- Get link
- X
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- X
- Other Apps
NA MWANDISHI
WETU
Miongoni
mwa Malengo Endelevu ya Maendeleo (SDGs) lengo namba nne ni kuhakikisha unakuwepo ujumuishi na uwiano wa elimu bora na kuboresha fursa za kujifunza maishani kwa
wote.
Hali
kadhalika zimekuwepo kauli mbiu zinazoweka wazi kuwa elimu ndio ufunguo wa
maisha, kuwekeza katika elimu ni kuwekeza katika ustawi wa jamii pamoja na nyingine zinazosisitiza umuhimu wa
elimu katika maendeleo.
Kwa
kuzingatia hilo ni dhahiri kuwa haki ya elimu kwa wote ni lazima ifikishwe kwa watoto, vijana na hata watu wazima walio na ulemavu.
Ndani
ya mtazamo huo ni kwamba walemavu
wanatakiwa wawe na fursa ya kusimamia maisha yao kuliko kuwa watu wa kuangaliwa
kimyakimya au kupewa uhisani.
Hili
linajiweka karibu na fikra za hivi sasa kuhusu haki kwa msingi wa mtazamo wa
maendeleo, ambako kunaongeza kuridhiwa na serikali na mashirika ya maendeleo ya
kimataifa duniani kote.
Hali
hiyo pia inamaanisha kuwa mizizi ya umasikini na kukosa nguvu, ni jambo ambalo haliko kwenye mkondo wa
biolojia bali ni katika jamii na linaweza kufanyiwa mageuzi.
Aidha,
mtazamo wa haki za binadamu kwa maendeleo unatoa fursa kwa mageuzi ya
kiutamaduni na kijamii. Hali kadhalika unatoa mwanya kwa watu walemavu kuwa na
dhana ya mtazamo wa namna wanavyojiona kutoka kwenye dhana ya kunyanyapaliwa na
kuingia kwenye mtazamo wa kuthaminiwa maisha yao.
Ufanisi
katika njia hiyo ni kupitia elimu na ndio maana
sera za taifa za maendeleo ya elimu
zinajumuisha mtazamo
jumuishi ambao umekuwa unajadiliwa na serikali pamoja na jumuia ya wahisani
kimataifa.
Mfano
hai ni Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Tanzania (Mkukuta) ambao
miongoni mwa malengo ya uendeshaji wake
katika nyanja ya elimu ni pamoja na kuongeza uandikishaji wa watoto
walio na ulemavu shuleni.
Kwa
mujibu wa Mkukuta 2005, inabainishwa kuwa uwiano wa watoto walio na ulemavu wanaoandikishwa na wale
wanaohudhuria na kumaliza
elimu unalenga kuongezeka kutoka asilimia 0.1 ya mwaka 2000 kufikia asilimia 20 mwaka 2010.
Hata
hivyo bila kuwajibika kisheria na kuwepo
kwa bajeti lengo hilo halitafikiwa hivyo kundi hili la jamii kuwa limesokomezwa
pembezoni na kutopea katika umaskini.
Shirika
la Elimu Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa (Unesco) linasema, “Ujumuishi
unaonekana kama hatua ya kuangalia na
kuwajibika kwa anuai ya mahitaji ya wote
wanaojifunza kwa kuongeza ushirikishwaji
wa kujifunza, utamaduni na jumuia na kupunguza kutengwa kwenye elimu.
“Unahusisha
mabadiliko na kuboreshwa kwenye yaliyomo, mtazamo, muundo na mikakati kukiw ana
dira ya pamoja ambayo inahusisha watoto
wote walio na miaka inayotakiwa na kuufanya kuwa ni jukumu lililo
kwenye mfumo wa kawaida wa elimu kwa watoto wote...ujumuishi unamaanisha
kutambua na kuondoa vikwazo...”
Kwa
upande wa Tanzania ni kwamba imeshajipambanua
kuhusu haki ya watoto walio na ulemavu kwamba lazima wapate elimu
kulingana na mahitaji yao kupitia Azimio la Haki ya Mtoto la mwaka 1990, na
Azimio la Afrika la Haki za Mtoto la mwaka 2003 na Sera ya Elimu ya mwaka 1996.
