Featured Post

MATAJIRI VISIWANI ZIWA VICTORIA WANAISHI VIBANDA VYA MBAVU ZA MBWA


NA CONGES MRAMBA, MWANZA
ZAIDI ya vibanda 500 vya mabanzi, vilivyokuwa vinatumiwa  na wafanyabiashara kama maduka na makazi, viliteketezwa kwa moto, Sengerema mkoani Mwanza.
Vibanda hivyo vilikuwa vimejengwa kwa mabanzi ya miti, huku vikiwa vimeezekwa kwa karatasi za nailoni na makuti au nyasi, huku mali za thamani kubwa pia ziliteketea.

Aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi, alisema,  zaidi ya vibanda 300 viliteketea kwa moto Juni 30, 2016 majira ya saa 8:00 mchana katika Kisiwa cha Kabiga, Kata ya Maisome, Tarafa ya Kahunda.
Kamanda Msangi alisema, vibanda hivyo vilikuwa vimejengwa kwa mabanzi na miti huku vikiwa vimeezekwa kwa karatasi za nailoni, huku mali za thamani kubwa zikiwemo ndani, ambazo pia ziliungua na kuwa majivu.
Polisi walisema, moto huo uliwashwa na watu wasiofahamika.
Wafanyabiashara wengi wa visiwani wana kawaida kununua mafuta, hususan petroli, wanayotumia katika injini za boti za uvuvi Ziwa Victoria.
Petroli hiyo huwa inahifadhiwa katika mabanda haya wanayoyatumia kama nyumba za kuishi, nyumba za kulala wageni na mabanda ya biashara.
Polisi walisema, siku hiyo ya ajali ya moto, inakisiwa wezi waliiba mafuta, wakawa wanagawana ndani ya moja ya vibanda hivyo.
Kufuatia vibaka hao kugawana petroli jirani na vibanda hivyo, moto ukalipuka. Pengine kuna mtu aliwasha sigara jirani na mahali hapo.
Vibaka hao walitoroka wakawa wanatafutwa na polisi ili wafikishwe mahakamani kujibu mashitaka.
Aidha, siku hiyo hiyo ya Juni 30, 2016, katika kisiwa kidogo cha Migongo huko huko Maisome wilayani Sengerema, vibanda vingine 200 viliteketea kwa moto majira ya saa 4:00 usiku na kusababisha mali za thamani kubwa kuteketea.
Chanzo cha moto huo kilitajwa kuwa ni mshumaa uliounguza makuti.
Wafanyabiashara hawa wanamiliki fedha nyingi, lakini wanaishi katika vibanda hivi vya makuti, huku wakiweka bidhaa za thamani na magudulia yaliyojaa petroli!

HAWAJENGI NYUMBA BORA
Matukio ya moto yamekuwa ya mara kwa mara kutokana na makazi holela katika visiwa hivyo zaidi ya 100 vya Ziwa Victoria katika mikoa ya Kagera, Mwanza, Geita na Mara.
Makazi ya visiwani ambako ardhi ni mchanga, hakuna hata vyoo.
‘Matajiri’ hawa wamekuwa wakienda haja ndogo na kubwa ufukweni mwa Ziwa Victoria.
Kulingana na wataalam wa magonjwa ya milipuko, kipindupindu huanzia visiwani humo kila mwaka na kuua maelfu ya watu.
Hata wanapougua kipindupindu, watu hawa husema kwamba ‘wamerogwa’ na wachawi kwa kutumia uchawi wanaoita, ‘Kadumu’!
Mwaka 2016 walikufa mamia ya wavuvi na wafanyabiashara hawa visiwani humo.
“Wachawi hujaza sumu ya uchawi wao katika galoni (kadumu); halafu uchawi huo humwagwa ziwani au mitoni, mtu akinywa maji, tayari anahara na kutapika!" ndivyo wanavyosema.
Hizo ndizo imani za ‘Matajiri hawa Uchwara’ wa visiwani…na ndiyo chimbuko la uchawi wa ‘Kadumu’ ambao maofisa wa afya wa mikoa ya Mara, Kagera na Mwanza wanaamini ni kipindupindu.
Vifo vya magonjwa ya kuambukiza yatokanayo na ngono zembe (Sexually   Transmitted Diseases) kama Ukimwi, ni ya kawaida sana katika visiwa hivi.
Na mtu akiugua hawezi kutambua kwamba ameambukizwa kutokana na uzembe au kukosa elimu. Atasingizia uchawi na wachawi.
‘Matajiri’ hawa wa visiwani wana imani potofu, ndiyo maana wana fedha lakini hawaachani na mila na desturi za kale zinazorutubisha ushirikina.
Wengine wamepiga ramli na kukatazwa kuishi katika nyumba bora, wengine hawalalii vitanda, na wengine hawavai viatu. Wanaita, ‘ndagu’.
Ndagu hizi hutafutwa kwa njia haramu hata kuua albino na kunyofoa viungo. Hawa ndiyo wenye imani kwamba, sangara akiona nywele za albino katika nyavu, hata akiwa Kisumu nchini Kenya, anakuja kwa kasi na kunasa mtegoni!

