- Get link
- X
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- X
- Other Apps
NA ALOYCE NDELEIO
Alipokuwa akiwasilisha Bungeni Makadirio ya Mapato na
Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii Waziri wa wizara hiyo Dkt. Hamisi
Kigwangalla, alisema kuwa kanuni na taratibu
zitatumika kudhibiti biashara ya wanyamapori na mimea iliyo hatarini
kutoweka.
Aidha, eneo la wanyamapori hai alisema kuwa umeandaliwa
mpango madhubuti wa kusimamia kwa karibu kazi ya ukamataji wa wanyamapori hai
ikiwa ni pamoja na kufanya utafiti
utakaoonesha hali halisi ya wanyamapori na kushauri kuhusu biashara ya
wanyamapori hai.
Yote hayo yalikuwa sawa. Lakini licha ya biashara ya
wanyamapori hai ipo biashara ya nyama ya wanyamapori ambayo kimsingi inatishia
viumbe hivyo hususani vile ambavyo nyama yake hutumiwa na binadamu kama sehemu
ya lishe.
Matumizi ya nyama pori kihistoria na kiutamaduni ni chakula
kikuu cha jamii kulingana na shughuli zilizokuwa zinafanywa na jamii hususani zilizokuwa na
mfumo wa uzalishaji wa kuwinda wanyama na kukusanya matunda na mazao mengine ya
asili kama vyakula.
Ongezeko la idadi ya watu na kushuka kwa kiwango cha maisha
ni miongoni mwa sababu zinazochochea kuendelea kuwepo au kuongezeka kutegemea
kile kinachopatikana katika hali ya asili
au maliasili hiyo kama chanzo kikuu cha virutubisho na hususani protini
kwa wanajamii na hivyo kuifanya biashara hiyo kupanuka kutokana na wingi wa
mahitaji.
Matokeo ya ongezeko kama hilo na usimamizi mbovu wa vyanzo
vyake kumeifanya sehemu kubwa ya
biashara hiyo kuwa haramu licha ya kuwepo vizuizi vya kisheria.
Kwa mujibu wa Utafiti uliofanywa na taasisi ya Traffic ya
Mashariki na Kusini mwa Afrika kwa udhamini wa Kamisheni ya Ulaya kwa miaka
miwili unabainishwa kuwa nyama pori ni chanzo kikuu cha chakula na mapato
yanayotumika kuendeshea maisha kwa baadhi ya wanajamii.
Inabainishwa kuwa miongoni mwa nchi saba ulikofanyika
umekuwepo utegemezi mkubwa wa kupata protini inayotokana na nyama pori kwa njia
zisizo halali kuanzia wanyama wakubwa
kama tembo hadi aina mbalimbali za wadudu.
Utafiti unaarifu kuwa ongezeko la watu ndani ya jamii
zinazozunguka hifadhi huongeza mahitaji
ya nyama pori na hata kutishia uwepo wa wanyamapori kwani ni mara chache fununu
zinazohusu uwindaji haramu zimekuwa zinatolewa.
Utafiti huo unajulisha kuwa
tafiti nyingi za nyama pori zinaelekezwa maeneo ya Afrika Magharibi na
Kati, na kuyafanya matumizi ya nyama pori kuonekana ni tabia iliyojikita
kwenye maeneo ya misitu ya tropiki.
Ilibashiriwa kuwa
kuongezeka kwa matumizi na
biashara ya nyama pori kunaweza kuleta
athari kubwa kwa mazingira na hata kwa binadamu iwapo hatua za kudhibiti
hazitachukuliwa.
Unaarifu kuwa kimsingi inatakiwa matumizi ya nyama pori kwa
njia halali ufanyike kwa kuboresha mawasiliano kati ya hifadhi za wanyama na
sekta nyingine za mawasiliano.
Utafiti huo ulinuia kuangalia na kulinganisha biashara
halali na haramu ya nyama pori, faida za kiuchumi hususan kwa jamii za vijijini na athari za
uvunaji katika maeneo ya hifadhi na aina ya wanyama wanaopendelewa kibiashara.
Nchi saba zilizohusika kwenye utafiti huo ambako matumizi ya
nyama pori ni makubwa ni Botswana,
Kenya, Malawi, Msumbiji, Tanzania, Zambia na Zimbabwe
Kwa mujibu wa utafiti huo ilibainika kuwepo aina nyingi za
wanyama pori wanaolengwa na kutumiwa mara kwa mara huanzia wadudu, jamii ya panya na ndege,
wanyama wenye ukubwa wa kati hususan
jamii ya swala na wanyama wakubwa
kama tembo na nyati; na wanyama kama ngiri na jamii ya swala aina ya pala kwa ujumla hupendelewa kwani nyama yao kuwa
ina ladha nzuri.
