Featured Post

KILELE CHA MWONGO WA USALAMA BARABARANI 2020, AJALI ZINAZIDI



NA ALOYCE NDELEIO
AJALI  za barabarani, zinatisha, zinahuzunisha na zinasikitisha na dhihirisho la hili katika kipindi cha hivi sasa kwa Tanzania, limo katika kauli hii ya kiongozi w anchi Rais Dkt. John Pombe Magufuli  Julai 2, mwaka huu.
Alisema, “Nimechoka kutuma rambirambi kila siku, inatoka ajali hii, inakuja hii,  na kwa bahati mbaya mimi ndiye pekee ninayetuma  rambirambi, Waziri wa Mambo ya Ndani hahangaiki kutuma rambirambi…wameshakufa 40, mnataka wafe wangapi…?”
Huzuni na masikitiko ya Rais hapo yalionesha wazi kukosekana kwa uwajibikaji katika kushughulikia na kudhibiti matukio ya ajali. Katika kuwajibisha wahusika yeyé akaanza na kumng’oa waziri mhusika na kutoa maagizo kwa mteule mpya  kushughulikia hilo.

Kupambana na suala la ajali barabarani ni suala lililoleta hisia katika jamii na hata kimataifa hali iliyosababisha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa  kuzindua mwongo wa usalama barabarani kwa kipindi cha miaka kumi ili kukazia hatua zinazochukuliwa dhidi ya ongezeko kubwa la ajali za barabarani.
Azimio hilo la Umoja wa Mataifa namba A/64/L.44/Rev.1 lilipitishwa kwa kauli moja na wajumbe wote 192 wa Baraza Kuu, likiwa linataja  hatua kadhaa zinazopaswa kuchukuliwa ili kupunguza ajali za barabarani ambazo licha ya kuwa chanzo vya vifo na ulemavu, pia zimekuwa na athari kubwa kwa uchumi na maendeleo kwa nchi zenye uchumi mdogo.
Alama mpya au nembo ya usalama barabarani ilizinduliwa pia katika kutilia mkazo umuhimu wa Muongo wa Umoja wa Mataifa wa kuchukua hatua dhidi ya ajali za barabarani. 
Hatua hiyo mpya ya kupambana na ajali za barabarani ilichukuliwa ili kuokoa maisha ya watu kutokana na kukithiri kwa ajali za barabarani ambazo zimekuwa zinasababisha vifo vya watu milioni 1.3 kwa mwaka.
Nembo hiyo inalenga kuwa ni njia ya kuijengea jamii  uelewa wa masuala ya usalama barabarani  ikiwa ni sawa na riboni za Ukimwi/ VVU au mshipi mweupe unaovaliwa mkononi  kwa ajili ya kupambana na umaskini.
Kila siku wastani wa watu 3500 duniani kote huuawa kwenye barabara, na asilimia 90 ya ajali zote hutokea  miongoni mwa nchi zinazoendelea. Kishikizo hicho kimetengenezwa na wakala wa WPP plc ambaye yuko kwenye ubia wa kuunga mkono Mwongo wa Hatua za Usalama Barabarani 2011 -2020.

