Featured Post

MBOWE, WENZAKE KUSOMEWA MASHTAKA SEPTEMBA 27



VIONGOZI tisa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wanaokabiliwa na mashtaka 13, katika kesi ya jinai namba 112 ya mwaka huu kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, watasomewa maelezo ya awali (PH) Septemba 27, mwaka huu akiwemo Freeman Mbowe.

Washtakiwa hao walipaswa kusomewa maelezo hayo na upande wa mashtaka jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri lakini ilishindikana kwa sababu mshtakiwa wa tano, Esther Matiko ambaye mbunge wa Tarime Mjini hakuwepo mahakamani,  mdhamini wake alisema ana tatizo la kiafya kwenye mfumo wa uzazi.
Hata hivyo, Wakili Peter Kibatala anayewatetea washtakiwa hao aliieleza mahakama kuwa mshtakiwa Peter Msigwa ambaye ni Mbunge wa Iringa mjini alikuwa akitetewa na wakili Jeremiah Mtobesya ambaye amejitoa.
Baada ya Kibatala kueleza hayo, mchungaji Msigwa alinyoosha mkono mahakamani hapo na kuieleza mahakama kuwa ana kesi nyingine katika Mahakama ya Iringa kwani muda mwingi yupo katika Mahakama ya Kisutu hivyo aliomba mahakama hiyo iiandikie samasi Mahakama ya Iringa.
Pia mchungaji Msigwa aliomba mahakama impatie muda wa wiki tatu ili aweze kutafuta wakili.
Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ambapo ni Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA Zanzibar, Salum Mwalimu na Naibu Katibu Mkuu Bara ambaye pia ni Mbunge wa Kibamba, John Mnyika, Mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche, Mbunge wa Kawe, Halima Mdee na Mbunge wa Bunda, Esther Bulaya.
Wengine ni Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Msigwa, Mbunge wa Tarime Mjini, Matiko na Katibu Mkuu wa Chama hicho, Dkt. Vincent Mashinji.
Washtakiwa hao kwa pamoja wanakabiliwa na mashtaka 13, ikiwemo kula njama, kufanya mkusanyiko wenye ghasia, kuhamasisha hisia za chuki, kushawishi hali ya kutoridhika, uchochezi, kushawishi utendaji jinai kati ya Februari Mosi na 16, mwaka huu, jijini Dar es Salaam.

Comments