Kati ya aina zote za wanyama wanaotumiwa katika maeneo
yaliyofanyiwa utafiti, nyati, swala pala na kudu wanawindwa sana na huchangia
kiasi kikubwa cha nyama inayopatikana. Hata hivyo, idadi ya wanyama wakubwa
inapungua kwani huwindwa kupita kiasi kwa kigezo kuwa wanaharibu mazingira.
Kupungua huko kunawafanya watumiaji wa nyama hiyo kubadilika
na kuwalenga wanyama wadogo
wanaopatikana katika maeneo hayo bila kusababisha uharibifu mkubwa wa
mazingira.
Utafiti huo wa Traffic umebaini kasi ya ongezeko la matumizi
ya nyama pori kupo sanjari na ongezeko
la haraka la idadi ya watu, kukithiri kwa umasikini na ukosefu wa ajira, hali
inayofanya nyama pori ionekane kama chanzo muhimu kitakachoinua hali zao za
maisha.
Inaarifiwa katika utafiti huo kuwa uwindaji wa aina ndogo za wanyama ni alama tosha
ya kupungua kwa kiwango kikubwa kwa wanyama pori na hususani aina
inayopendelewa zaidi.
Kupungua kwa idadi ya wanyama hao na kwenye maeneo husika
kunatokana na uwindwaji wa kupita kiasi na kuifanya bei yake kupanda hivyo
wawindaji na wafanya biashara kulenga
kila aina ya mnyama anayeingia kwenye mitego yao.

Aidha, moto wa kupata faida na kuongezeka kwa thamani ya
nyama pori umewafanya wawindaji kuongeza
kasi ya kupata nyama hiyo kwa namna yoyote ile hata kwa njia hatari hivyo
kuwepo kwa uwindaji usio endelevu wa matumizi ya nyaya, uwindaji wa kutumia
kurunzi nyakati za usiku na matumizi ya silaha kali zaidi kama bunduki za
machinegun.
Utafiti huo pia umebaini kuongezeka kwa mahitaji ya nyama
pori miongoni mwa jamii za Mashariki na Kusini mwa Afrika na matokeo yake ni
wanyama kukoseshwa muda wa kuzaliana na
kuongezeka pindi misimu ya uwindaji unapofungwa.
Hali kadhalika mfumo wa kitamaduni wa usimamizi katika
uwindaji kama vile kuchagua jinsia ya kuwindwa au kukataza kuwawinda wanyama
wenye mimba umekuwa hautiliwa maanani katika maeneo yote.
Hata hivyo, miiko inayowalinda wanyama nayo imekuwa
inapuuzwa na juhudi zinazofanywa na vyombo vya dola kukabiliana na uwindaji
haramu unaochochewa na mahitaji ya nyama pori zimepungua kwani adhabu
zinazotolewa ni faini ndogo ikilinganishwa na thamani ya nyama pori inayokuwa
imewindwa.
Uvunaji halali wa nyama pori unaweza kusaidia kukabiliana na
uwindaji haramu lakini kiwango kinachotakiwa hakifikiwi.
Kwa nchi zote saba zilizofanyiwa utafiti uvunaji wa nyama
pori kwa kutumia njia halali za vitalu vya wanyama au uwindaji wa leseni na
kupitia mikakati ya uwindaji kwa kudhibiti wanyama huwezesha kupatikana nyama
ya wastani wa mita 8,500 kwa mwaka; na kiwango hicho ni kidogo ikilinganishwa
na kiwango halisi ambacho kingetakiwa kuvunwa.
Kiongozi wa chama cha kulinda viumbe duniani, Dkt. Jane
Smart, amesema orodha ya viumbe vilivyo hatari barani Afrika kusini mwa jangwa
la Sahara ni kubwa na asilimia 20 inasababishwa na baishara haramu ya nyama ya
pori.
Kupotea kwa wanyamapori wanaowindwa kwa ajili ya nyama
huenda kukasababisha kupotea kwa mapato huku maeneo yakiachwa bila viumbe na
hivyo kutowavutia tena wageni. Jambo hili huenda pia lisababishe athari za
kiuchumi pamoja na hasira miongoni mwa wakazi wa maeneo hayo.
Hali kadhalika utafiti huo ulibaini kuwa mikakati ya uvunaji
halali inakwamishwa na sheria za nyama
ambazo hupendelea uzalishaji wa nyama kutoka kwa wanyama wanaofugwa hivyo kuwa
kikwazo kwa soko zuri la nyama pori.
Kwa vyovyote vile
lazima iwepo mikakati ya kudhibiti biashara hiyo pia kwani kuufanya
uvunaji wake kwa kuzingatia kanuni na taratibu kutalifanya soko lake kuwa la
uhakika na kufanywa uhai wa viumbe hivyo kuwa endelevu.
CHANZO: TANZANITE







Comments
Post a Comment