Featured Post

HILI NDILO SHIRIKA LA NDEGE ALILOLITAKA MWALIMU NYERERE



NA DANIEL MBEGA
SHIRIKA la Ndege Tanzania (ATCL) limerudi katika enzi zile za Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, ambaye ndoto zake zilikuwa kuona Tanzania inajiimarisha katika usafiri wa anga kwa ajili ya kukuza uchumi na kuimarisha usalama wake.

Tangu Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Magufuli iingie madarakani Novemba 5, 2015, jitihada kubwa zimeonekana katika kulifufua shirika hilo lililokuwa likikabiliwa na madeni mengi huku likiwa halina hata ndege moja.
Wapiga dili waliligeuza kitegauchumi chao, ambapo ilifikia mahali hata sare za wahudumu zilishoneshwa ng'ambo kwa mamilioni ya shilingi, fedha halali za walipa kodi na wavuja jasho wa Tanzania.
Tayari mpaka sasa ATCL inazo ndege nne - tatu ni Bombardier DHC-8-Q400 NG na moja ni Boeing 787-800 Dreamliner 5H-TCG - ambazo tayari zinafanya safari sehemu mbalimbali katika miji ya Bukoba, Dodoma, Kigoma, Kilimanjaro, Mbeya, Mwanza, Tabora, Zanzibar, Mtwara, Songea, Dar es Salaam na Moroni visiwani Comoro wakati ambapo safari za kwenda Mumbai, India na Guangzhou, China zinatarajiwa kuanza mwezi Septemba mwaka huu 2018.
Ndege hizi ni sehemu ya ndege sita ambazo Serikali imepanga kununua kwa fedha taslimu, ambapo ndege mbili zaidi zinatarajiwa kuwasili nchini Novemba 2018.
Ujio wa ndege hizi umerejesha heshima ya Tanzania katika usafiri wa anga tofauti na ilivyokuwa nyuma ambapo siyo tu serikali ilikuwa ikikosa mapato kwa kushindwa kusafirisha abiria, lakini hata kiusalama haikuwa vizuri kwa kuwa ndege zilizokuwa zikifanya safari ni za binafsi.
Leo hii Watanzania wanafurahia safari za ndani zenye uhakika, tena kwa gharama nafuu kulinganisha na mashirika ya binafsi, hatua ambayo imewafanya wawe na imani kubwa na serikali ya sasa.

Kelele za wapinzani
Licha ya jitihada hizo zinazofanywa na serikali, lakini wapinzani wanaendelea kubeza kila kinachofanyika, huku wakisahau kwamba ni ATCL hiyo hiyo ambayo ilikuwa ikiingizia Serikali hasara kubwa kwa kukodi ndege kuu kuu na Tanzania kushindwa kuwa na ndege zake yenyewe ambayo ni alama ya utaifa na uzalendo.
Wapinzani wanasema kwamba, ATCL inabebwa kwa nguvu kwa sababu ya mtazamo alionao Rais Magufuli, lakini halibebeki.
Wanakejeli kwamba, kuongezeka kwa ndege hizo maana yake ni kuwa gharama za kuendesha shirika nazo zinaendelea kuongezeka hata kama ni kwa kulibeba.
Wengine wanasema eti hizi ndege zilizopo zinaweza zisitosheleze iwapo kweli tunanuia kuruka kimataifa hivyo huenda huko baadae tukalazimika kuongeza ndege zingine na hii itakuwa ni gharama nyingine.
Kweli hali itakaporuhusu itabidi kuongeza ndege nyingine kwa sababu huo ndio uhakika wa kujiimarisha kimataifa na kuwa na uhakika wa kuingiza wageni wengi, wakiwemo watalii na wawekezaji.
Wapo wanaosema ni bora kuuza ndege zote na kujiimarisha kwenye usafiri wa reli, lakini unawashangaa watu kama hao vichwa vyao vikoje kwa sababu hatuna treni inayoweza kwenda nje ya nchi, ikiwemo Ulaya.
