Featured Post

LEO NI BAJETI KUU YA SERIKALI 2018/2019

NA MWANDISHI WETU, DODOMA

BAJETI Kuu ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019, ambayo ni ya tatu kwa Serikali ya Awamu ya Tano, inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli, itasomwa bungeni Mjini Dodoma leo na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango.

Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Zungu, aliyasema hayo bungeni Mjini Dodoma jana muda mfupi kabla ya kuhitimisha shughuli za Bunge kwa siku hiyo.
“Bajeti Kuu ya Serikali itasomwa kesho (leo), saa kumi jioni, asubuhi kutakuwa na mpango wa maendeleo,” alisema.
Aliongeza kuwa, viongozi mbalimbali mashuhuri wakiwemo Mabalozi ambao wanaziwakilishi nchi zao nchini, watakuwepo bungeni na kuwataka wabunge wa vyama vyote kuwepo bungeni bila kukosa.
Alisema baada ya hotuba hiyo, wabunge wanaweza kwenda kuungana na familia na ndugu zao ili kusherehekea sikukuu baada ya kumalizika kwa Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
Akiwasilisha mapendekezo ya Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2018/19 kwa wabunge Machi 13, mwaka huu, Dkt. Mpango alisema bajeti hiyo inatarajia kukusanya na kutumia sh. trilioni 32.476, ikiwa ni ongezeko la sh. bilioni 764 ukilinganisha na bajeti ya mwaka 2017/18.
Mpango alitaja vipaumbele vya bajeti hiyo kuwa ni Mradi wa Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Stiegler’s Gorge katika Mto Rufiji kitakachozalisha megawati 2,100, ujenzi wa reli ya kisasa (SGR), kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro, kilometa 300 na Morogoro hadi Makutupora kilometa 336 na uboreshaji wa Shirika na Ndege Tanzania (TTCL).
Pia kuna ujenzi wa bomba la kusafirisha mafuta kutoka Hoima nchini Uganda hadi Tanga, uzalishaji wa makaa ya mawe na umeme Mchuchuma na Liganga, uendeshaji wa shamba la miwa, ujenzi wa Kiwanda cha Sukari Mkulazi, mkoani Morogoro, uboreshaji bandari za Tanga, Dar es Salaam na Mtwara.
Pia bajeti hiyo inatarajiwa kupunguza bei ya vitu mbalimbali vikiwemo vinywaji baridi na vyakula ambapo ongezeko la kodi linategemewa kuwepo kwenye vinywaji vikali pamoja na sigara.
Bajeti hiyo Kuu ya Serikali ya Tanzania inatarajiwa kusomwa kwa wakati mmoja na bajeti za nchi zote wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Comments