Featured Post

MIRUNGI NI JANGA, HUSAKWAMISHA UYEYUSHAJI WA CHAKULA MWILINI



NA MWANDISHI WETU
Iliporipotiwa katika vyombo vya habari kuwa gari la wagonjwa la Halmashauri ya Wilaya ya Tarime lililotakiwa kusafirisha mgonjwa kutoka Hospitali ya Wilaya ya Tarime kwenda Bugando jijini Mwanza, kukamatwa likiwa na kilo 800 za mirungi ilionesha kuwepo vyombo vya umma vinavyotumika katika uhalifu.
Gari hilo, lenye namba DFPA 2955, inadaiwa kuwa lilikuwa  likipiga ving’ora kama limebeba mgonjwa. Hali hiyo inamaanisha kuwa bado baadhi ya wanajamii ni viziwi kwa madhara ya dawa za kulevya na vikwazo kwa umma katika mapambano ya kuzitokomeza.

Kwa ambao hawazifahamu wanaweza kuchukualia taswira hii kwamba  unapita mjini au uko kwenye basi  unaona  mtu anachambua  aina fulani ya majani kama vile  mtu anayechambua  majani ya matembele lakini  baadhi ya sehemu anazitupa na nyingine anaweka mdomoni anatafuna.
Hali hiyo alikutana nayo mwandishi mmoja Abdullah bin Abdul Kadir kutoka Malaysia mwaka 1854 alipotembelea Yemen na kuona utamaduni huo wa ajabu wa kutafuna majani akasema, “Niliangalia tabia hii ya ajabu katikati ya mji na kushangaa  kila mtu anatafuna majani kama  mbuzi.” 
Iwapo utaona tukio la aina  hiyo basi ufahamu kinachotafunwa ni aina fulani ya majani  ambayo ni dawa za kulevya, ambayo ni mirungi.
Mirungi ina majina mengi  ambayo ni pamoja na Jaad (Somalia), Miraa (Tanzania na Kenya); majina mengine ni pamoja na mbaga, magoka, veve, gomba, na kashamba.
Inaaminika kuwa chimbuko la  mirungi ni Ethiopia na inaaminika  ilisambaa na kuenea maeneo mengine ya milimani Afrika Mashariki na Yemen. Wengine wanaamini kuwa ni Yemen  na baadaye ulisambaa na kuingia  kwenye maeneo ya Ethiopia.
Kwa mujibu wa tathmini za kibotania inaelezwa kuwa  chimbuko ni Yemen na kutoka maeneo hayo ukasambaa hadi nchi za Kenya, Somalia, Malawi, Uganda, Tanzania, Arabia, Congo, Zimbabwe, Zambia na Afrika Kusini.
Abdullah bin Abdul Kadir alibainisha kuwa watu waliokuwa wanatafuna  mirungi hiyo  baadhi walipokuwa wanatema mate yalikuwa ni kijani akalazimika kuuliza, “Ni  faida gani anayoipata mtu anapotafuna majani hayo?”
Alijibiwa, “Hakuna  anayejua…hiyo ni  hali tuliyoizoea Lakini ni jambo  linalotugharimu, tumekua na kujikuta tukiingia kwenye hali hiyo… lakini wale wanaotumia  majani haya  wanalazimika kutumia siagi na asali vinginevyo wataugua.”

Kilimo  cha mirungi
Tabia ya kutafuna mirungi inaelezwa kuwa ni kama kutumia kitu cha kuchangamsha mwili kama ilivyo kwa wanywaji wa kahawa na mara nyingine majani yake hukaushwa na kutumiwa kwa kuchanganya kwenye chai.
Matumizi ya mirungi  yamejikita maeneo ambayo inalimwa kwa sababu ni majani mabichi tu  ndiyo hutoa  aina  hiyo inayodaiwa ‘kuchangamsha mwili’ kuliko majani  makavu.
Kusambaa kwa mirungi Afrika Mashariki kunatokana na  kutengenezwa kwa miundombinu  ambayo  imewezesha na kurahisiha usafirishaji wake kutoka  nchi moja hadi nyingine.
Mirungi ni aina ya inayostawi kwenye hali ya unyevu nyevu na milima yenye  urefu  kati ya mita 4000 hadi 9000 na  kwa upande wa Tanzania  imekuwa inapatikana kwenye  maeneo yenye uoto wa asili katika mikoa ya  Arusha, Kilimanjaro, Manyara na Tanga. Lakini kiasi kikubwa cha mirungi inayotumika nchini inatoka nchi jirani ya Kenya.
Kilimo  cha Mirungi ni maarufu nchini Yemen  na  kimekuwa  kinatumia  sehemu kubwa  ya ardhi  inayofasa kwa kilimo na inakadiriwa kuwa  asilimia 40 ya maji ya nchi hiyo  yanatumika kwa ajili ya kumwagilia mashamba yake na mazao  yamekuwa  yanaongezeka  kutoka asilimia kumi hadi 15 kila mwaka.
Matumizi ya maji ni makubwa hivyo kwamba maji ya ardhini ambayo  yanapatikana  kwenye Bonde la Sanaa yanaelekea kukauka, na kuwafanya  maofisa wa serikali kufikia hatua ya kuwahamishia wakulima wa eneo hilo ukanda wa pwani ya Bahari ya Sham.
Moja ya sababu za  kuendesha kilimo  cha mirungi  nchini Yemen ni mapato makubwa yanayopatikana  kutokana na kilimo  chenyewe.
Baadhi ya  tafiti  zilizofanywa mwaka 2001 zinakadiria kuwa  mapato yanayopatikana kwa  kulima mirungi ni takribani riale  milioni 2.5 kwa hekta moja  na kama matunda yake  yaklikusanywa  huingiza  kipato cha  riale  takribani 570,000 kwa  hekta.
Hilo limesababisha wakulima kuendeleza kilimo  hicho badala ya   kilimo  cha mazao mengine kama kahawa na matunda.
Kati ya mwaka 1970 na 2000 eneo  lililokuwa linalimwa mirungi liliongezeka kutoka  hekta 8000 hadi hekta 103,000 na  hayo ni  makadirio tu  kwani idadi halisi inaweza kuwa kubwa zaidi.

