Featured Post

HUYU NDIYE DEKULA KAHANGA ‘ALIYEMTIMULIA VUMBI’ BABU SEYA NDANI YA MARQUIS DU ZAIRE



  Orchestra Maquis Original mwaka 1987 katika ukumbi wa Wapiwapi's Bar, Chang'ombe jijini Dar. Kutoka kulia ni: Mbuya Makonga "Adios", Dekula Kahanga "Vumbi", Mpoyo Kalenga na William Maselenge. Aliyechuchumaa ni Juma Choka. Picha kwa hisani ya wanamuzikiwatanzania.blogspot.com.

Na Daniel Mbega, MaendeleoVijijini Blog

Wasifu
Jina kamili: Dekula Aloyce Obeid Kahanga
Kuzaliwa:  Aprili 2, 1962
Mahali: Kivu, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
Mtaalamu: Gitaa la solo, mtunzi, mwimbaji,
Bendi alizopitia: Kyalalo Band, Gramick Jazz, Bavy National, Grand Mike Jazz, Chamwino Jazz, Marquis du Zaire, Makonde Group (Sweden).
Bendi ya sasa: Dekula Band (Sweden).


Dekula Aloyce Obeid KahangaVumbi’ (alizaliwa Aprili 2, 1962 katika Kijiji cha Lumera, Wilaya ya Kivu Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo). Ni mwanamuziki wa Congo mwenye uraia wa Sweden ambaye alijipatia umaarufu mkubwa akiwa nchini Tanzania wakati akipiga muziki na bendi ya Orchestra Marquis du Zaire. Dekula ni mtaalamu wa kupiga gitaa hasa la solo na umahiri wake unasikika katika nyimbo nyingi za Marquis kama Makumbele, Ngalula, Tipwatipwa na kadhalika.
Ni baba wa familia akiwa na mke na watoto watatu. Dekula ni mtoto wa kwanza kati ya watoto kadhaa wa Mzee Aloyce Obeid Dekula, aliyekuwa mfanyakazi katika serikali ya Zaire iliyokuwa ikiongozwa na rais Mobutu Seseseko.
Dekula ni kati ya wanamuziki wachakarikaji ambaye amepata mafanikio makubwa hivi sasa akiwa jijini Stockholm, Sweden pamoja na bendi yake anayoimiliki ya Dekula Band.

Maisha ya awali
Akiwa huko kwao wilaya ya Kivu, ‘Vumbi’ alikuwa msikilizaji mzuri wa Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) ambayo ilikuwa ikisikika wakati huo na alizitamani sana nyimbo zilizokuwa zikiporomoshwa na bendi za Morogoro Jazz, Jamhuri Jazz, Tabora Jazz, Nyanyembe Jazz,  NUTA Jazz,  Mlimani Park, Maquis du Zaire na Orchestra Safari Sound.
Awali baba yake hakupenda apige gitaa, lakini kwa bahati nzuri alikulia kwa bibi yake katika mji wa Uvira, Mkoa wa Kivu, ambako alipata wasaa mzuri wa kujifunza na kutumia ala hiyo.
Huko alikuwa na uhuru zaidi na akaanza kwa kutengeneza magitaa yake, ambapo yalikuwa yakivunja kila mara baba yake alipokuwa akienda kumtembelea bibi yake.
Jirani na alipokuwa akiishi kulikuwa na baa iliyoitwa Sikiya Sosi ambapo palikuwepo na bendi iliyoitwa Gramick Jazz iliyokuwa ikitumbuiza hapo. Bendi hiyo ilipitiwa na wanamuziki wengi ambao baadaye walikwenda Tanzania, akiwemo Ramazan Mtoro Ongalla ‘Dk. Remmy’.
Dekula alikuwa akisikiliza muziki uliokuwa ukipigwa katika baa hiyo na yeye akawa anafuatisha kwenye gitaa la kutengeza mwenyewe la nyuzi tatu.
Bibi yake akamnunulia gitaa dogo la nyuzi nne ambalo alikuwa anaenda nalo hadi shuleni, ambako mwalimu wake siku nyingine alikuwa akimwita awatumbuize wanafunzi wenziwe.
Baadaye akakutana na jamaa aliyekuwa akipiga katika bendi iliyokuwa ikimilikiwa na mapadri, Dekula akawa anamnunulia sigara huyu jamaa, naye akaanza kumfundisha chords mbalimbali za kupiga gitaa.
Aliendelea vizuri hatimaye akajiunga na bendi hiyo ya mapadri iliyoitwa Kyalalo Band akiwa mpiga rhythm.
Wanamuziki wa Kyalalo hawakuruhusiwa kujiunga na bendi zilizokuwa zinapiga muziki kwenye baa wala bendi yenyewe kwenda kupiga kwenye baa. Kulikuwa na ukumbi mkubwa wa kanisa na hapo ndipo walipofanya mazoezi na maonyesho.
Alipata elimu ya sekondari katika shule mbili tofauti za Bukavu na Uvira huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Alihitimu kidato cha nne mwaka 1979.