UKEREWE
Mfanyabiashara na mkazi wa kitongoji cha Bukini, Kijiji cha Chifule huko Bukungu, Tarafa ya Ukara, Ukerewe alipoteza maisha kufuatia moto mkali kulipuka na kuunguza nyumba nzima, wakati  yeye na mwenzake aitwaye Dotto wakimimina mafuta aina ya petroli.
 Zephania Bitta (42) alikumbwa na mkasa wa kulipukiwa petroli Julai 30, 2016, saa 4:30 asubuhi.
Kamanda wa Msangi, alisema kwamba, marehemu akiwa na mwenzake Dotto, walikuwa wakimimina petroli hiyo kwenye madumu katika chumba cha kulala.
Naam, petroli katika chumba cha kulala!
Ghafla nje akaja mtu aliyekuwa akivuta sigara, moto huo wa sigara ukalipua petroli,  ukaunguza nyumba hiyo na kusababisha watu hao kuungua vibaya!
Kufuatia kuungua kwa nyumba hiyo, thamani ya mali iliyoteketea haikujulikana.
Kufuatia hali hiyo, Kamanda Msangi alitoa rai kwa wakazi wa Ukerewe kuwa macho na kutunza petroli katika nyumba zao za kulala, huku sigara zao zikiwa hazibanduki midomoni, wakipuliza moshi angani mithili ya treni!
Wilaya ya Ukerewe peke yake ina jumla ya visiwa 38.
Mkoa wa Mwanza una visiwa 79. Mikoa ya Mara, Kagera, Simiyu na Geita, hufanya visiwa takriban 100 ambako wanakaa wavuvi hawa wenye imani za kijima.

MATAMBIKO
Hata mitumbwi yao na nyavu hufanywiwa matambiko ili iweze kunasa samaki kwa wingi na kuleta utajiri mkubwa.
Kandoni mwa makazi ya watu hawa, unaweza kukuta vibanda vidogo vya mviringo (tembe) vilivyokandikwa kwa udongo na kuezekwa kwa nyasi.
Humo ndani, ni mahali pa kutambikia mizimu, wao huita “Bhinyasamba”, wanaamini mizimu yao huishi humo, kwa hiyo kila siku wanawaletea mizimu hao kilo nyingi za nyama, ili bahati au baraka isije ikawaacha!
Nataka kusema kwamba, katika visiwa vingi vya Ziwa Victoria ni mahali pa kutambikia mizimu.
Nahodha wa Meli ya Samar II ya jijini Mwanza (jina linahifadhiwa) aliwahi kuniambia kwamba, kina cha maji ya ziwa hili hupungua sana nyakati za kiangazi.
Kufuatia kupungua kwa kina cha maji, basi miamba mingi huzuka ziwani na kuhatarisha meli au boti zinazoweza kukwaa miamba hii na kutoboka.
Mahali pengine meli hizi hushindwa kutembea baada ya nyavu za wavuvi kukusanywa na ‘propellers’ za injini, hivyo meli kulazimika kuzima majini.
Wakati mwingine pia meli au mitumbwi na boti hunasa kwenye tope zito katikati ya ziwa, hasa mpakani mwa nchi tatu za Kenya, Uganda na Tanzania.
Ikitokea meli ikanaswa au ikazima injini, watu hawa huamini ‘imeshikwa na mizimu’, hivyo hulazimika kutambika kwa kujikata vidole ili damu imwagwe ziwani!

