- Get link
- X
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- X
- Other Apps
Msafiri Sambagi mlemavu wa macho, akifanya
mahojiano na mwandishi wa Makala haya, katika kijiji cha Mwanyengo.
Na Oliver Motto, Iringa
UKIMUONA,
ni kijana mjanja, mcheshi na mwenye kujua mambo sana, anazungumza
kwa kujiamini, licha ya kutoona kwake, anajituma katika shughuli za kiuchumi,
huwezi kudhani kuwa haoni.
Nikiwa
katika kitongoji cha Mwanyengo, katika kijiji cha Migoli ndani ya Halmashauri
ya Wilaya ya Iringa, mara nakutana na kijana, nasema kwangu hii ilikuwa bahati
ya kujifunza mengi kutoka kwake.
Msafiri ni
kijana mwenye uhakika na anachozungumza kwa kuwa anajiamini sana, awali
sikutambua kama ninayezungumza naye hanioni, nilifanya naye mazungumzo kadha wa
kadha, lakini baadaye niliona akihangaika kuitafuta njia.
Aaah,
nilishikwa na mshangao na kulazimika kuwauliza wenyeji wangu, juu ya tatizo la
Msafiri sambagi, nilisikitika kuambiwa kuwa haoni hata kidogo.
Kwa kweli
ya Mungu mengi, na kabla hujafa hujaumbika, niliingiwa na huzuni huku
nikimsindikiza kwa macho, yeye akiendelea na safari ya kurudi nyumbani kwake.
Nilianza
kumfuata kwa nyuma, nilipomshika bega alistuka, nikamuita “Msafiri” akaniitika,
nikamwambia ninaomba kufanya mazungumzo naye.
Hakunionyesha
ukaidi Msafiri, niliangalia eneo lenye kivuli na kumshika mkono kumuelekeza
nilipotaka tukae ili kuliepuka jua kali lililokuwa likipenya katikati ya utosi
hivyo kuona lingekuwa kikwazo cha mazungumzo yetu.
Mimi na
Msafiri tulikaa na akaanza kunieleza kilichomsibu hadi yeye kufikia hatua hiyo
ya kuwa mlemavu.
Msafiri
Sambagi ana umri wa miaka 33, anasema alizaliwa katika kitongoji cha Mwanyengo
mwaka 1977.
Amezaliwa
akiwa hana hitilafu ya aina yoyote, nikiwa nina hamu ya kujua nini kilimpata
hadi kuwa mlemavu wa macho, Msafiri anasema alipokuwa na umri wa miaka 7 alijiunga
na elimu ya msingi katika shule ya wasioona
ya Bugiri iliyopo mkoani Dodoma.
Anasema
elimu hiyo aliipata kutoka kwa wafadhili, kutokana na wazazi wake kutokuwa na
uwezo wa kumudu gharama za ada ya shule.
Anasema
hali mnamo mwaka 1994 alimaliza elimu ya msingi, na hivyo kulazimika kurejea
nyumbani kwao Mwanyengo.
Anaeleza
kuwa hakuweza kuendelea na masomo ya elimu ya sekondari, na hivyo kubaki
nyumbani licha ya kupata ujuzi mbalimbali kutoka katika shule aliyokuwa
akisoma, kufundisha masomo ya ufundi wa sanaa.
“Shule
niliyokuwa nikisoma tulikuwa tunajifunza namna ya kutengeneza mazulia, kupiga
kinanda, lakini tulikuwa tunacheza michezo mingi kama mpira wa miguu wenye kengere
ndani, mipira ile ilikuwa inatusaidia sisi tusieona kujua mpira unakwenda
uelekeo gani, na pia tulijifunza kilimo,” anasema Msafiri.
Anasema
mnamo mwaka 2000 alipatwa na majonzi makubwa, baada ya kuondokewa na baba yake
mzazi hatua iliyoyafanya maisha yake na familia kwa ujumla kuwa magumu zaidi.
Anasema
hapo alilazimika kujituma zaidi ili kuziba pengo aliloliacha mzazi wake huyo,
pasipo kujali hali aliyonayo ya kutokuona.
Maisha
ambayo aliona kwa wakati huo yanamfaa ni kilimo, kwani hakukuwa na mbadala
mwingine wa kufanya kutokana na kutoona.