Aanza rasmi muziki
Mwaka 1980, safari yake katika muziki ilianza kwa kujiunga na bendi ya Grand Mike Jazz. Kama ni kuanza rasmi muziki wa ushindani, basi ilikuwa mwaka 1983 wakati Dekula alipojiunga na bendi Orchestre Bavy National kama mpiga rhythm. Bendi hiyo ilikuwa ikipiga muziki pale pale Sikia Sosi Bar mjini Uvira, mkoani Kivu. Bendi hiyo iliongozwa na Packot ambaye pia alikuwa mpiga solo, Maboko alikuwa akipiga gitaa la bass, Merry-Djo alikuwa akipiga drums na waimbaji walikuwa Djo Mali na Simplice Mofeza.
Akiwa hapo akakutana na mwimbaji Issa Nundu ambaye alikuwa anafanya kazi hospitali na jioni kujiunga na bendi. Baadaye Kyanga Songa ambaye kazi yake ilikuwa Bwana Shamba naye akajiunga nao.
Katika kipindi hicho wakazi wa Kongo ya Mashariki, ambako kunazungumzwa Kiswahili, walikuwa wakisikiliza na kuzijua bendi nyingi kutoka Afrika Mashariki. Bendi kama Tabora Jazz, Mangelepa, Simba wa Nyika, Mlimani Park zilisikilizwa sana, na wimbo kama Kassim ulikuwa maarufu wakati huo na hivyo ikawa ndoto ya Vumbi kuwa lazima siku moja aende huko unakotoka muziki mtamu ili naye aweze kushiriki. 
Kutoka kulia mstari wa nyuma ni Dekula (Rythm), Packot (Solo na Kiongozi), Maboko (Besi), Merry-Djo (Drums). Kutoka kulia mstari wa mbele, waimbaji ni Djo-Mali,Issa Nundu na Simplice Mofeza. Hii ilikuwa mwaka 1983 katika ukumbi wa "Sikia Sosi Bar" mjini Uvira, Kivu katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