Binafsi ninawaunga mkono wanaosema suala siyo ndege, bali ni uendeshaji wa shirika, na hilo ndilo ambalo Serikali ya Magufuli inalifanyia kazi.
Tunapaswa kujiuliza pia kama kweli shirika letu halikuwa linahujumiwa, life ili watu wengine waingize midege yao na kuchukua ukanda katika usafiri wa anga.
Twende ndani tukachunguze na kuona ni akina nani wanamiliki mashirika yaliyofumuka tangu mwaka 1997, huku ATCL ikifilisika na kukodishwa kabla ya kuchungulia kaburi.
Haitashangaza hata mara moja kukuta kwamba wapo vigogo waliopata kuwa na nyadhifa za juu za maamuzi serikalini, ambapo hata mashirika hayo ya binafsi yalianzishwa wao wakiwa madarakani.
Kumiliki ndege ni gharama, hilo halina ubishi na hasa suala la matengenezo, lakini hatuwezi kukwepa kununua ndege eti kwa sababu ya gharama, vinginevyo hatuna haja hata ya kufanya kazi au kuweka akiba kwa sababu sote ipo siku tutakufa!
Tukitaka ATCL iimarike na itengeneze faida baadaye, lazima kuja na mkakati wa kupambana na ushindani katika bei badala ya kuweka nauli za juu, kwa sababu hiyo ndiyo itakuwa silaha kubwa ya kujiendesha, achilia mbali silaha ya msingi - Uzalendo!

Ndoto ya Mwalimu
Anachokifanya Rais Magufuli ni kufufua ndoto ya Mwalimu Nyerere aliyelianzisha shirika hilo miaka 41 iliyopita, na kamwe hakukosea.
Ilikuwa Ijumaa, Machi 11, 1977 wakati Shirika la Ndege Tanzania (ATC) linaanzishwa, Rais wa wakati huo, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, alikuwa na ndoto za kuona Tanzania inajiimarisha katika usafiri wa anga.
Usafiri wa anga wakati huo ulikuwa umesimama kwa muda baada ya kuvunjika kwa Shirika la Ndege la Afrika Mashariki (EAA) kufuatia kuvunjika kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki mwaka huo, kwani EAA ilimilikiwa kwa pamoja na Kenya, Tanzania ya Uganda.
Itakumbukwa kwamba, baada ya kuvunjika kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki, usafiri wa anga kwa kiasi kikubwa ulikuwa mikononi mwa Kenya, wakati Tanzania yenyewe ilibaki na usafiri wa reli.
Kwa maana nyingine, Kenya, ambayo ilikuwa imeanzisha Shirika lake la Ndege (Kenya Airways), ndiyo iliyokuwa ikitawala usafiri wa anga wakati huo.
Jambo hili lilimfanya Mwalimu Nyerere aone umuhimu wa kuanzisha haraka Shirika la Ndege Tanzania na mara tu ATC ilipoanzishwa, serikali ikakodi ndege yake ya kwanza aina ya Douglas DC-9-32, 5Y-ALR (ambayo ilikuwa miongoni mwa zilizokuwa ndege za EAA) kutoka Kenya Airways.
Mwaka huo huo zikapatikana ndege nyingine ndogo mbili, DC-9-32 5Y-ALR na Fokker F27-600, PH-EXC c/n 10566 iliyotoka Schiphol, Uholanzi.
Baadaye zikapatikana ndege nyingine aina ya DeHavilland Canada DHC6 Twinn Otter 300 5H-MRB c/n 579 mwaka 1978 na Boeing 720-022 N62215 ilikodishwa mwaka 1979 kutoka Caledonian Airlines INC, lakini ATC ililazimika kuvunja mkataba huo miezi mitatu baadaye kutokana na mkodishaji kupunguza idadi ya abiria waliopaswa kusafirisha, ni abiria 28 tu.
