- Get link
- X
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- X
- Other Apps
NA ALOYCE NDELEIO
Mafanikio ya kuwalinda tembo dhidi ya ujangili yametokana
na mikakati kadhaa ya msingi ambayo
imewezesha wanyama hao kuongezeka ikiwemo ushirikishwaji wa jamii, kuongeza
askari, matumizi ya teknolojia kupambana na majangili na ushirikishwaji wa
jumuia ya kimataifa.
Aidha mikakati mingine ni kusitisha biashara ya meno ya
tembo, ushirikiano miongoni mwa nchi za Afrika, mikataba baina ya nchi jirani,
uratibu wa utekelezaji wa sheria, mchango wa mashirika ya wanyama pori na
tafiti mbalimbali duniani.
Hizi ndizo nyenzo ambazo zimewezesha kuleta matumaini kwenye
maisha ya mnyama huyo, na hata hivyo ushirikishwaji wa jumuia na watu hususan
katika muundo wa Maeneo ya Uhifadhi
ya Wanyama pori (WMA) imewezesha jumuia kwenye maeneo yanayozunguka hifadhi
kujihusisha kwenye kuhifadhi
na matumizi endelevu ya bidhaa
zinazotokana na wanyama pori
Awali maeneo hayo yalikuwa yakisaidiwa na serikali ya Tanzania na Shirika la Misaada la Marekani
(USAID) na WMA nyingine kama Ikoma
zimekuwa na mafanikio kwenye kupata fedha na hali kadhalika kwenye
kuhifadhi.
Jumuia kwenye maeneo haya zimekuwa zinafanya upelelezi ambao
umekuwa unasaidia juhudi za serikali katika kupambana na ujangili kwenye maeneo
hayo.
Kwa upande wa matumizi ya askari wanyama pori inafahamika
kuwa iwe iwavyo hakuna kinachoweza
kuchukua nafasi ya askari hao kutokana na kujituma kwao kulinda wanyama pori
nchini Tanzania.
Kipindi cha hivi karibuni idadi ya askari wanyama pori
iliongezwa mara mbili zaidi ili
kukabiliana na changamoto zilizopo
kwenye mfumo wa ikolojia wa Ruaha-Ruangwa ambao umekuwa unaonekana kama
kitovu cha uhalifu wa ujangili Tanzania
na hivyo kuwa ndio lengo kuu katika kuchukua hatua.
Matumizi ya teknolojia katika kupambana na ujangili ni jambo ambalo limekuwa likifanyika kuanzia kwenye majaribio hadi kufanikiwa
kutumia ndege zisizo na rubani (drone), matumizi ya kidijitali ya mawasiliano ya Very High
frequency (VHF) na matumizi ya kompyuta
zilizo na GPS miongoni mwa askari wanyama pori mambo ambayo yameifanya
Tanzania kuwa mstari wa mbele katika
mstari wa kupambana na majangili.
Ongezeko la matumizi ya ndege maalum, helikopta na hali
kadhalika aina mbalimbali za magari kwenye uwanja wa mapambano kumekuwa kunabadilisha mwenendo wa vita dhidi
ya ujangili.
Serikali ilishabainisha kuwa kwenye ushirikiano wa kimataifa
kwamba tangu kuridhiwa kwa mkakati wa kupambana na ujangili, serikali imefanya kazi kwa ukaribu na washirika wake
wa maendeleo katika kukabiliana na tatizo hilo kwa pamoja.
Hali hiyo ilisababisha kunaamini kwenye uwazi na ufumbuzi
katika kuendeleza mafanikio yaliyopatikana kwenye vita dhidi ya ujangili.
Programu ya Maendeleo ya Umoja wa Mataifa (UNDP), Ujerumani,
Uingereza, Marekani, China na Benki ya Dunia
ndio wamekuwa washirika wanaoongoza katika kushirikiana na Tanzania
kwenye juhudi zake za kupambana na ujangili.
“Tanzania pia imejiunga na
Mkakati wa Kulinda Tembo Afrika (AEPI) pamoja na nchi za Botswana,
Gabon, Chad na Ethiopia chini ya uongozi
wa Uingereza kuratibu juhudi za
Afrika kwenye mataifa yaliyo mstari wa
mbele katika vita dhidi ya ujangili.
“Mbali na maazimio ya mkutano mbalimbali Tanzania imejikita
kufanya kazi na serikali ya Uingereza kupitia makubaliano na shirika la Stop
Ivory ambalo ni shirika la hisani la
Uingereza na imeshuhudiwa ikifanya kazi
na wataalamu wakiwemo kutoka CITIES
katika kukusanya shehena kubwa ya pembe za ndovu nchini.
Kuhusu ushirikiano miongoni mwa nchi za Afrika Novemba 2014 Tanzania ilikuwa mwenyeji wa mkutano wa kikanda
uliozikutanisha nchi 11 kwa ajili ya
kujadiliana na kufikia maamuzi ya hatua
zinazotakiwa kuchukuliwa kudhibiti na
kuzuia uhalifu dhidi ya wanyama pori.