MAANA YA MWANZA
Jina la Mwanza limetokana na neno, “Ngwahnzah’au   ‘Mwah-n-zah’, maana yake ni majaruba ya mpunga!
Ni jiji lililojengwa kandoni mwa fukwe za Ziwa Nyanza.
Ziwa Nyanza (Nyanza mana yake Maji Mengi), liliitwa Victoria kwa heshima ya Malkia Victoria wa Uingereza, binti wa Mfalme Edward aliyekuwa mtoto wa nne wa Mfalme George III.
Alitawala kuanzia 1837-1901 aliporithiwa na mwanaye mkubwa, Edward VII.
Aliyeliita ziwa hili kwa jina hili ni John Hanning Speke (miaka ya 1850) alipokuwa akitafuta chimbuko la Mto Nile, ule unaotiririka kuanzia Mto Luvironza, Burundi hapa Afrika Mashariki hadi Bahari ya Mediterranean, umbali zaidi ya kilomita 6,656 kama maili 4,160.
Hivyo, ziwa hili ni kivutio kikubwa cha utalii (tourist site) ambacho kinaweza kuiingizia nchi fedha nyingi za kigeni.
Ziwa hili linaumbwa na maji yanayotiririshwa na mito mikubwa kama Kagera  na Nzoia, hususan nyakati za mvua kubwa za vuli na masika kutoka misitu mbalimbali hapa Afrika Mashariki na Kati.
Hii misitu inayoleta mvua na kujaza ziwa hili sasa inafyekwa kwa kasi ya kutisha.
Ziwa hili huletewa maji na mito mingi midogo kama Simiyu, Duma, Mara na kadhalika kutoka nyanda za juu za miinuko na milima yenye misitu minene.
Ni ziwa la pili kwa kuwa na maji baridi hapa duniani, nyuma ya Superior huko Marekani.
Lina ukubwa wa kilomita  68,000;  kama maili 26,828 na humilikiwa na nchi tatu za Afrika Mashariki ambazo ni Kenya (asilimia 6), Uganda(43%) na Tanzania (51%).
Kina chake ni futi 270, ni kina kifupi sana. Ziwa Tanganyika lina kina cha futi 4,823.
Kuna mnara ambao unaonesha maandishi yanayoeomeka kwamba, mwaka 1858,John Hanning Speke alikuwa Mzungu wa kwanza kuliona Ziwa Victoria akiwa kilima cha Isamilo.
Dk. Speke alikuwa akipeleleza chanzo cha Mto Nile, na aliyaita maji haya ya Ziwa Nyanza maana yake Maji 'Inyanja' kwa Wakerewe na Wajita, na 'Lweru' kwa Wahaya, kwa heshima ya Malkia wa Uingereza, Victoria.
Jiji la Mwanza linatambulishwa na mawe haya yaliyobebana yanayoitwa, Bismarck ama Bismarck Rock, yaliyoko katika fukwe za Ziwa Victoria.
Mawe haya yamepewa jina la aliyekuwa Chancellor wa Ujerumani, Chancellor Bismarck miaka ya 1880.
Mahali pengine mawe haya huabudiwa. Kuna mawe Ukara wanasema yanacheza dansi (The Dancing Rock), na mengine yapo visiwa vya Irugwa.
Mamilioni ya watu katika nchi hizi hulitegemea ziwa hilo kwa maji ya kunywa, chakula, usafiri na usafirishaji wa mizigo na abiria - nazungumzia mchango wa Ziwa Victoria katika uchumi wa wakazi wanaolizunguka na uchumi wa taifa kwa ujumla.
Uchumi wa wakazi wa ufuo wa ziwa hili hutegemea uvuvi wa samaki ili kujipatia chakula chao (samaki ni chanzo cha protini nyingi) na mahitaji mengine muhimu ya kiuchumi.
Mazao na shehena nyingine hutegemea ziwa hilo kusafirishwa kwenda viwandani, ng’ambo au kutoka sokoni.
Rwanda, Kenya, Tanzania, Uganda na kadhalika hutegemea ziwa hili kusafirishia shehena ya mazao au bidhaa nyingine.