Katika miaka hiyo Enzi za Mwalimu hasa mwaka 1980-1981, ndege za ATC zilifanya safari nyingi za kitaifa na kimataifa kwa kutumia ndege zake za Boeing 707 na 737 na Fokker kutoka Dar es Salaam hadi Athens - Ugiriki (707), Antanarivo - Madagascar (737), Bombay - India (707) Bujumbura - Burundi (737), Cairo - Misri (707), Frankfurt - Ujerumani (707), Kigali - Rwanda (737), London Gatwick - Uingereza (707), Mahe - Shelisheli (737), Maputo - Msumbiji (737), Mauritius (737), Moroni - Comoro (FKF), Muscat - Oman (737) na Rome - Italia (707).
Kuanzia kiangazi cha mwaka 1981, safari zilifanywa kwa kutumia ndege ya Boeing 707-320 (N762TW c/n 17675 "Ngorongoro Crater") kwenda Misri-Ulaya, Dubai-Pakistan-India ingawa safari hizo zilivunjwa baada ya ndege hiyo kupata ajali kwenye uwanja wa ndege Dar es Salaam.
Kulikuwa na safari nyingi za ndani kutoka Dar es Salam hadi Bukoba (DHT), Dodoma (DHT/FKF), Iringa (DHT), Kigoma (737), Kilimanjaro (707/737/DHT/FKF), Kilwa (DHT/FKF), Lindi (FKF), Mafia (DHT), Masasi (DHT), Mbeya (DHT), Mtwara (737/DHT/FKF), Musoma FKF), Mwanza (737/FKF), Nachingwea (FKF),  Njombe (DHT), Pemba (DHT/FKF),Songea (FKF), Tabora (FKF), Zanzibar (DHT/FKF).
Safari nyingi za ndani ziliongezeka kwa kutumia ndege za Boeing 737-2R8C (Adv) 5H-ATC c/n 21710 "Kilimanjaro" na Fokker F27-600RF Friendship 5H-MPU c/n 10569 na Serikali ikaongeza ndege ya De-Havilland Canada DHC-6 Twin Otter 5H-MRC kwa ajili ya safari za ndani kutoka Kilimanjaro.
Na tunakumbuka jinsi ndege yetu ya 5H-ATC Boeing 737-2R8C ilivyotekwa mara mbili - mara ya kwanza Februari 26, 1982 kwenye Uwanja wa Ndege wa Mwanza wakati ikiruka kwenda Dar es Salaam ambapo akina Mussa Membar na wenzake waliiteka kwa kutumia bastola bandia na kuipeleka London, Uingereza.
Mara ya pili ilikuwa Februari 13, 1988 wakati watekaji wawili walipoiteka kwenye Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam ikijiandaa kwenda Nairobi wakitaka ndege hiyo iwapeleke Stanstead, Uingereza. Tukio hilo lilidumu kwa siku mbili na watekaji walikamatwa baada ya ndege kuzingirwa.

Baada ya Mwalimu
Tangu Mwalimu Nyerere alipoondoka madarakani na hasa baada ya ndege kadhaa za ATC kuharibika kutokana na ajali na uchakavu, shirika hilo likaanza kuyumba na kupoteza kabisa mwelekeo.
Kwanza, kati ya mwaka 1991 na 1992 Serikali ikakodisha ndege ya Boeing 767-200 ET-AIZ kutoka Shirika la Ndege la Ethiopia lakini ndege hiyo ilionekana kuwa kubwa zaidi na haikuwa na maslahi, hivyo ikabidi irudishwe kwa wenyewe.
Mnamo Desemba 12, 1993, ndege ya 5H-MPT Fokker F27 ilianguka wakati ikitua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam. Ndege hiyo ikaondolewa kwenye orodha na ikatumika kwa vipuri tu.
Mnamo mwezi Mei 1994, kampuni ya Shannon Aerospace ya Ireland ilikodishwa kuzitengeneza ndege mbili za Boeing 737-200C, ndege tatu za De Havilland DHC-6 Twin Otter 300 na ndege tatu za Fokker F27-600.
Lengo la ATC lilikuwa kufufua ndege hizo ili zichukue nafasi ya ndege kongwe ya Boeing 737 kwa kutumia model mpya ya Fokker F27 na mbili za Fokker 50.
