Featured Post

KAULI ZA WALIOONJA MVINYO NI ZA KWELI



NA ALOYCE NDELEIO
Mara nyingi watu wanapokuwa wamepiga kinywaji na kikawaingia kama mpo kwenye mazungumzo jua yote yatakayozungumzwa yatakuwa na ukweli ndani yake kwa asilimia zote.
Kutokana na hali hiyo  upo msemo mmoja wa lugha ya Kilatini  unaosema  ‘In vino veritas’ ambao kwa tafsiri rahisi ‘Ndani ya mvinyo kuna ukweli’ kwa maana kwamba ni vigumu kwa mtu aliyekwishapata kilevi kusema uongo.
Mara nyingi watu wa rika la kati walipokuwa wanataka kupata wosia au busara  kutoka kwa wazee wenye umri mkubwa  wengi walikuwa wanawanunulia kinywaji na hapo simulizi zilikuwa zinatolewa kwa mtiririko hivyo kwamba kinywaji ndicho kinakuwa kimemrubuni mkongwe huyo.

Lakini mvinyo hapo unaweza kuwa ni kiashiria na kiwakilishi cha kitu chochote kile ambacho kinaweza kumfurahisha au kinachoweza kutumika kumrubuni ili kupata kitu au jambo fulani.
Mfano wajukuu wengi kwenye familia za ki-Afrika  ambazo zimezama kwenye utamaduni na mila (sio familia nyingi za sasa zilizosombwa utapiamlo wa kiutamaduni kwa kubugia utandawazi) wamekuwa wakizawadiwa mali na babu zao kutokana na  kufurahishwa na zawadi ambazo wamekuwa wakipata kutoka kwao.
Madaraka au mamlaka yanaweza kuwa kama mvinyo wenye kulevya na hivyo kuwafanya waliopewa madaraka hayo kulemaa na kutoa kauli ambazo kwao wanaziona ni sahihi lakini kwa upande mwingine zinaonekana kuwa sivyo.
Lakini baadaye inaweza kubainika kuwa hiyo ndio kweli aliyoisema na aliisema akiwa amedhamiria.
Inapotokea kwamba mzito anatoa kauli kwamba hakuna Mtanzania mwenye uwezo wa kuwekeza kwenye uchimbaji wa gesi asilia na kwamba kampuni zao  zina uwezo wa kusindika juisi moja kwa moja anaonesha kulewa mvinyo wa madaraka ambapo mara nyingi huishia kudharau hata kule walikotoka.
Hali hiyo inamaanisha kuwa ile dhana ambayo inaelezwa na wataalamu wa sayansi ya siasa kwamba tumekuwa tunajianika uchi kwa kufanya uza uza ya kila kitu hapa ina mashiko.
Aidha ile dhana kwamba kasi ya uwekezaji ni kwa wawekezaji wa nje hapa nayo inajidhihirisha. Mazingira ya aina hiyo inaonesha  ni jinsi gani na kwa namna gani jamii itakavyokuwa wasindikizaji kwenye  kuzionja tamu za rasilimali zilizopo nchini.
Kama hali ndio hivyo leo hii hakuna cha kushangaza kuhusu utajiri wa baadhi ya wazito kwani hayo ni matokeo ya mambo ambayo Mwalimu Julius Nyerere aliyazuia sana wakati wa uongozi wake (1962 – 1985).
Mwalimu aliita “miujiza” ya aina hiyo ni “ulevi wa madaraka” na ni matokeo ya Azimio la Zanzibar (1992) lililofuta Miiko ya Uongozi katika Azimio la Arusha (1967).
Pia ni matokeo halisi ya yale yanayoelezwa na taasisi ya kimataifa iitwayo Transparency International (TI) kwa Kiingereza kuwa ni “Grand Corruption” yaani “Rushwa Kabambe” au ufisadi kwa neno maarufu lililokita ndani ya jamii hivi sasa.
TI imeeleza rushwa kabambe kwa Kiingereza kuwa ni: “Misuse of entrusted power for private gain”. Tafsiri yake: “Matumizi mabaya ya madaraka kwa maslahi binafsi”.
Haieleweki ni kwanini watu wanashangaa leo kuhusu taarifa kwamba kuna watu walioficha fedha nje ya nchi na kuibuka kwa kebehi za kuzitaja fedha hizo kwamba ni vijisenti.
Haiyumkini kwamba kujishangaa huko kunatokana na kuwapa madaraka makubwa na badala ya kuitumikia jamii wamekuwa wanajitumia wao wenyewe kwa maslahi yao. 