Ajali za barabarani Tanzania 
Wakati hali ikiwa hivyo, Tanzania katika siku za karibuni imekuwa inakabiliwa na matukio mbalimbali ya  ajali za barabarani na rejea zipo nyingi ikiwemo  ajali ya basi jijini Arusha mwaka jana 2017, ambayo ilisababisha  vifo vya wanafunzi 33, mwalimu wao pamoja na dereva wa basi hilo.
Nyingine ni ajali zilizotisha zilitokea Julai 2011,  mkoani Morogoro ambapo watu 13, wanamuziki wa kikundi cha Five Star Modern Taarab na nyingine  ni iliyotokea Moshi,  Kilimanjaro na kusababisha vifo vya watu 11 na majeruhi 26.
Pamoja na hali hiyo kilichoonekana kimataifa ni kuwepo haja ya kuwa na Mwongo wa kuchukua hatua ili kupunguza ajali za barabarani.
Katika dhana hiyo njia ilionekana ni kuiunganisha dunia kuchukua hatua ambapo Mkurugenzi wa Kuzuia Madhara kwenye Shirika la Afya Duniani Etienne Krug alisema, “Hospitali na vyumba vya kuhifadhia  maiti  sehemu mbalimbali dunia  zimejaa wahanga wa  ajali za barabarani. Muongo wa Kuchukua  Hatua wa Umoja wa Mataifa  ni fursa ya kipekee.
“Ukiwa unatambulishwa kwa Kishikizo cha usalama barabarani, mwongo huu  utawezesha  wahusika wengi kuunganisha nguvu na kuiweka kwa vitendo programu ya kuzuia na huduma zinazohitajika katika kuepuka hasara isiyo ya lazima.”
Mwongo wa Kuchukua Hatua za Usalama Barabarani ulizinduliwa rasmi Mei 11, 2011 kwa matukio mablimbali  duniani. Lengo la Mwongo lililoridhiwa na  serikali 100  kwenye Baraza Kuu la Umoja wa mataifa  ni, “Kuimarisha na kupunguza” vifo vya barabarani  duniani ifikapo mwaka 2020.
Shirika la Afya Duniani na kamisheni za kikanda za Umoja wa Mataifa  zikiratibu mwongo huo kwa niaba ya Umoja wa Mataifa
Krug anasema, “Usafiri salama  ni lazima uonekane kuwa ni haki ya msingi ya binadamu  kama  inavyokuwa  kwenye mahitaji ya maji salama,  hivyo ni  hitaji la msingi kwa ajili ya kusaidia mamilioni ya watu kuboresha fursa za maisha yao na  kuondoka kwenye umaskini.”
Miongoni mwa nchi zinazoendelea watu wamekuwa wanakabiliana na mabadiliko ya kasi ya mifumo ya usafiri katika kipindi cha miaka 20 hadi 30 na bado imebakia kuwa ni hatua inayobadilika kwa kasi.
Idadi ya magari duniani  inakadiriwa kuongezeka kwa  mara tatu ifikapo mwaka 2050 na asilimia 80 ya ongezeko hilo linatarajiwa kuwa miongoni mwa nchi zinazoendelea.
Hali hiyo inamaanisha kuwa kuna haja ya kuwa na lengo la kuzuia  utoaji wa hewa ya Dayoksaidi ya  Kaboni  kwa kiwango cha nusu ya kinachotolewa  hivi sasa  na Umoja wa Ulaya.
Anafahamisha, “Wakati kuna mabadiliko ya hali ya hewa na suala muhimu kama hili  inaweza kuwa ni  muhimu kuwasaidia wapanga sera na sekta ya magari kupunguza athari zinazotokana na ongezeko kubwa la idadi ya magari kwa kuboresha uchumi wa mafuta na kupunguza utoaji wa gesi joto.
“Kila baada ya sekunde 30 mtoto mmoja hufariki au kujeruhiwa, zaidi ya watoto wanne  kati ya kila watoto watano wanaofariki kutokana na ajali za barabarani  wanaishi miongoni mwa  nchi  zenye kipato cha kati na cha chini  na inakadiriwa kuwa  vifo vinavyotokana na ajali za barabarani  miongoni mwa nchi hizo zitaongezeka hadi kiwango cha  zaidi ya asilimia 80 ifikapo mwaka 2020.”
Benki ya Dunia hivi karibuni ilikadiria kuwa nchi zinazoendelea hupoteza takribani dola bilioni 100 kila mwaka kutokana na ajali za barabarani  kiasi ambacho kinalingana na kiwango  kinachotolewa kama misaada ya maendeleo.
Jambo linalofanya hata kuiona hali hiyo kuwa ni mbaya, ni kwamba zipo nyenzo na  njia za  kusitisha hali hiyo, kuokoa maisha lakini hakuna jambo ambalo limeshafanyika. 
Jambo ambalo pia linaweza kujikita kwenye mawazo ya wanajamii ni kuona athari za kutisha  kwenye maisha ya watu  wakati wapanga sera  wanaichukulia hali hiyo kinyume au kudharau tatizo.  Janga la ajali za barabarani linaweza kudhibitiwa lakini linahitaji kuangaliwa na dunia  kuitupia macho.
Barabara zisizo salama pia ni barabara ambazo haziwavutii watumiaji wengine wa barabara  wasiotumia magari, waendesha baiskeli au waenda kwa miguu katika hali hiyo ipo haja ya kuhakikisha kuwa maskini na watu walio pembezoni ambao hawana uwezo wa kumiliki gari kwamba na wao wanakuwa na huru na salama kwenye mifumo ya usafirishaji.
Zipo sababu kumi zinazoweza kueleza ni kwa nini ni muhimu kuchukua hatua dhidi ya vifo vinavyosababishwa na  ajali za barabarani
Sababu ya kwanza ni kwamba  watu milioni 1.3 hufariki kila mwaka kutokana na ajali za barabarani. Pili ajali za barabarani  zinaua  watu wengi kuliko ugonjwa wa Malaria. Tatu watu milioni 50 hujeruhiwa na matokeo yake  wengi hupata ulemavu.
Nne asilimia 90 matukio ya ajali  hutokea miongoni mwa nchi zinazoendelea. Tano vifo vinavyotokana na ajali vinatarajiwa kuongezeka na kufikia  milioni 1.9 ifikapo mwaka 2020.
Sita ajali za barabarani  ni chanzo namba moja kinachosababisha vifo vya vijana duniani kote na Saba ajali za barabarani zitakuwa ni mzigo  unaoielemea  sekta  ya afya kwa watoto walio na umri  chini ya miaka mitano.
Hata hivyo sababu ya Nane hasara inayopatikana kiuchumi kwa nchi zinazoendelea hufikia takribani dola bilioni moja kwa mwaka. Tisa ni kwamba majeruhi  husababisha kuwepo kwa mzigo mkubwa katika mifumo ya hospitali na afya kwa ujumla na Kumi ni kwamba ajali za barabarani zinaepukika.

Comments