- Get link
- X
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- X
- Other Apps
NA ALOYCE NDELEIO
UTANDAWAZI unalenga kuiweka dunia kwa ukaribu na kuifanya
kama kijiji na hata hivyo hali hiyo haijaleta ufanisi kwa jumuia za wakulima
wadogo na hususan kwa nchi zinzoendelea kutokana na kukabiliwa na vikwazo
kadhaa.
Miongoni mwa vikwazo hivyo ni pamoja na kukosekana au
kushindwa kupatikana kwa habari iwe za kuchapishwa au kutangazwa, umaskini
ambao unakuwa hauruhusu kuwa na uwezo wa kununua vyombo vya kisasa kama vile
televisheni, redio, kompyuta n.k ambavyo vitawawezesha kunufaika na utandawazi.
Aidha, kukosekana kwa miundombinu ya msingi kama vile kuwepo
kwa umeme wa uhakika na njia nyingine za mawasiliano nako kunawaathiri
wakulima.
Vikwazo wanavyokabiliwa navyo jamii ya wakulima pia
vinawanafanya washindwe kufikia ugunduzi au ubunifu wa mbinu mbalimbali za
kilimo.
Utandawazi unatafsiriwa kuwa ni kuongezeka kuunganika kwa
dunia, kufungamana na kutegemeana katika nyanja za kiuchumi, kisiasa, kijamii,
kiteknolojia, kiutamaduni, kisiasa na kiikolojia.
Kwa mujibu wa Benki ya Dunia faida zinazotokana na
utandawazi zinajumuisha kukua kwa uchumi, kuboresha viwango vya maisha,
kupunguza umaskini, kuongeza kiwango cha kuishi na kukua kwa uhuru wa
kidemokrasia.
Kutokana na mtazamo huo ni wazi kuwa utandawazi unajumuisha
nyanja tofauti za shughuli za binadamu na mojawapo ni suala la uhakika au
usalama wa chakula duniani.
Kwa mujibu wa Kamati ya Uhakika wa Chakula ya Shirika la
Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa (FAO) inabainishwa, “Uhakika wa chakula
unamaanisha chakula kinakuwepo muda wote hivyo kwamba watu wote wanakipata au
kukifikia kikiwa na virutubisho vya kutosha katika nyanja ya ubora, wingi na
aina tofauti na kwamba kinapatikana katika utamaduni unaokubalika.
“Aidha ni wakati ambapo hali zote hizo zinapokuwepo ndipo
idadi ya watu inaweza kuelezwa kuwa ina usalama wa chakula. Lengo ni
kujitegemea katika ngazi ya kitaifa na kaya. Katika kufanikisha huko mikakati
ni lazima iwe kwenye misingi ya kanuni za kiuchumi, usawa, ushiriki kwa upana
na matumizi endelevu ya maliasili.”
Hata hivyo kumekuwepo tishio dhidi ya uhakika wa chakula
duniani kutokana na kushuka kwa uzalishaji wa chakula. Uhakika wa chakula ni
mtazamo mkubwa wa utandawazi.
Ili kuwa na tija kwenye utoaji wa ongezeko la chakula,
utandawazi umekuwa unakuza na kuhimiza biashara huria ambayo itahakikisha
kuongezeka kwa ufanisi na kuboresha mazingira ya kiuchumi ya wakulima.
Inatarajiwa kuwa biashara huria inaweza kutoa fursa za
kuongezeka kwa bei za mazao ya kilimo, kukuza hali ya kiuchumi ya wakulima, na
kuboresha nyanja za utumiaji wa chakula.
Tanzania kwa upande wake ndani ya mazingira hayo Agosti
2009, Serikali ilisema, “... lipo suala zima la kuimarisha masoko ya mazao ili
mkulima apate soko la uhakika na bei zenye tija kulingana na jasho lake.
“Kipimo cha mafanikio yetu kama taifa katika kufuta umaskini
nchini kinategemea kilimo cha kisasa na cha kibiashara na sekta ya viwanda
inayohudumia kilimo na kukuza ushindani wa Tanzania katika soko la dunia la
utandawazi.”
Upatikanaji wa habari na ubunifu au ugunduzi unaohusiana na
utendaji wa kilimo kwa wakulima wengi ni mdogo. Wakulima hutegemea maofisa
ugani ambao wanakutana nao uso kwa uso ili kupata habari zinazohusiana na
kilimo.
Kwa bahati mbaya idadi ya maofisa ugani ni ndogo hivyo
inakuwa vigumu kwa wakulima kupata habari mpya kwani uwiano kati ya maofisa
ugani na wakulima upo chini.
Kilimo, utandawazi na
kuhabarishwa
Inatarajiwa kuwa utandawazi utapunguza uhaba wa chakula
Afrika hivyo kujenga uhakika wa chakula kwa misingi ya faida linganifu.
Hali kadhalika inatarajiwa kuwa taifa linatakiwa kuzalisha
mazao ambayo kwayo yana faida linganifu na itaagiza kutoka nje mazao ambayo
haliwezi kuyazalisha kwa ufanisi kutoka kwenye nchi ambako mazao hayo yanaweza
kuzalishwa kwa bei rahisi.
Utandawazi pia unaboresha kuunganishwa kwa mashamba madogo
ya kilimo kwenye mashamba makubwa yanayotumika kilimo cha mashine. Dhana
nyingine ni biashara huria na kuondoa ruzuku kwenye pembejeo kama vile mbolea
za chumvi chumvi.
