Featured Post

KATIBU MUENEZI WA KATA YA MASEKELO CHADEMA NA WANACHAMA WA CHAMA HICHO ZAIDI YA 500 WAHAMIA CCM



Mwandishi Wetu, Shinyanga
ZAIDI ya 500 wa chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Kata ya Masekelo Manispaa ya Shinyanga akiwemo katibu mwenezi wa kata hiyo wamehamia Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa kile walichodai wananyimwa uhuru na viongozi wa Chama hicho ngazi ya juu.

Wanachama hao ambao walikuwa wamesimika mizizi katika kata hiyo na kuisababishia kata hiyo kuchukua nafasi zote kuanzia ngazi ya kijiji hadi kata wametambulishwa jana kwenye mkutano wa hadhara kilichofanyika kata na kusema kuwa walipokuwa kwenye chama hicho walinyimwa uhuru  na kupewa masimango .
Wamesema baada ya kukisababishia ushindi chama hicho ngazi zote wamedharauliwa na kugeuzwa kuwa madaraja na kupewa masimango na viongozi wa ngazi za juu hali ambayo wamedai wameshindwa kuvumilia wameamua kurudi CCM kwenye Chama cha wakarimu.
Akizungumza kwenye kikao hicho aliyekuwa muenezi wa kata Chadema Jastin Mwasiga alisema ameamua kuhama chama kwa sababu chama chake kimemnyima uhuru,  kina masimango na unyanyasaji mkubwa hivyo ameona ahamie chama cha CCM cha watu wakarimu.
"Kwa kweli mimi binafsi nimeamua kuhamia CCM kwa sababu chadema tumegeuka madaraja ya kuvukia hatuthaminiwi na huku ndiyo tulisaidia viongozi wote kuanzia kwa mwenyekiti wa serikali za mitaa mpaka kwa diwani, tukapata ushindi mkubwa"alisema Mwasiga.
"Kwa kweli mimi nilisaidia sana kupata ushindi chadema lakini viongozi hawakulitambua hilo  nimenyanyasika sana na nimevumilia sana na sasa nimechoka nimeona  nirudi CCM tushirikiane kupata ushindi naamini awamu hii Masekelo itachukua nafasi zote kwa sababu najua mbinu za ushindi tutashirikiana kwa pamoja kuanzia leo uenezi wangu wa chadema umekoma"aliongeza.
Hamza Hamis ambaye alikuwa mwanachama wa Chadema amesema ameamua kurudi CCM kwa kuwa chama hicho kilikua cha wazazi wake, kwani ameona kinafaa tofauti na chadema alikokimbilia bila kujua kama kuna matatizo au kuna unyanyasaji wa kuburuzwa.
Kwa upande wake katibu muenezi wa kata hiyo Mashimba Kadama aliwataka wanachama wa CCM wasikae wakajisahau kwa kujua kwamba chadema imeisha,  lengo la kila mwanachama alete  wanachama wajiunge na CCM na kuirudisha kata iliyochukuliwa na wapinzani.
"Wanachama wenzangu tusikae tukajisahau kwa kusema chadema imeisha tunatakiwa kuhakikisha wameisha kabisa hata mmoja, kwa mfano unaweza ukauwa nyoka lakini bila kumsigina kwenye kichwa atakuwa hajafa hivyo tunatakiwa kuwasigina kabisa hadi kichwa tuhakikishe hapa masekelo hawapo wapinzani"alisema Kadama.
Naye katibu wa CCM kata Petro Kolimba alisema wamefurahi kwa kujiunga kwa hao wanachama kwa nyakati tofauti kwa sababu wamegundua nyubani kuna ukarimu wanakaribishwa na sasa waliorudi CCM kutoka vyama vya upinzani ndani ya miezi sita ni zaidi ya 500 awali walikuwa wanachama 950.

Comments