Katika kipindi hicho Kyanga Songa na Issa Nundu waliondoka kwenye bendi ya Bavy National na kwenda nchini Tanzania. Bendi ikatetereka sana, lakini Vumbi naye wakati huo akawa na hamu ya kwenda Afrika Mashariki.
Bahati nzuri mtu mmoja Alida Shanga akamfuata akiwa ametumwa na Mzee John Luanda aliyekuwa anamiliki Chamwino Jazz kwenda Zaire kutafuta wanamuziki. Akawachukua yeye Dekula, waimbaji akina Sisko Lunanga, Fanfan Bwami, Baposta na mwenzao mmoja Baposta Kilosho ambaye hatimaye alirudi Congo.
Wakatua Tandale jijini Dar es Salaam, na siku hiyo waliyofika tu wakaanza mazoezi. Wakiwa vijana bado yeye na wenzie watatu walikuja wakiwa na staili ya kuimba na steji show ambayo wakati huo iliitwa sarakasi, na pia wao ndio walioanzisha mtindo wa kurap katikati ya nyimbo.
Katika bendi ya Chamwino wakati huo wapiga magitaa walikuwa Vumbi Dekula, Kazembe wa Kazembe (huyu alikuwa Msukuma ambaye aliishi kwa muda Congo na alikuwa mpiga gitaa hodari sana), na Mzee Albert, na baadaye wakamchukua Muhidin Kisukari ambaye alikuwa mpiga bass wa Dk. Remmy.
Rekodi yao ya kwanza ilimuacha aliyekuwa mtangazaji maarufu nchini, ‘Uncle J’ Julius Nyaisanga akishangaa vituko vya vijana hao.
Mwaka 1983 alikutana na mwanamuziki Tshimbwiza Tchinsensi Nguza Mbangu ‘Viking’, maarufu Babu Seya, katika ofisi za Ubalozi wa Congo nchini Tanzania. Nguza wakati huo alikuwa mpiga gita la solo pia alikuwa mmoja kati ya wanahisa wa Orchestra Marquis Company (OMACO) na mmoja kati ya viongozi wa bendi ya Orchestra Marquis du Zaire. Katika maongezi yao, Nguza alimpa mwaliko yeye na wenzake kwenda kuburudisha kwenye ukumbi wa White House, uliokuwa maeneo ya Ubungo jijini Dar es Salaam.
Dekula alikubali mwaliko huo na Weekend moja walifika na kupewa nafasi ya kuburudisha kwa muda mfupi.
Walipopanda jukwaani waliweza kuzikonga nyoyo za wapenzi wa muziki waliokuwa wamefurika ukumbini humo pamoja na wanamuziki wa bendi hiyo ya Marquis du Zaire. Wakati huo walikuwa wakipiga nyimbo za kukopi, kama Mario, Maze na kadhalika. Walipopanda jukwaani wakazipiga hizo na watu wakafurahi sana na kuwatuza fedha nyingi, wakachanganyikiwa maana bendi yao ya Chamwino ilikuwa haina mshahara na si mara moja walitembea kwa miguu kutoka Buguruni hadi Tandale kwa kukosa mapato.
Japo wakati huo walikuwa wadogo kwa umri na hata umbo (walifika mahala marehemu Ndala Kasheba alikuwa anawaita ‘Vimario’) upigaji wao ulikuwa mzuri sana. Nguza Vicking aliwashauri wawe wanakwenda kupiga kabla Marquis hawajaanza maonyesho. Hivyo wakaamua kuacha Chamwino na wakawa wanasindikizana na Marquis. Jambo hilo lilimuudhi aliyewaleta na siku moja wakiwa kwenye ukumbi wa Silent Inn, maofisa wa Uhamiaji walikwenda kuwachukua wakalazwa Kituo Kikuu cha Polisi kabla ya kupelekwa mahabusu katika Gereza la Keko.
Wakiwa huko mahabusu wakamwandikia Mzee Luanda kuwa wanarudi Chamwino, basi wakaachiwa na kurudi kusuka upya Chamwino Jazz. Hata hivyo, hawakukaa muda mrefu Mzee Makassy akaja kuwaomba waingie katika bendi yake. Wenzake Sisco Lunanga na Bwami Fanfan wakaenda kuimarisha safu ya uimbaji ya Orchestra Makkasy, yeye akabaki Chamwino.