Idadi ya Watumiaji
Inakadiriwa kuwa  mamilioni ya watu ni watumiaji wa mara kwa mara wa mirungi. Watumiaji  wakubwa wanatoka  nchi za Sudan na Madagascar na katika  eneo la kusini magharibi mwa Ghuba ya Arabia hususani Yemen.
Nchini Yemen asilimia 60 ya wanaume na asilimia 35 ya wanawake wanatumia mirungi  na wamekuwa wanaitafuna kwa muda mrefu wa maisha yao.
Kupigwa marufuku  kilimo cha mirungi mara nyingi limekuwa ni jambo linalopigwa vita  na viongozi wa dini kwa kutumia  vigezo  vya maandiko  ya  Koran  kwamba  ni marufuku  kitu chochote kinachodhuru mwili kutumiwa. Nchini Somalia  asilimia 61 ya watu wake  wanatumia mirungi.
Watafiti wanakadiria kuwa  takribani  asilimia 70 hadi 80 ya raia wa Yemen wenye umri kati miaka 16 na 50 wanatumia  mirungi.
Miongoni mwa watafiti Dk. Ali Al-Zubaidi anakadiria kuwa  kiasi cha fedha  zinazotumika ambazo zinatumiwa na  familia  zimeongezeka kutoka  reale bilioni  14.6 mwaka 1990 hadi kufikia reale  bilioni 41.2 mwaka 1995.
Watafiti pia  wanakadiria  kuwa familia zinatumia takribani  asilimia 17 ya mapato yake  kwa ajili ya mirungi (lakini idadi kamili  inaweza kuwa zaidi). 
Moja ya athari kubwa za kiuchumi ni kwa  tabaka la chini ambalo hujikuta  likitumia fedha nyingi inazozipata  kununulia  mirungi badala ya  chakula.

Mapambano dhidi ya mirungi
Marufukudhidi ya matumizi  ya  mirungi  hukumbana na vikwazo  kwa mfano Somalia Baraza la Mahakama ya Kiislamu  ambalo lilikuwa  linashikilia sehemu kubwa ya nchi hiyo mwaka 2006 lilipiga marufuku matumizi hayo wakati wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan jambo lililosababisha  upinzani mkubwa  kwenye mji wa Kismayu.
Hali ikawa hivyo nchini Kenya  Novemba 2006 wakati serikali ilipopiga marufuku  usafiri wa anga kwenda Somalia  kutokana na sababu za kiusalama hali  iliyoibua upinzani mkubwa kutoka kwa wakulima wa  mirungi.
Kutokana na hali hiyo  Mbunge wa Ntonyiri, wilaya ya Meru Kaskazini  alifahamisha kuwa ardhi ya  eneo hilo  imekuwa  inatumiwa kwa kulima mirungi na tani 20 zenye  thamani ya dola 800,000 zilikuwa zinasafirishwa kwenda Somalia  kila siku. Hivyo kupiga  marufuku usafiri  wa anga  kwenda Somalia  ilikuwa ni kuharibu  uchumi wa eneo hilo.
Ushindi kwa serikali ya mpito ikisaidiwa na majeshi ya Ethiopia  mwishoni mwa Desemba 2006 kulifanya  biashara ya mirungi kurudi kama kawaida katika barabara za Mogadishu  japo wafanyabiashara wa Kenya  walisema kuwa  biashara  haikufikia kiwango  kilichokuwepo awali kabla ya kupigwa marufuku.

Kudhibiti matumizi
Ripoti ya Shirika la Afya Duniani mwa 1965 ya timu ya wataalamu kuhusu kutegemea  uzalishaji wa mihadarati ilibainisha, “Kamati  imefurahishwa kuona kuwa Azimio la Baraza la Uchumi na Jamii ni vizuri matumizi ya  mmea huo yakadhibitiwa.”
Kutokana na hali hiyo mirungi haikuwekwa kwenye kundi la mihadarati lakini mwaka 1980 Shirika hilo liliweka matumizi ya mirungi yanaweza kusababisha utegemezi wa kisaikolojia.
Madhara ya mirungi  ni mengi  lakini baadhi yake ni  matatizo ya kisaikolojia kama vile ukatili, mtu anakuwa na tabia hiyo na jingine ni kukosa hamu ya kula.
Mtumiaji anaweza kukabiliwa na  vidonda vya tumbo, sanjari na vidonda mdomoni, kukosa choo kunakuambatana na kupungukiwa maji mwilini.
Madhara mengine ni  kukumbwa na shinikizo la damu  na kukosa  hamu ya kufanya mapenzi, kupungua kwa nguvu za kiume, mwili kuwasha, maumivu makali ya kichwa na  kuharibikiwa kwa ini.
Mbaya zaidi  mirungi husababisha mtumiaji kukosa usingizi  kwa muda mrefu  hivyo kuongeza uwezekanowa kupata  ajali  hususani kwa madereva wanaofanya  safari za mbali  na wanafunzi kushindwa kuelewa masomo darasani.

Comments