Wakati huo safari za kimataifa zilikuwa Bujumbura, Djibouti, Entebbe, Gaborone, Harare, Johannesburg, Kigali, Lilongwe, London, Lusaka na Muscat. Safari za Johannesburg zilifanywa na Air Malawi kwa niaba ya ATC.
Ni katika kipindi hiki ambapo ATC iliingia katika mazungumzo ya kuwa na hisa asilimia 10 kwenye Ushirikiano wa Pamoja na Shirika la Alliance Air (baadaye ikajulikana kama SA Alliance), shirika la ndege ambalo lilikuwa na makao yake kwenye Uwanja wa Ndege wa Entebbe, Uganda.
Makubaliano hayo yakafikiwa mwaka 1994 kati ya ATC, Shirika la Ndege la Afrika Kusini (SAA) na Shirika la Ndege la Uganda kwa lengo la kushindana na mashirika ya ndege ya kimataifa. Ushirika huo ulikuwa na ndege moja aina ya Boeing 747SP-44, ZS-SPA cn 211321/280 iliyokodishwa kutoka Shirika la Ndege la Afrika Kusini ambapo ilifanya safari zake kati ya Afrika Mashariki na Ulaya.
Ubia huo ulikoma Oktoba 2000, baada ya kuingia hasara ya Dola za Marekani milioni 50.
ATC ilibinafsishwa mwishoni mwa mwaka 1998 na mipango ya kuiunganisha moja kwa moja na Alliance Air ilishindikana. Shughuli za Alliance Air zilikoma mwaka 1999 kutokana na mzigo mkubwa wa madeni. Wakati huo Alliance Air ilikuwa ikifanya safari zake kati ya Dar es Salaam, Kilimanjaro na London - Heathrow kutoka Uwanja wa Ndege wa Entebbe.
Kutokana na hilo, mipango ya kulibinafsisha shirika la ATC likabaki chini ya serikali kama ilivyokuwa awali.
Wakati huo huo, ndege ya Boeing 737-200, 5H-ATC ilitakiwa kufanyiwa uchunguzi (C-check), ATC ikakodisha ndege ya Boeing 737-300 XA-SWO c/n 27284 "Ngorongoro" kutoka Transportes AƩreos Ejecutivos (TAESA) ya Brazil kwa kipindi kifupi.

Ndoa ya ATC, SAA
Mnamo Februari 2002, serikali ikaanza mchakato wa kulibinafsisha shirika la ATC kwa kutangaza zabuni kwenye magazeti ya ndani na kimataifa. Mashirika manne kati ya manane yakaingia kwenye mchakato huo ambayo ni Shirika la Ndege la Afrika Kusini (SAA), Kenya Airways, Shirika la Ndege la Comair Afrika Kusini) na Nationwide Airlines pia la Afrika Kusini.
SAA ikashinda zabuni hiyo na mwezi Desemba 2002 wakasaini mkataba ambapo serikali ilikuwa na asilimia 51 ya hisa kwenye ATC.
Kwa bahati mbaya, ndege mbili za Boeing 737-2R8C(Adv) - 5H-ATC na 5H-MRK zikaondolewa kwenye huduma na kupelekwa Afrika Kusini. SAA ilikuwa na mpango wa kununua ndege za Boeing 737-800 lakini badala yake ikanunua ndege kuu kuu za Boeing 737-200, mbili za Fokker F-28 na mbili za De Haviland Dash 8-315.
Mnamo Januari 31, 2005, ATC ikafuta moja kati ya safari zake za kimataifa kutoka Dar es Salaam kwenda Nairobi, Kenya, kutokana na ushindani mkubwa kutoka Kenya Airways.
Mwaka huo huo ATC ikatangaza kupata hasara ya Dola milioni 7.3 katika mwaka wake wa kwanza wa ubia na SAA, hasara ambayo ilichangiwa na kushindwa kupanua safari zake kwani awali ilikuwa imepanga kupanua safari zake kwenda Dubai, India na Ulaya lakini ikashindikana kwa kuwa ndege pekee walizokuwa nazo ni Boeing 737-200 ambazo pia zilikuwa kuu kuu.
