Featured Post

MIAMALA YA UONGO YADAIWA KUTUMIKA KUFICHA MALI ZA MHASIBU TAKUKURU



NA MWANDISHI WETU
KESI ya utakatishaji fedha na umiliki wa utajiri kuliko kipato chake inayomkabili aliyekuwa Mhasibu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Godfrey Gugai na wenzake imechukua sura mpya baada ya upande wa mashtaka kuieleza Mahakama jana kuwa mhasibu huyo alitumia miamala ya uongo kuficha umiliki wa mali zake.

Hayo yalielezwa jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam wakati watuhumiwa hao wakisomewa maelezo ya awali, ambapo licha ya kuyakubali maelezo yao binafsi, walikana mashtaka yote yanayowakabili.
Mbali na Gugai, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni George Makaranga, Leonard Aloys na Yasini Katera.
Wakili wa Serikali, Awamu Mbangwa, aliwasomea washtakiwa maelezo hayo ya awali (preliminary hearing - PH) mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi.
Wakili Mbangwa alidai kuwa, Gugai anakabiliwa na makosa mbalimbali ikiwemo kumiliki mali isiyoelezeka, kughushi na kutakatisha fedha ambayo anadaiwa kuyatenda kati ya mwaka 2005 na mwaka 2006.
Alidai kuwa, Gugai aliajiriwa na Takukuru kama mchunguzi daraja la tatu mwaka 2001 na baadaye 2009 aliteuliwa kuwa Mhasibu Mkuu wa Takukuru, kazi aliyoendelea nayo hadi Agosti 2016 alipofukuzwa kazi.
Alidai, washtakiwa wenzake wote ni marafiki zake wa karibu na kwamba katika kipindi chote cha ajira, Gugai hakuwa na chanzo cha mapato ambacho kingeweza kumpatia kipato zaidi ya ajira yake.
Alidai kwamba, kwenye mishahara ya mshtakiwa na marupurupu mengine, alijipatia kipato halali cha Shs. 852,183,160.46 kutoka kwa mwajiri wake.
Pia mikopo yote aliyoipata katika benki ya CRDB, NBC, Benki ya Posta na Saccos ya Takukuru ilikiwa ina thamani ya Shs. 137 milioni.
Alidai kwamba, mwaka 2009 alitakiwa kufanya matamko juu ya umiliki wa mali zake ambapo alitamka kuwa hakuwa na vyanzo vingine vya mapato zaidi ya ajira yake na kwamba hakutamka mali zote alizokuwa nazo.
Aidha, Mbangwa alidai kuwa, mwaka 2014/015, Gugai alisajiri kampuni mbili za familia zenye majina ya Guru Medical Investment Ltd na Agobest (T) Ltd, ambazo hazikuwahi kufanya kazi yoyote wala kupata leseni ya biashara tangu ziposajiliwa.
Aliendelea kudai kuwa, Januari 2016 baada ya kuanzishwa kwa uchunguzi mshtakiwa Gugai alisajili kampuni ya biashara kwa jina la Cheers Wine and Spirit ambayo hadi mwishoni mwa mwaka huo haikuwahi kuwaingizia kipato chochote.
Alisema, mwaka 2015/2016 katika uchunguzi ilionyesha kuwa, Gugai alijipatia utajiri wa juu zaidi ya kipato chake halali wa Shs. 3,634,961,105.02 ambapo alimiliki nyumba 19 na viwanja 37 vilivyopimwa.
Utajiri huo alishindwa kuutolea maelezo ya jinsi alivyoupata ambapo ilisomwa kuwa, Juni 2016, Gugai alifanya juhudi za makusudi kuficha mali hizo kwa kushirikiana na washtakiwa hao wenziwe kwa kutengeneza mikataba ya uongo wakionyesha kuwa ameuza au kuhamisha umiliki wa mali hizo kabla ya 2016 wakati wakijua si kweli.
Wakili Mbangwa alidai, uchunguzi ulibaini siyo kweli kuwa mshtakiwa Gugai aliuza ama kuhamisha umiliki wa mali hizo bali alifanya miamala ya uongo kwa lengo la kuficha umiliki halali wa mali hizo.
Kesi hiyo itaanza kusikilizwa Juni 28, 2018.
Katika kesi hiyo, washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka 43 yakiwemo 20 ya utakatishaji fedha haramu, kumiliki mali zisizoendana na kipato na kughushi mikataba ya mauziano ya viwanja katika maeneo mbalimbali.

Comments