Kuwepo ushiriki hai wa Benki ya Dunia (WB), Umoja wa Ulaya
(EU), Marekani, Uingereza, Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB), China, Ufaransa,
Ujerumani na nchi 11 za Afrika ambazo ni
Tanzania, Kenya, Uganda, Burundi, Rwanda, Sudan Kusini, Malawi, Zambia,
Msumbiji, Afrika Kusini na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC), zilikubaliana
kuhusu hatua za ziada zinazotakiwa kuchukuliwa kwa pamoja katika kusitisha mauaji ya wanyama pori.
Hata hivyo kuhusu makubaliano na nchi jirani yapo
makubaliano ya Selous-Niassa kati ya
Tanzania na Msumbiji ambayo ni matokeo
ya mkutano uliofanyika Arusha hivi
karibuni.
Kwenye makubaliano hayo juhudi za kimataifa ziliwekwa pamoja katika kuisaidia Tanzania na Msumbiji kuyaweka kwenye utendaji makubaliano ya
kuulinda mfumo mkubwa wa ikolojia ya wanyama pori ambao unahusisha eneo la
ardhi ya kilomita za mraba 110,00.
Makubaliano hayo hatimaye yalisainiwa Mei 2015 na ni moja ya
mafanikio makubwa ya uhifadhi ndani ya
mwongo huu, kwani yatahakikisha tembo wanaishi katika kipindi cha miaka ijayo na hata kuvuka
mipaka.
Aidha kwa upande mwingine
Tanzania na Kenya zinashirikiana mfumo wa ikolojia wa Serengeti-Mara.
Kwa kuzingatia utafiti wa tembo uliofanywa mwaka 2014 mfumo huo wa ikolojia umefanikisha kuongezeka kwa idadi ya tembo
kwa asilimia 98 kutoka mwaka 2009 hadi 2014.
Juhudi za pamoja zikiwemo za kushirikiana kiintelijensia
kati ya Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa) na Huduma ya Wanyama pori ya Kenya
(KWS) kumeonesha mafanikio katika ushirikiano wa kuhifadhi kwenye eneo la
mpakani.
Tembo hawajui mipaka na uhamaji wa wanyama wa Serengeti-Mara
ni dhihirisho la aina yake duniani la uhamaji wa wanyama kwa msimu kutoka nchi
moja kwenda nyingine.
Hata hivyo umekuwepo
uratibu kwenye utekelezaji wa sheria ambapo mashirika ya ndani pamoja na ya
kimataifa yamezidisha kasi ya kufanya kazi pamoja katika kushughulikia na
kufuatilia bidhaa haramu za wanyama pori pamoja na dawa za kulevya.
Polisi wa kimataifa, Kikosi kazi cha makubaliano ya Lusaka
pamoja na mashirika mengine makubwa duniani yamekuwa yakitafuta njia za kufanya
kazi pamoja katika kushughulikia suala la usafirishaji lakini pia kuwafikisha kwenye vyombo vya
sheria wote wanaohusika na ujangili.
Mchango wa mashirika ya utafiti na wanyama pori duniani nao umewezesha kudhibiti shughuli za
ujangili ambapo makundi kama Jumuia ya Kuhifadhi Wanyama pori ya Chuo Kikuu cha Cambridge
yametoa mchango maalum katika kuhifadhi flora na fauna za Afrika kwa ajili ya
kizazi cha leo na kizazi kijacho.
Tafiti zisizoisha
zikiangalia tabia za wanyama, magonjwa yanayoambukiza miongoni mwa wanyama wanaofugwa na wanyama pori kumewezesha
watafiti kusaidia kuhabarisha maamuzi kuhusu uhifadhi endelevu.
Jambo lililo wazi ni kwamba kuhifadhi wanyama pori
kunachangia upatikanaji wa maendeleo na aina ya
uhifadhi wa mafanikio na endelevu utaweza kushughulikia changamoto
zinazohusu masuala ya maendeleo ya watu katika dhana nzima ya kuwalinda wanyama
pori kwa ajili ya utalii na matumizi mengine au uvunaji wa wanyama pori.
Aidha ni muhimu kwamba watafiti wanaendelea kuangalia namna
nzuri ya utendaji ambao jumuia
zinaweza kuangalia faida za uhifadhi
kwenye maeneo yao ili dunia iweze kufanikiwa kwenye kuhifadhi urithi wa wanyama
pori.
Tofauti na nchi nyingine barani Afrika, Tanzania imetenga
asilimia 30 ya ardhi yake kwa ajili ya
hifadhi ya wanyama pori na amana hizi
zimekuwa zinasimamiwa kupitia mfumo
rasmi wa utawala wa taasisi mbalimbali.
CHANZO: TANZANITE


Comments
Post a Comment