Featured Post

MABARAZA YA ARDHI YAJENGEWA UWEZO KUMALIZA MIGOGORO



NA PETER KIMATH, MOROGORO
WIZARA ya Ardhi, Nyumba na Makazi kupitia Programu ya Kuwezesha Umilikishaji  Ardhi (LTSP) wametoa mafunzo kwa mabaraza ya ardhi ya vijiji ili kuweza kuwajengea uwezo na hatimaye kumaliza migogoro ya ardhi inayoanzia ngazi ya chini.

Akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo hayo yaliyofanyika katika Kata ya Kiberege na kuhusisha vijiji vinne vya kata hiyo, Ofisa Ardhi Mwandamizi kutoka Wizara ya Ardhi, Frank Mizikuntwe, alisema mafunzo hayo yatatolewa katika mabaraza ya ardhi ya vijiji vyote vya Wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi ambapo ndipo upo mradi wa LTSP kwa sasa.
Mizikuntwe alisema, mafunzo hayo ya uwezeshaji ni kutekeleza mfumo ambao upo katika mradi wa LTSP unaolenga kupima na kutoa hati lakini pia kuna kipengele cha utatuzi wa migogoro ya ardhi
Alisema walishaanza kutoa mafunzo katika mabaraza ya Ardhi ya kata na sasa zoezi hilo linaendelea katika Wilaya za Ulanga na Malinyi na baada ya kuona hivyo imebidi pia watoe mafunzo kwa mabaraza ya vijiji kutokana na huko kimsingi kuwa na migogoro mingi inayohitaji usuluhishi itakayopelekea migogoro kutokwenda ngazi ya juu.
Afisa huyo mwandamizi Wa Ardhi alisema mafunzo hayo yatakuwa na awamu Mbili ambapo awamu ya kwanza itaanza kwa vijiji 37 na baadae wataendelea katika vijiji kadri vingine na kubainisha kuwa hali ya migogoro ya Ardhi katika Wilaya hizo bado ni mbaya.
Kuhusu kuongeza baraza la Ardhi la wilaya tokana na hivi sasa baraza Mona kuelemewa na kesi nyingi toka Wilaya hizo tatu,Mizikuntiwe alisema awali baraza moja lilitosheleza tokana na muundo wa Wilaya Mbili ila tokana na migogoro kuwa mingi wameamua kutoa mafunzo kwa mabaraza na wakiona migogoro ibaendelea wataangalia utaratibu Wa kuanzisha baraza lingine ila wataangalia uwezo Wa kibajeti.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi na Nyumba katika Wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi, Roginus Rugarabamu, alisema mafunzo hayo ni muhimu kwani migogoro mingi ya chini inatakiwa itatuliwe na wananchi wenyewe na siyo kufika katika baraza lake.
Rugarabamu alisema, wajumbe wa mabaraza wakipatiwa mafunzo na kuelewa wajibu wao wa kusuluhisha migogoro itakuwa tiba kubwa kwa wananchi na kudai kuwa kwa sasa kuna kesi 1,400 zinazoendela katika baraza lake na katika kesi hizo asilimia 80 zimekatiwa rufaa toka mabaraza ya kata.
Awali akifungua mafunzo hayo, Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, James Ihunyo, alisema mafunzo hayo yamekuja wakati muafaka baada ya kukithiri migogoro mingi ya ardhi katika wilaya hizo na kusema kuwa migogoro mingi ni ya kutengenezwa.
Ihunyo alisema, mabaraza mengi yanatoa maamuzi kimaslahi na kuwataka wajumbe kutoa haki itakayosaidia kupunguza mrundikano wa kesi katika Baraza la Wilaya na kusisitiza kuwa kama mjumbe anaona hawezi kazi aache na serikali inafuatilia kwa karibu wale wanaofanya kazi kimaslahi zaidi.


Comments