Baadaye viongozi wa Marquis du Zaire akina Chibangu Katayi ‘Mzee Paul’, Mutombo Lufungula ‘Audax’ na Mbuya Makonga ‘Adios’ walimtaka aandike barua ya kuomba kujiunga na bendi yao kwa mkataba usio na mshahara. Alitakiwa na bendi hiyo ili kuziba nafasi ya Nguza ambaye alikuwa tayari ameanza mgomo baridi. Vumbi alikubali na ndio ukawa mwanzo wa kujiunga rasmi na Marquis kama mpiga gitaa la solo nambari mbili (second solo). Aliwakuta wanamuziki kama Maneno Uvuruge, Omari Makuka, Keppy Kiombile, Ilunga Lubaba, William Maselenge, Mbuya Makonga ‘Adios’, Mpoyo Kalenga, Juma Choka na wakongwe wengine.
Siku moja bendi ilikuwa inapiga maeneo ya Ukonga. Kwa kawaida Mzee Lubaba alikuwa anapiga kuanzia saa tatu mpaka saa sita usiku, kisha Nguza Viking akiingia na kuendelea. Siku moja Nguza hakuonekana ukumbini na ndipo Vumbi akaweza kupiga nyimbo zote za Nguza, kesho yake akaambiwa afike ofisini akasainishwa rasmi mkataba wa kuwa mwanamuziki kamili wa Marquis.
Vumbi anaikumbuka siku mmoja wakipiga muziki katika ukumbi wa Temeke Stereo, alimuona Nguza akiwa amejibanza pembeni mwa ukuta ukumbini humo huku akisikiliza midundo inavyounguruma.
“Nilipomuona, nikaingiwa na hofu kubwa nikijihisi kama ninamvunjia heshima Nguza. Nikaomba nimpishe ili ashike nafasi yake.” Dekula anakumbuka.
Lakini viongozi wake akiwemo Chibangu Katayi ‘Mzee Paul’ na Ilunga Lubaba walimwamuru aendelee kushika ‘mpini’. Amri hiyo, ilikuwa kama fisi aliyeachiwa bucha kuilinda. Alizicharaza kwa umahiri mkubwa nyimbo zote zilizokuwa zikipigwa na Field Marshal Nguza zikiwemo za Makumbele, Ngalula, Seya, Malokelee, Karubandika, Mage, Dora Mtoto wa Dodoma, Clara, Mwana Yoka ya Bato te, Nimepigwa Ngwala na nyingine nyingi pasipo kutofautisha kati yake na Nguza.
Aliachiwa kulivurumisha gita hadi mwisho wa onyesho hata mpiga solo Ilunga Lubaba hakutaka kuligusa siku hiyo. Baada ya hapo kwa adabu zote alikwenda kumsalimia Nguza pale alipo naye hakusita kumpa hongera kwa kazi nzuri.
Mgogoro kati ya uongozi wa Marquis du Zaire na Nguza ‘Vicking’ ziliendelea hatimaye aliondoka rasmi na kwenda kuanzisha bendi yake ya Orchestra Sambulumaa akiwa na wanamuziki wengine akiwemo mwanaye Nguza Mbangu lakini bendi hiyo ikafa na ndipo alipoanzisha bendi yake ya Achigo Band iliyokuwa ikipiga kwenye ukumbi wa Motel Tiger, Mbezi Beach, ambayo ilikuwa na wanawe akina Papii Kocha lakini ikasambaratika tangu mwaka 2004 wakati yeye na wanawe walipohukumiwa kifungo cha maisha jela kwa makosa ya ubakaji.
Baada ya kuondoka kwa Nguza walirekodi ule wimbo maarufu wa Makumbele. Solo ya wimbo huo ilikuwa awali ikipigwa na Mzee Lubaba, lakini afya ya mzee Lubaba ilianza kuzorota naye akawa anawafundisha nyimbo zake wanamuziki wengine. Wimbo wa Makumbele alifundishwa Makuka na akawa anaupiga katika maonyesho mbalimbali, lakini wakati wa kutaka kurekodi kamati ya uongozi ya Marquis iliamua Vumbi aufanyie mazoezi na aurekodi.
Kurekodi kwa album ya Makumbele ilitokana na safari ndefu ya bendi ambayo ilichukua miezi mitatu katika mikoa ya Kanda ya Ziwa, hivyo waliporejea Dar wakakuta sifa ya bendi imepungua.
Kwa hiyo basi, walirekodi album ya Makumbele iliyokuwa na nyimbo kama Tipwatipwa, Ngalula na Makumbele, sifa ya bendi ikarudi juu tena kwa mara nyingine.
Ni wakati huo ambapo bendi ilihamia katika ukumbi wa Lang’ata, Kinondoni jijini Dar es Salaam ikitokea ukumbi wa White House.