TOPE
Mito kama Simiyu na Duma imegeuka kuwa kitisho kwa uhai wa Ziwa Victoria.
Mito hii huingiza ziwani asilimia 40 ya kiasi cha tope zote zinazoingizwa nyakati za mvua.
Tope zinapojazwa ziwani kutoka nchi kavu husababisha kina cha ziwa kupungua kila mwaka.
Tope zikijaa ziwani wenyeji wakiona mitumbwi imenaswa, wanasema wameshikiliwa na mizimu.
Kina cha ziwa kinapopungua huleta athari nyingi ikiwa ni pamoja na uharibifu wa mazalia ya samaki, kuongezeka kwa gugu maji (water hyacinth) linaloondoa oksijen kwa viumbe wa majini.
Adui wa kwanza wa Ziwa Victoria ni kilimo ndani ya mita 60 kutoka mito inayomwaga maji yake ziwa hili, kinacholeta mmomonyoko wa udongo baada ya misitu kufyekwa kwa ajili ya upanuzi wa mashamba.
Adui namba moja wa Ziwa Victoria ni wananchi wanaoendesha kilimo ndani ya eneo la mita 60 kutoka ziwa lenyewe kama barabara ya Makongoro jijini Mwanza, na kando ya mito mikubwa kama Simiyu, Duma, Kagera, Nzoiya na kadhalika.
Inadaiwa, ziwa hili liliwahi kukauka miaka mamilioni yaliyopita, ingawa Biblia inasisitiza dunia ina umri wa miaka zaidi kidogo ya 6,000 tu tangu kuumbwa na Yehovah.
Kwa kipindi cha kati ya mwaka 1998 na 2006, maji ya Ziwa Victoria yalipungua kutoka mita 1,141.24 juu ya usawa wa bahari hadi mita 1,139.20.
Upungufu huu ulikuwa wa wastani wa mita 2.04.
Kufuatia hali hiyo, hata meli zimekuwa zikishindwa kutia nanga bandarini hususan huko Nansio, Ukerewe, na meli zinakuwa hatarini kuparamia miamba na kupasuka kufuatia kuzuka kwa miamba.
Hali hii ni hatari kwa maisha ya abiria na mizigo yenye thamani ya mamilioni ya fedha.

JIJI LA MWANZA
Kilomita za eneo 425 ndizo nchi kavu na eneo lililobaki ni maji ya Ziwa Victoria.
Hali ya hewa hapa ni joto; nyuzi joto kati ya 25 C hadi 30.2 nyakati za hari.
Wakati wa baridi hali ya hewa huwa nyuzi joto 15.4 hadi 18.6 C, na wastani wa mvua kwa mwaka ni 700-1,000 mm hasa mvua  za vuli hunyesha hapa kati ya Oktoba na Desemba na masika ni Aprili hadi Mei.

MINYOO NA KICHOCHO
Kulingana na Shirika la Afya la Umoja wa Mataifa (WHO) asilimia 25 ya watu wanaoathiriwa na sumu hapa duniani ni wale waliokula sumu hizo kupitia maji ya kunywa.
Hata wana minyoo na kichocho. Wakivimba matumbo, utasikia wanasema, “Wachawi wamewatega uchawi kwenye viti vya kienyeji!”
Kwa lugha za wenyeji, ukiwa na kitambi cha minyoo, wanasema ‘Bhamamulisya!” yaani amelishwa uganga, uchawi, mabhugota!
Asilimia takriban 80 ya wakazi wa Mwanza  na maeneo haya ya visiwa, wana kichocho, minyoo, safura na wanahara na kutapika (kipindupindu) kufuatia uchafu na hujuma wanayolifanyia ziwa hili muhimu kwa maisha yao.
CHANZO: FAHARI YETU


Comments