Kwenye kumbukumbu za Bunge kuhusu hoja ya rasilimali  Mbunge wa Bariadi Magharibi Februari 12, 2004 akiwa Dodoma alisema,  “Niseme tu hapa Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu ina utajiri mkubwa sana wa madini. Kwa taarifa tu za utafiti uliofanywa, mkienda hapa Ofisi yetu ya Madini hapa, ukiomba wakuonyeshe ‘geological data’ iliyopo kwa nchi nzima, utasema kweli tunachofanya sasa hivi ni kidogo mno.
“Lakini narudia kwamba Watanzania hatuwezi kuendelea kila siku tunasema, tuna potential nzuri sana. Hatuwezi kuishi kwa kula potential. Madini haya lazima tuyatafute kokote yalipo, tuyapate, tuyachimbue, tuyasafishe, tuya-process na kisha tuweze kuyauza na tutumie mafao yanayotokana na mauzo hayo kwa faida ya maendeleo ya nchi yetu na watu wake....
“Lakini madini yaliyopo siyo madini ya dhahabu peke yake au almasi au vito, yapo madini mengi sana, madini ya vyuma, mkaa wa mawe na odium, unaweza kusema uranium na mengine yote mpaka kule maeneo ambayo yana madini mengi tunayafahamu lakini kwa leo mimi nasema tunaboresha maeneo haya...”
Kwa nukuu hiyo ni dhahiri kwamba rasilimali zilizopo nchini thamani yake inapanda kila siku kutokana na kugundulika kuwepo kwa kiwango kikubwa. Kimsingi madini hayo hayaozi.
Ardhi nayo haionekani kuwa nzuri kwa kilimo kama ambavyo ingetarajiwa lakini kwa kuwa wageni wanaona utajiri wa rasilimali hiyo kwenye uzalishaji wa mazao na hususani kwa kutumia kilimo cha umwagiliaji na kwamba mazao yanaweza kuzalishwa mwaka mzima wapanga sera nao wamekuwa wanadanganyika kwa kuwapa maeneo makubwa kwa ajili ya uwekezaji.
Katika mazingira hayo ni wazi kuwa haitashangaza kuona kuwa hata huduma na bidhaa ambazo zitakuwa zinazalishwa kutokana na uwekezaji huo hapo baadaye na hata zitakazokuwa zinabakia ndani kwamba zitaangukia mikononi mwa watu wasio wazawa au mikononi mwa tabaka la walioonja pepo.
Ukweli unabakia kuwa ili kuelewa hali halisi ya uchumi wa nchi hii ni vyema kufahamu ni kwanini tuna uelewa duni wa utambuzi kuhusu umuhimu wa rasilimali za asili na pia inatakiwa kufahamu ni kwanini sehemu  kubwa ya utajiri huo unaangukia kwenye mikono wageni ambao kwa ujumla wanaishi nje ughaibuni.
Katika kurejea kwenye historia ni kwamba tangu zamani ndani ya jamii  walikuwepo wanajeolojia ambao walikuwa wanafahamu miamba iliyokuwa na dhahabu pamoja na shaba.
Wakati wazungu wanafika kwenye karne ya 19 waligundua kuwa miamba yote iliyokuwa shaba au dhahabu ilikuwa imeshachimbwa na wajamii japo sio kwa kiwango kikubwa kama ambavyo wazungu walifanya kwa kutumia zana zao za kisasa.
Katika mazingira hayo kinachojitokeza hivi sasa ni kuona kuwa wazawa kwamba hawana uwezo  ni hatua ya marudio ya kihistoria kwamba wawekezaji wa nje ndio wanaoweza tu.
Aidha hali hiyo tayari inaonesha ni jinsi gani wapanga sera wetu jinsi ambavyo fikra zao zimeshatekwa au kuuzwa ughaibuni.
Haiyumkini kwamba ni vyema kuchukulia kauli za wataalamu wa masuala ya maendeleo na uchumi kwamba bara la Afrika ndilo litakalokuja kuchipukia  na kuongoza kwa maendeleo kwa kuwa rasilimali zake nyingi hazijaguswa.
Kauli hiyo inamaanisha rasilimali hizo ziondoe umaskini wa watu wake ndipo maendeleo hayo yatapatikana. Lakini kwa upande mwingine  hao wawekezaji kutoka nje nao walishaliona hilo na ndio maana  kila mahali zinapoibuliwa rasilimali huanza kupigana kumbo kwenda kuwekeza na wanapoingia na kuwakuta watu wake wamejilegeza basi huutumiwa mwanya huo vizuri kupoka rasilimali hizo.
Lakini ni vyema ikiwa wapanga sera watabaini kuwa mamlaka yao wameyatumia vibaya wakaja baadae na msemo huu wa kilatini mea culpa, mea culpa, mea maxima culpa” kwamba “nimekosa mimi, nimekosa mimi, nimekosa sana”.
CHANZO: FAHARI YETU

Comments