Aenda Ulaya
 Dekula Kahanga akionyesha umahiri wa kucharaza gitaa la solo huko Ughaibuni.
Dekula Kahanga akiwa na farasi.

Miaka ya 1989 na 1990 Dekula alikuwa kivutio kikubwa kwa wapenzi wa Marquis Original, jina lililozaliwa kutoka Marquis du Zaire baada ya kuhamia katika ukumbi wa Lang’ata Kinondoni. Mtunzi na mwimbaji Marquis Original Tshimanga Kalala Assosa, alikuwa akipaza sauti ya kumpandisha mori kwa kumuita mara kwa mara “Vumbiii! Vumbiii! Vumbiii!” kama kibwagizo wakati wa chorus kwenye wimbo wa Ngalula.
Vumbi wakati huo alikuwa na umri ambao unamruhusu kuhangaika kutafuta maisha yenye maslahi mazuri. Hivyo uamuzi mgumu ukaanzia hapo Lang’ata baada ya kuamua kuiacha Marquis Original, iliyompa jina na akaondoka na kutua katika jiji la Stockholm nchini Sweden ambako hakujua atakuwa mgeni wa nani huko ughaibuni.
Akiwa Stockholm, Vumbi alianza kuchacharika mitaani akitafuta bendi ya kupiga, hatimaye akakutana na mwanamuzi kutoka Uganda, aitwaye Sammy Kasule. Mwaka 1993 wakaamua kuanzisha bendi yao ikiitwa Makonde Group.
Baada ya mihangaiko mingi, hatimaye alifanikiwa kuanzisha bendi yake ya Dekula Band, ambayo kwa sasa ina mkataba wa kupiga mara mbili kwa mwezi katika ukumbi wa Lala Vin, jijini Stockholm.
Mwaka 1999, Dekula alifyatua album iitwayo Bolingo Ekeseni iliyosheheni nyimbo za ‘Dunia kuna mambo’ na ‘Mpenzi Asha’.
Dekula Band ina wanamuziki mahiri kutoka nchi mbalimbali duniani, wakiwemo akina Luhembwe Mwanahita ‘Bobo Sukari’ ambaye ni mwimbaji na mcheza show kutoka Congo ambaye alipigia bendi kadhaa nchini Tanzania, Sammy  Kasule, huyo ni injinia pia huimba, kupiga gita la besi, drums na kinanda. Wengine ni Joe Gerald Nadibanga, ambaye huimba, kupiga konga na kucheza show, Christina Frank na Marceline Kouakoua. Mwenyewe Dekula hulicharaza gila la solo na rhythm pamoja na Arne Winald ambaye ni mbonyezaji wa kinanda.
Safu hiyo kwa pamoja huufanya muziki wao kukubalika kimataifa hadi kupata mialiko lukuki ndani na nje ya Sweden zikiwemo nchi za Ulaya, Asia, Marekani, Japan, Falme za Kiarabu na Afrika.
“Hakuna kitu muhimu kama kuwa na uhusiano mwema na watu kutoka nchi mbalimbali ninazotembelea. Nimefikia kuweza kuongea kwa ufasaha lugha tano tofauti za Kiswahili, Kiingereza, Kifaransa, Lingala na Kiswidi,” alisema Dekula.
Dekula Kahanga anajivunia kwamba yeye ni mwanamuziki wa kwanza kutoka Afrika aishiye Sweden kufyatua album. Alitoa album iitwayo ‘Dekula Sultan Qaboos’ yenye nyimbo za Sultan Qaboos, Mon Amour, Babylon, Mayanga (aliutunga akiwa na Marquis), Rozina, Mambo leo na Nostalgie nyimbo ambazo zinapigwa katika vituo vingi vya redio duniani.
Ili kupata unafuu wa maisha nchini Sweden, Dekula alilazimika kuomba uraia wa nchi hiyo baada ya kufuata taratibu zote. Alichukua uamuzi mgumu mwingine wa kuukana uraia wa nchi yake ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ili kupata uraia wa nchi hiyo. Hivi sasa yeye na wanamuziki wenzake wa bendi hiyo ni raia halali wa Sweden.


Comments