwa mwandishi huyo katika kitabu chake tu, bali pia watu maarufu kutoka nchi zilizoendelea nao wamekuwa na mawazo yanayoonesha kuwa upo unafiki mkubwa katika utoaji huo wa misaada.
Rais wa 39 wa Marekani, Jimmy Earl Carter katika nukuu  yake moja alisema kuwa wakati Marekani inatoa kiwango kikubwa cha misaada ya kivita kwa nchi inazoziona kimkakati kuwa ni muhimu, inashika nafasi ya chini miongoni mwa nchi zilizoendelea  katika kiwango cha misaada ya kibinadamu inayotoa kwa nchi maskini; na kuongeza, “Tumekuwa wang’ataji  kushinda mataifa yote.”
Kauli ya Rais wa zamani wa Marekani Jimmy Carter aliitoa hivi karibuni  katika Chuo cha Principia kilichopo Elsah, katika jimbo la Illinois.
Kwa mtazamo huo ndipo zinapoibuka kauli kwamba itakuwa inashangaza sana kuwaona watu na akili  zao timamu kushangilia kupata msaada. 
Mshangao huo unaibua hoja  kwamba wanatusaidia kwa sababu gani?  Wana mapenzi na nchi  maskini kwa sababu ipi? Ni wajomba, wazazi na wana uchungu na nchi maskini? Kuna ule msemo kwa lugha ya Kiingereza "there is no free lunch", tafsiri yake hakuna mlo wa mchana wa bure.
 Jambo la msingi ni kwamba nchi zinazoendelea hususani Tanzania na kwa kulingana na kauli ambayo iliwahi kutolewa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwamba nchi hii si ya kuomba kwa mtu yeyote kwani ina kila kitu. 
Aidha jambo linalotakiwa ni kuwa na uhuru kamili juu ya rasimali zetu kwa kuzitumia kwa ufanisi, kuziongezea thamani, na kushiriki kupanga bei ya kuuza bidhaa zinazotokana na rasilimali zetu bila ya kupangiwa bei kwa maufaa yetu na si kuegemea katika  huo uhuru wa bendera ulipo. 
Japo lililo dhahiri ni kwamba uwezo huo upo kwa jamii  kuacha kuwa makuwadi na badala yake kipaumbele kiwe ni kuiweka Tanzania mbele badala ya kuweka ubinafsi, wizi, udanganyifu, ubadhirifu, ufisadi na aina yoyote ile ya uchafu wenye taswira ya kuipeleka nchi kombo.
Hali hiyo inamaanisha kile alichokisema Rais kuwa badala ya wao kuwa watoa msaada sisi ndiyo  tunatakiwa kuwapa msaada kwani wao wanatuhitaji sisi kuliko tunavyowahitaji. 
Tafakari inayoweza kuweka jambo hilo kwa uwazi ni ya kujiuliza ni bara gani duniani lenye rasimali nyingi zaidi hapa duniani kwa wakati huu ambazo bado hazijatumiwa? Kwa nini kila mataifa makubwa yako kiguu na njia kuja Tanzania, Congo DRC na Afrika ya Kusini na nchi nyingine za Afrika?
 Sharon LaFraniere, mwandishi  wa gazeti la New York Times, Julai 2005  aliandika  kuwa  kiasi kikubwa cha fedha za msaada zaidi ya dola milioni 300 zilizotolewa kwa Afrika kuanzia mwaka 1980 ziliishia kwenye  mashimo ya utapeli, ubadhirifu na kupotea katika mazingira yasiyoeleweka.
Hata hivyo mchumi mwandamizi Paul Collier yeye aliandika kwenye Jarida la Uchumi la Afrika Mei 2006 kwenye makala yake, “Nini tunatarajia  kutoka kwenye msaada kwa Afrika?… ukweli uko wazi  na kinyume na imani hiyo. Misaada  haijapotea bure; bali imeuweka uchumi wa Afrika kuelea na kupita kwenye kipindi kigumu.”
Kwa mujibu wa Benki ya Dunia kwenye mada  inayohusu misaada kwa nchi za  Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara na mustakabali wa dola bilioni 650 inatuhumu kuwa misaada imekuwa inatiririkia mikononi mwa madikteta na tawala za rushwa ambazo hazina nia za dhati na maendeleo ya taifa.
Hali kadhalika kwa mujibu wa Kituo cha Utafiti wa Maendeleo  Kimataifa cha Ufaransa, kufungamana na nchi zilizokuwa zinazitawala wakati wa ukoloni nako kumekuwa ni kigezo cha kihistoria  cha  kutolewa kwa misaada.
 Hata  hivyo Chuo Kikuu cha Maryland  katika kupima watendaji wanavyoshikilia madaraka  kwa kutumia mfumo unaofahamika kama   ‘Polity IV’ kinabainisha kuwa  takribani  nusu ya misaada yote  kuanzia mwaka 1960-90 ilienda kwa nchi ambazo zilikuwa na ‘mamlaka ya utendaji isiyo na mipaka’ na asilimia 10 tu  ilienda kwa nchi zilizokuwa na demokrasia yenye ‘mipaka ya utendaji’.
 Ipo nahau moja inayosema, ‘Kula mtu kivuli’ inayomaanisha  kumfanyia mtu mambo ya kumdhuru na kumwendea kinyume na hali mbele ya macho yake unamwonesha kuwa mwema kwake.
Hivyo ndicho nchi zilizoendelea zinazifanyia nchi zinazoendelea.

Comments