Featured Post

KANUNI MWENDO YA NEWTON INASADIFU KUHUDUMIA UMMA


  

NA ALOYCE NDELEIO
Yeyote yule aliyesoma somo la Fizikia lazima akubali kuwaalikutana na majina  ya wanasayansi wa mwanzo kabisa na ambao wameuweka uhai wa somo hilo katika duniani hii na miongoni mwa wanasayansi hao ni Isaac Newton.
Newton katika maisha yake alivumbua kanuni mwendo tatu lakini ambayo  imekuwa ikiegemea au kupenyeza katika nyanja nyingine ambayo ni kanuni  mwendo ya tatu.

Kwa lugha ya Kiingereza inasema, “Action and reaction are equal and opposite in direction” au  “ For every action, there is an equal and opposite reaction” ambayo kwa tafsiri isiyo rasmi ni 'Kila tendo na mjibizo wake huwa na nguvu sawa na mwelekeo tofauti'.
Kinachozungumzwa hapo ni mwendo na nyanja inayohusiana na shughuli za kisayansi na hususan kwenye nyanja ya Fizikia lakini mwendo huo pia unaweza kuingiza kwenye maisha ya kila siku ya mienendo mingine ya maisha ya jamii kiuchumi kisiasa na kijamii.
Katika uwanja wa siasa kumekuwepo shughuli au mienendo mingi na hususan tangu kuingia kwa mfumo wa siasa za vyama vingi hapa nchini na hadi sasa ni zaidi ya miaka 17 chaguzi zilipoanza kuhusisha vyama vingi vya siasa.
Ukiondoa uchaguzi wa kwanza uliofanyika mwaka 1995 uchaguzi wa mwaka 2010  unaweza kuelezwa kuwa ulikuwa na ukinzani mkubwa ikilinganishwa na chaguzi nyingine za mwaka 2000 na 2005.
Kimsingi hapa ni kuibuka kwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ambacho kilizoa majimbo mengi na hata kuwaangusha baadhi ya wakongwe waliogombea kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Lakini jambo jingine lililojidhihirisha ndani ya chama hicho ni kutoa fursa kwa vijana ambao waligombea kwenye majimbo na kupata ushindi wa kishindo ndani ya majimbo hayo.
Chadema baada ya uchaguzi kimepata fursa ya kuunda Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni ambapo kiongozi wake ni mwenyekiti wa chama  hicho na Mbunge wa Jimbo la Hai, Freeman Mbowe.
Katika mazingira hayo ni kwamba Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linajumuisha kambi mbili za chama tawala na kambi ya upinzani.
Hivyo kila kambi inawajibika kuhakikisha kuwa kile inachokisema  kina manufaa kwa jamii kwa sababu pande zote zinawakilisha wananchi ambao ni walipa kodi.
Kila upade umekuwa ukiwakilisha hoja zake au matakwa yake yanayolenga kuleta maendeleo kwa wananchi katika kile kinachofahamika kama ilani za vyama.
Hakuna hoja ambazo zimekuwa zikiwakilishwa zikiwa kinyuime na mahitaji ya jamii ila katika utekelezaji chama kilicho madarakani ndicho kimekuwa na jukumu la kushika usukani.
Hata hivyo umekuwepo udhanifu kuwa hoja au maoni yanayotolew ana kambi ya upinzai yamekuwa hayatekelezwi na kwamba kinachotekelezwa ni hoja za upande mmoja wa chama tawala tu.
Udhanifu huo si sahihi kwani kila jambo ambalo limekuwa likifanyika halijatoka upande mmoja tu bali ni kutoka pande zote.
Rejea zinaweza kuwa katika kampeni za uchaguzi ambapo suala la elimu bure lilikuwa limeelezwa na na vyama vyote na hata hivyo limetekelezwa na serikali iliyopo madarakani.
Jingine ni kufufua baadhi ya taasisi zilizokuwa zimedhoofu au kufa ili ziweze kutumika kwa manufaa ya umma wote. Mfano ni kulifufua  Shirika l ndege Tanzania ATCL ambalo limepewa kipaumbele na uongozi wa Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli  ikiwa ni pamoja na kununua ndege za bombardier na ndege kubwa ya Dreamliner 787.
Yapo mambo mengi zikiwepo huduma za jamii kuanzia maji,  sekta za kilimo, mifugo, maliasili, miundombinu, uvuvi na madini.
Hata hivyo katika eneo ambalo limekuwa likipigiwa kelele ni suala la kodi nalo ndilo lililopewa kipaumbele kikubwa na hata  kuongeza chachu katikauwajibikaji  jambo ambalo limeonesha kuwepo kwa ufanisi.
Lakini jambo moja ambalo limekuwa likipiga kelele zaidi ni kutowajibika kwa baadhi ya watendaji wa serikali ambako kulikuwa kunaisababishia  serikali hasara.
Katika eneo hilo kumekuwepo kuwajibishwa kwa viongozi ambako kumejipatia msamiati wa utumbuaji wa majibu.
Lakini bila kuegemea upande wowote kinachojidhihirisha ni kwamba  mlengwa katika  hoja zinazotolewa na pande zote ni mwananchi bila kuangalia masuala ya itikadi.
Hata kama ilani inayotekelezwa ni ya chama kilichopo madarakani na hata kama inadaiwa kuwa chama kilichopo madarakani kinatekeleza moja ya ilani iliyokuwa ya chama kingine hiyo haiwezi kuwa ni hoja.
Hoja ni kwamba kinachotekelezwa kinakidhi maslahi ya umma wote bila kujali chimbuko la ilani ni sehemu gani.
Hali hiyo inayoweza kuwa ni udhanifu imekuwa haiangalii kwamba mambo yanafanyika kwa kuzingatia fikra za watu pamoja na tathmini za kujenga kwa maslahi mapana.
Kama jambo linakidhi matakwa ya umma na limetoka  upande usio na mamlaka ya kiutendaji na kwamba mamlaka hiyo imelitohoa, na kuliingiza katika utekelezaji  kwa kuwa ni jema inasadifu kuwa kuna kutegemea katika kauli zenye manufaa kwa umma.
Hapo ndipo kauli mwendo ya Newton inaingia kwamba pande zote zina mchango katika kushughulikia maslahi ya umma licha ya kwamba zipo tofauti za kiitikadi au mwelekeo baina yake.
Kinachofanya hali hiyo isionekane mara nyingi ni mtazamo unaofanyika katika misingi ya propaganda unaokuwa umeegemea upande mmoja. Hilo ni sawa kwani kwa mtazamo huo  ni miongoni mwa mikakati inayolenga kujiimarisha.
Lakini ufanisi unapochukuliwa kwa mtazamo wa kanuni mwendo ya Newton, haiyumkini taswira itakayojengeka ni kwamba, pande zote ni washirika katika utekelezaji wa mahitaji kama si matakwa ya jamii.
Pamoja na hali yote hiyo ni wazi kuwa utekelezaji wa ilani hakuna hata moja ambayo inaweza kuelezwa kuwa ni kikwazo katika mikakati yote ya maendeleo.
Kama kuna fikra za aina hiyo inasadifu kusema ni fikra mfu.
Hali hiyo inamaanisha kuwa kanuni mwendo ya Newton katika mwenendo mzima wa ulingo wa siasa ni wazi 'Kila tendo na mwitiko wake huwa na nguvu sawa lakini mwelekeo huwa ni tofauti’
CHANZO: TANZANITE

Comments