Featured Post

H/SHAURI RUNGWE YAAGIZWA KUREJESHA MILIONI 438.6/-



NA MWANDISHI WETU, DODOMA
HALMASHAURI ya Rungwe, mkoani Mbeya, imeagizwa kurejesha sh. milioni 438.6 ambazo walitumia kinyume na utaratibu kwa kujenga maabara ya shule za sekondari.
Maagizo hayo yalitolewa jijini Dodoma jana na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), Abdallah Chikota.
Alitoa agizo hilo baada ya kamati yake kufanya mahojiano na halmashauri hiyo kuhusu hoja za ukaguzi za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka wa fedha 2016/17.

Chikota ambaye pia ni Mbunge wa Nanyamba (CCM), alisema fedha hizo zilikuwa kwa ajili ya kulipa wakandarasi waliokuwa wakitekeleza miradi mbalimbali.
“Fedha hizi sehemu kubwa ni za wakandarasi, huko waliko wanalalamika na kuipaka matope Serikali kwamba hailipi madeni wakati hii halmashauri imezitumia kwa matumizi mengine,” alisema Chikota.
Kutokana na hali hiyo, aliagiza fedha hizo zirejeshwe ili wakandarasi walipwe ili kupunguza manung’uniko huku akitaka malipo yanapofanyika vielelezo viwasilishwe ofisi ya CAG kwa ajili ya uhakiki.
Alieleza kuwa, kwa kuwa fedha hizo zimetumika kinyume na utaratibu, deni hilo lilipwe ndani ya mwaka huu wa fedha 2018/19 hususani ifikapo Juni, 2019.
Chikota alisema Kamati hiyo imebaini kuna ucheleweshaji wa utekelezaji miradi ya maji ikiwemo mradi wa masoko ambao kamati ilipotembelea iliona kuna kusuasua.
Alimwagiza Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) kuunda timu maalumu ya ufuatiliaji miradi ya maji katika halmashauri ya hiyo na kwamba baada ya kamati kufuatilia na kubaini kuna kulegalega itaandaa taarifa, itawasilishwa ofisi ya CAG kabla ya Desemba 30, mwaka huu.
“Halmashauri hii kwa miaka mitatu iliyopita ina deni kubwa la fedha za Mfuko wa Wanawake na Vijana, inadaiwa zaidi ya sh. milioni 576.9, pia inadaiwa sh. milioni 43 za fedha ambazo ni asilimia 20 ya mapato ya ndani yanayorejeshwa kwa vijiji,” alisema na kuongeza.
“Tunataka mtuandikie barua ambayo itaonesha mkakati wa kulipa deni hili hadi litakapoisha, akati wa kutoa mikopo hii ifuate muongozo uliowekwa kwa vikundi vya wanawake na vijana,” alisisitiza.
Akizungumzia kitengo cha ukaguzi, Chikota alisema kamati imeagiza kuwezeshwa kwa kitengo cha ukaguzi cha halmashauri hiyo ili kitimize majukumu yake ipasavyo.
Aliongeza kuna, changamoto ya uwepo wa uhakika wa vyanzo vya mapato vinatoa kiasi gani na mara nyingi Serikali imekuwa ikiagiza yafanyike makadirio kwa kila chanzo cha mapato.
“Kamati inaagiza Halmashauri ya Rungwe kwa kushirikiana na Ofisi ya RAS ifanye tathmini ya vyanzo vya mapato ili bajeti ijayo yawekwe makisio ambayo yanakaribiana na uhalisia,” alisema.
Awali akijibu hoja za wajumbe wa kamati hiyo, Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Loema Peter alikiri kuwa walikopa fedha hizo, kuzitumia kujengea maabara tatu kwa shule zote za sekondari wilayani humo.
Alisema wameanza kulipa fedha hizo ambapo mwaka uliopita walipeleka Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) sh. milioni 50 kwa ajili ya kulipa wakandarasi.
KYELA YARUDISHWA
Wakati huo huo, Kamati hiyo imeshindwa kufanya mahojiano na Halmashauri ya Wilaya ya Kyela kutokana na vitabu vyao kuwa na dosari mbalimbali ikiwemo katika fedha za elimu bure ambapo mchanganuo wa matumizi ya fedha hizo hazipo vizuri.
“Ukiangalia mchanganuo wa matumizi waliouleta kwa matumizi ya sekondari wanasema wametumia sh. milioni 792.4 kwa mwaka huo lakini ukiangalia kwenye kitabu chao wameonesha matumizi ya sh. milioni 163.4, sasa sh. milioni 510 hazijaoneshwa zimetumika kwa shughuli zipi,”alisema Chikota.

Comments