Ili kunufaika na utandawazi nchi nyingi zinazoendelea
zimejiunga na Makubaliano ya Pamoja ya Biashara na Ushuru (GATT) na Shirika la
Biashara Duniani (WTO). Katika mazingira hayo nchi nyingi za Afrika
zimeshahurisha biashara ili kuweza kuuza bidhaa nyingi za kilimo.
Matokeo ya hali hiyo wakulima wengi wameacha kilimo cha
mazao ya chakula na kuingia kwenye mazao ya biashara ambayo yatawawezesha
kupata fedha nyingi kutoka kwenye soko la dunia. Hali hiyo ni tishio kwa
uhakika wa chakula.
Kufungamanishwa kwa mashamba madogo ya kilimo kwenye kilimo
cha mashine cha mashamba makubwa hakujawa na ufanisi kutokana na umiliki wa
kina na wenye nguvu wa ardhi kwa wakazi wa Afrika.
Mtazamo huo unawezekana kuwa unatokana na kutoelewa faida
zinazoweza kupatikana ambazo zitatoka kwenye kufungamana kwa sekta ya mashamba
madogo na mashamba makubwa yanayoendeshwa kwa kilimo cha kutumia mashine.
Jambo jingine linalochangia ni uwezo mdogo wa kifedha
miongoni mwa wakulima wengi wa Afrika wa kununua pembejeo za kilimo ambazo
zingewawezesha kuongeza kasi ya uzalishaji wa chakula, hivyo serikali kuondoa
ruzuku kwenye pembejeo za kilimo kumesababisha wakulima wengi kuachana na
kilimo.
Sababu zote hizo kwa pamoja zinafanya uzalishaji kwenye
kilimo kupungua. Hali kadhalika utandawazi unatarajiwa kutoa ufanisi na habari
za papo hapo kwa shughuli yoyote.
Kutokana na hali hiyo inatarajiwa kuwa wakulima wadogo
wataweza kupata ubunifu wa karibuni kuhusu shughuli za kilimo. Mchango wa Vituo
vya Habari kwa wakulima vinatakiwa kutoa
habari za mara kwa mara kwa wakulima ili kuwajenga ufahamu mpana kwa kuzingatia
kuwepo kwa kiwango kikubwa cha kutojua kusoma, tofauti za kiutamaduni na
kukosekana kwa teknolojia.
Kwa mujibu wa Griffith na Smith kwenye mada iliyochapishwa
kwenye Jarida la Academic Librarianship kuhusu Sera ya habari wanaelezea suala
la habari duniani kuwa ni miundombinu ya simu ambayo inaunganisha kaya,
shughuli za biashara, mashule, hospitali, maktaba vikiunganishwa pamoja na
vyanzo kadhaa vya habari vya elektroniki.
Katika mazingira hayo miundo mbinu ya simu inajumuisha
sehemu muhimu ya habari duniani.
Kwa mujibu wa Takwimu za Intaneti Duniani za mwaka 2006
Afrika ilikuwa na watumiaji wa simu milioni 33 ikilinganishwa na Ulaya ambako
kulikuwa na watumiaji milioni 315 wakati Amerika ya Kaskazini ilikuwa na watumiaji
milioni 233 na Asia ikiwa na watumiaji milioni 399.
Wakati Afrika ikiwa na asilimia 14.2 ya idadi ya watu
duniani ina asilimia 3.0 ya watumaiji wa intaneti na hata hivyo kiwango chake
cha kukua kwa matumizi hayo kati ya mwaka 2000 na 2007 kilikuwa ni kwa asilimia
638.4.
Kutokana na hali hiyo inatarajiwa kuwa matumizi ya intaneti
yanaweza kupanuliwa hadi maeneo ya vijijini ambako ndiko makazi ya wakulima.
Hakuna shaka kwamba kuna pengo kubwa la teknolojia kati ya
maeneo ya vijijini na mijini barani, lakini kusogezwa kwa mawasiliano ya simu
kwenye maeneo hayo kunawezekana kama juhudi zitafanyika kuendeleza miundombinu
ya mawasiliano vijijini.
Wakulima watanufaika kutokana na habari za dunia kama vituo
vya habari vitakuwa vipo maeneo ya vijijini vikiwa na vifaa vyote vya habari na
mawasiliano. Vifaa hivyo ni pamoja na kompyuta zilizounganishwa na intaneti,
mitandao ya karibu na mipana, redio na televisheni, simu, mashine za nukushi,
video na mashine za kurekodia.
Vituo kama hivyo vitatoa habari au vitahabarisha wakulima na
inatarajiwa kuwa vituo hivyo vitatoa mafunzo kwa watalaamu wa masuala la
maktaba na sayansi ya habari ambao watakuwa na jukumu la kukusanya habari
sahihi kutoka kwenye intaneti, wizara husika za kilimo na mashirika
yanayojihusisha na kilimo.
Aidha habari hizo zinatakiwa kurahisishwa na kuwa katika
mazingira ambayo yanaweza kufikiwa na wakulima wasiojua kusoma. Vituo hivyo
vinaweza pia kuwa na filamu au CD, kanda za kaseti zote zikilenga kuonesha
uendeshaji wa kilimo cha kisasa kwenye maeneo mengine.
Pindi wanapoona vipindi vya aina hiyo wanaweza kutafsiri
kile wanachojifunza kwa kuona na kukitekeleza kwa vitendo kwenye maeneo yao.
Licha ya kwamba kumekuwepo ukosoaji kuhusu utandawazi kwa
upande mmoja kwamba hauna faida au haunufaishi Afrika lakini kwa upande
mwingine kuna mambo yanayoweza kuwanufaisha wakulima wa Afrika kama kila mdau
atatoa mchango wake.
CHANZO: FAHARI YETU




Comments
Post a Comment