Anasema
amekuwa akihangaika kufanya kazi ya kibarua cha kulima katika mashamba ya watu,
ili kupata fedha kidogo za kujikimu kimaisha yeye na mama yake mzazi ambaye
anamtegemea.
Msimu wa
kiangazi, wakati shughuli za kilimo zikikoma humlazimu kujihusisha na kazi ya
kuchoma mkaa, kwa kuwa kuna wakati hulazimika kushinda njaa kutokana na maisha
magumu yaliyopo kijijini hapo.
Anasema
licha ya kufanya shughuli za kilimo laini amekuwa akikwamishwa na mpango wa
serikali wa ugawaji wa pembejeo za ruzuku, kwakuwa mpango huo hauna lengo la
kuwakwamua wakulima wadogo kutokana na kutumia pembejeo duni za kilimo.
“Hapa mimi
ningeishauri serikali kuwa ituweeshe kutukopesha pembejeo za kisasa ili tuweze
kuepukana na kilimo hiki duni cha kutumia majembe ya mkono, sasa wanapotupa
mbolea na mbegu, ina maana tunaendelea kuwa na eneo lile lile dogo na hivyo
kujikwamua si kazi rahisi,” anasema.
Msafiri
anasema endapo serikali itamuwezesha kumpatia jembe la kukokotwa kwa na wanyama
kazi kama Ng’ombe na Punda anaweza kuondokana na hali ya umasikini alionao kwa
kuwa angekuwa na uwezo wa kulima eneo kubwa la shamba na hivyo kupata mavuno
mengi ambayo baadhi yatamsaidia kwa chakula huku mengine akiuza na kujikwamua
kiuchumi.
Anafafanua
kuwa licha ya kujihusisha na shughuli za kilimo lakini amekuwa akipoteza nguvu
na muda mwingi pasipo kuambulia chochote, kutokana na kutumia jembe la mkono.
Anasema na
shamba lenye ukubwa wa ekari moja na nusu lakini amekuwa akipata gunia mbili
pekee ambazo hazikidhi mahitaji yake kwa mwaka, na hivyo kujikuta akimaliza
chakula hicho kabla ya mwaka haujaisha na hivyo kupata taabu sana katika kubuni
mbinu za ukupata chakula.
Moja ya
changamoto inayomkabili mlemavu huyu ni pamoja na uwepo wa Ndege, wadudu na
wanyama waharibifu wa mazao, ambapo kuna
msimu wa kilimo huambulia patupu, na kujikuta mazao yake yakimalizwa na
wadudu aina ya Mbilanzi (Viwavijeshi),
Kwembelele, Mijusi ambayo hutafuna mizizi ya mazao, wanyama kama Nyani,
pamoja na ndege aina ya Hondohondo, Kangapori pamoja na Njiwa.
Anasema
wadudu na wanyama hao wamekuwa wakichangia kudumaza uchumi wa wananchi wa
kijiji hicho na hivyo kujikuta kila mwaka wakiwa ombaomba kwa serikali ili
kupatiwa msaada wa chakula.
Akizungumzia
sababu za yeye kutoona, Msafiri anasema wakati akiwa na umri wa miaka miwili,
aliugua ugonjwa wa Surua, ambao ulimshambulia zaidi maeneo ya kichwa na hivyo
kuingia katika mboni za macho.
Anasema
kutokana na kuchelewa kupata matibabu kwa wakati, ugonjwa huo uliiathiri gololi
za macho yake na hivyo kuishia kuwa mlemavu asiyeona maisha,anasema tatizo hilo
linamfanya ashindwe kupata mke, na sababu kubwa ikiwa ni kutokuwa na hali nzuri
ya kiuchumi, hivyo wanawake kutomkubali kwa kuhofia maisha magumu.
Alisema hali ya zamani ingekuwa ni sasa,hangekuwa
mlemavu kwa kiasi hicho, kwani sasa kuna wataalamu na mabingwa wa macho wenye
uwezo wa kulikabiri tatizo hilo.
Msafiri
anawashauri walemavu wengine kuacha kubweteka na kuwa omba omba.
Amewataka
walemavu kujituma kwa kufanya kazi kwa bidii ili kujipatia riziki.
Comments
Post a Comment