“...watoto
walio na ulemavu lazima wajumuishwe
kwenye shule za kawaida, karibu na nyumbani hivyo kwamba wanashirikiana
rasilimali ya shule na uzoefu wa pamoja na wenzao ambao sio walemavu.”
Pamoja
na hali hiyo Tanzania imelipokea azimio
jipya la Haki ya Watu walio na Ulemavu la
Machi 30, 2007. Kifungu namba 24 cha elimu kinasema, “Idara za serikali
zitambue hali ya walemavu kupata elimu.
Hili
linatakiwa kuwa kwenye mtazamo kuwa haki
hiyo inatolewa bila ubaguzi na katika misingi
ya fursa sawa, pia ni lazima kuhakikisha
mfumo jumuishi wa elimu unakuwepo katika ngazi zote na unakuwa ni wa
muda mrefu na endelevu.
Katika
kutambua haki hii inatakiwa kuhakikisha kuwa
watu walio na ulemavu hawatengwi
kutoka kwenye mfumo wa jumla wa
elimu na wanaweza kufikia elimu ya
msingi jumuishi,bila malipo na iliyo bora pamoja na elimu ya sekondari katika
misingi ya usawa na wengine ndani ya
jumuia ambamo wanaishi.
Hali
kadhalika malazi kwa kila anayehitaji
ni muhimu yakatolewa pamoja na
watu walio na ulemavu kupata msaada unaotakiwa kwenye mfumo wa elimu kwa
jumla ili uwepo ufanisi kwenye elimu
yao.
Aidha
hatua zenye ufanisi kutoka kwa watu
binafsi zinatolewa katika mazingira
ambayo yatawezesha kufikia
kiwango cha juu cha elimu na maendeleo ya jamii pamoja na lengo la kufanikisha ujumuishi.
Katika
mazingira ya aina hiyo vifaa vya kusomea
ni muhimu ikiwa ni pamoja na kufanikisha
kupatikana kwa maandishi ya wasioona
nukta nundu (Braille), vifaa vingine mbadala, miundo ya mawasiliano na mbinu za kuyafikia.
Pamoja
na hayo kwa walemavu wa kuzungumza na kusikia mkakati ni wa kuwawezesha kusoma lugha za alama na kuboresha
utambulisho wa lugha kwa jamii zilizo na ulemavu wa kusikia.
Hali
kadhalika kuhakikisha kwamba elimu kwa watu na hususani watoto ambao hawaoni, viziwi au wenye ulemavu wa
kutosikia na kuona inatolewa katika
lugha sahihi na njia za mawasiliano kwa
kila mmoja na kwenye mazingira ya kupata maendeleo ya kielimu na
kijamii.
Ili
kusaidia kuhakikisha unakuwepo utambuzi wa haki hii idara zinazohusika zitachukua hatua ya kuajiri
walimu, wakiwemo walimu walio na
ulemavu ambao wamefuzu kwenye lugha za alama na maandishi kwa wasioona na kutoa mafunzo kwa wataalamu na wafanyakazi katika ngazi zote za elimu.
Mafunzo
ya aina hiyo yatajumuisha uelewa kuhusu ulemavu na matumizi ya njia sahihi na
mbadala za mawasiliano, mbinu za kielimu na zana kwa ajili ya kusaidia watu
walio na ulemavu.
Hali
kadhalika idara husika kuhakikisha kuwa
watu walio na ulemavu wanaweza kuifikia
na kuipata elimu ya kawaida, mafunzo ya ufundi, elimu ya watu wazima na mafunzo endelevu yasiyo na ubaguzi katika misingi ya usawa na
wengine wasio na ulemavu.
Mnyambuliko
huo unajidhihirisha kuwa fursa ya kupata
elimu kwa watu walio na ulemavu ni muhimu
ili kuwaondoa kwenye dhana dhanifu kuwa hawawezi bali ijengeke dhana kuwa wakiwezeshwa kielimu
wanaweza kubadili maisha yao.

Comments
Post a Comment