Septemba 7, 2006 Serikali ikanunua asilimia 49 kwenye ATC kwa gharama ya Dola milioni 1, hali iliyomaanisha kuvunja mkataba na SAA.
Mkataba huo ulivunjika kutokana na haja tofauti za wanahisa. Ndege mbili za Boeing 737-247 Adv, 5H-MVV na 5H-MVZ zilikuwa zimekodishwa kutoka Celtic Capital Air Corporation, Canada kwa miaka miwili kwa gharama ya Dola 50,000 kwa mwezi.
Mnamo Septemba 2007 kampuni ya Air Tanzania Company Limited (ATCL "Wings of Kilimanjaro") ilianzishwa baada ya kuvunjwa kwa mkataba na SAA na ilikuwa na safari za Dar es Salaam kwenda Mwanza kupitia Kilimanjaro.
Mnamo Oktoba 2007 ATCL ikakodisha ndege ya Airbus A320 kutoka kampuni ya Wallis Trading Company kwa muda wa miaka sita.
Ukodishaji huo ulikuwa sehemu ya mchakato wa ubia, ambapo ATCL ilikuwa iuzwe kwa hisa kwa kampuni ya Sonangol ya China, ambayo haikuwahi kusaini mkataba wowote rasmi wa makubaliano na serikali ingawa ilikuwa imeahidi kuinunulia ATCL ndege tano za Airbus hadi kufikia mwaka 2012 kama sehemu ya mpango wa ubinafsishaji.
Kwa kujua kwamba walikuwa wanaingia mkataba na Sonangol, menejimenti ya ATCL ikaharakisha kukodisha ndege ye A320-214 kutoka Wallis Trading, kampuni ambayo ilikuwa imedai kuwa na uhusiano na Sonangol ya China iliyoongozwa na mfanyabiashara wa Hong Kong, Sam Pa. Ndege hiyo ilikuwa imefanya huduma Liberia ambako ndiko ilikokodishwa, lakini kabla ilikuwa imekodishwa huko El Salvador.
Lakini wakati ATCL inaingia mkataba wa kuikodisha Oktoba 2007 ndege hiyo ilikuwa inatakiwa kufanyiwa ukaguzi (C-check) ndani ya miezi sita, hivyo kuingia katika hasara nyingine. Iliporejea kutoka kwenye matengenezo Mei 2008, ndege hiyo iliruka angani kwa miezi saba tu hadi Desemba 2008 wakati ilipoegeshwa ili ifanyiwe matengenezo mengine ya D-ckeck na haikuwahi kuruka tena angani, hadi ilipokodishwa na ATCL Oktoba 2011. Hiyo ilikuwa ni miaka miwili kabla ya mkataba wa ukodishaji kumalizika lakini gharama za ukodishaji zikabakia pale pale kana kwamba ndege ilikuwa ikifanya kazi katika muda wote wa mkataba.
Hali hii inadhihirisha namna ufisadi ulivyokuwa ikifanyika kiasi cha kulifilisi shirika hilo.
Mwaka 2008 ATCL ilikodisha ndege za 5H-MWH Airbus A320-214 c/n 363, 5H-MVV Boeing 737-247 Adv c/n 23520, 5H-MVZ Boeing 737-247 Adv c/n 23607, 5H-MWF De Havilland Canada DHC-8Q-311 DASH 8 c/n 475, na 5H-MWG De Havilland Canada DHC-8Q-311 DASH 8 c/n 462.
Tangu wakati huo hali ikawa mbaya zaidi kwa sababu Januari 2009 ndege mbili za Airbus A320 na Boeing 737 zikaondolewa katika utoaji huduma.
Kwahiyo, ujio wa Magufuli umelifufua shirika hili ambalo lilikwishakufa kwa sababu ya 'upigaji wa dili' na sasa heshima ya Tanzania imerejea kama Mwalimu Nyerere alivyokuwa akitamani kuliona.
0656-331974

Comments