- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
NA MWANDISHI WETU
VIGOGO mbalimbali, wakiwemo wanasiasa na wafanyabiashara,
waliokopa kwenye Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa (Suma JKT)
na kushindwa kulipa wataanza kusakwa na kukamatwa Jumatatu, Julai 16, 2018.
Taarifa iliyotolewa wiki hii imeeleza kwamba, zoezi la
kuwasaka wadaiwa hao litaanza kutekelezwa mara moja ikiwa ni pamoja na kukamata
mali zao, ambapo litasimamiwa na Suma JKT Auction Mart.
Mei 17, 2018 akiwa katika hafla ya uzinduzi wa Kituo cha
Uwekezaji cha Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kupitia Suma JKT
kilichopo Mgulani, jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali
Venance Mabeyo, alimweleza Rais Magufuli kuwa, JWTZ linazidai sekta binafsi
Shs. bilioni 40, huku taasisi za Serikali zikidaiwa Shs. bilioni 3.4, jambo
ambalo limekuwa likiwakwamisha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimaendeleo.
Alisema ili kuliwezesha jeshi hilo kuwekeza katika miradi
mbalimbali ya maendeleo, Jenerali Mabeyo alimwomba Rais Magufuli apokee orodha
ya wadaiwa ili aongeze msukumo katika ulipaji wake.
Rais Magufuli alitoa mwezi mmoja kwa wadaiwa wote,
kuhakikisha wamelipa madeni na kuagiza baada ya kuisha kwa kipindi hicho,
mamlaka zinazohusika na ukusanyaji madeni pamoja na vyombo vya ulinzi na
usalama, kuwachukulia hatua kali wadaiwa wote.
Baadaye, Suma JKT iliwatangazia wote wanaodaiwa kupitia
tangazo lao la hivi karibuni kwa kuwataka wadaiwa kulipa kabla ya Juni 15, muda
ambao tayari umeshaisha.
Tangazo lingine lililotolewa na Makao Makuu ya SumaJKT la
Jumanne wiki hii likiwa na kichwa cha habari 'Lipeni madeni kwa wakati'
lilisema wale walioshindwa kutekeleza agizo hilo watachukuliwa hatua za
kisheria.
Pia tangazo hilo liliwaeleza wale waliopatiwa huduma ya
ulinzi na Suma JKT Guard na kushindwa kulipa kuwa huduma hizo zitasitishwa na
watachukuliwa hatua kali za kisheria ikiwamo kukamata mali zao kufidia deni
wanalodaiwa.
Inaelezwa kwamba, licha ya baadhi ya wadaiwa kuandika barua
kuomba wapewe muda zaidi ili walipe madeni hayo, lakini uongozi wa Suma JKT
umewagomea kwa maelezo kwamba, walikuwa na muda wa kutosha na hawakuweza
kulipa.
Mwanzoni mwa wiki hii kituo kimoja cha radio kiliikariri
taarifa ya uongozi wa Jeshi ikisema kwamba, uamuzi wa kuwakamata wadaiwa wote
unafuatia wadaiwa hao kushindwa kulipa kwa wakati licha ya kukumbushwa mara kwa
mara.
Hivi karibuni, Suma JKT ilitangaza kwenye tovuti yake
kuwataka wadaiwa wake walioshindwa kutekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli la kulipa madeni wanayodaiwa kwa wakati,
kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.
Aidha, tangazo hilo lilisema, kwa waliopatiwa huduma ya
ulinzi na SumaJKT Guard Ltd na kushindwa kulipia, huduma hizo zitasitishwa na
kuchukuliwa hatua kali za kisheria ikiwemo kukamata mali zao kufidia deni
wanalodaiwa.
Kwa mujibu wa orodha iliyotolewa na Suma JKT, jumla ya
wadaiwa 1,561 walikopa matrekta wakati taasisi 26 zinadaiwa malipo ya huduma ya
ulinzi.
Miongoni mwa wadaiwa sugu waliokopa matrekta na kushindwa
kulipa wamo pia mawaziri wa sasa, mawaziri wastaafu, wabunge na wakuu wa mikoa
wa sasa na wastaafu.
Baadhi ya majina ya mawaziri wa sasa yaliopo kwenye orodha
hiyo ni Waziri wa Uvuvi na Mifugo, Luhaga Mpina na Waziri wa Mambo ya Ndani,
Kangi Lugola.
Pia kwenye orodha hiyo yumo Naibu Waziri wa Wizara ya Uvuvi
na Mifugo, Abdallah Ulega, ambaye ni Mbunge wa Mkuranga.
Mawaziri wastaafu waliotajwa kwenye orodha hiyo ni Dkt. Juma
Ngasongwa aliyewahi kuwa Waziri wa Viwanda na Biashara na waziri wa wizara mbalimbali
kwenye serikali zilizopita.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Bara, Rodrick Mpogolo, ambaye
aliwahi kuwa Mkuu wa Wilaya ya Chato mkoani Geita pamoja na aliyekuwa Waziri wa
Fedha kwenye utawala wa awamu ya nne, Mustapha Mkulo nao wamo.
Wakuu wa mikoa wa sasa waliotajwa kwenye orodha hiyo ni
pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Christopher Ole Sendeka na Mkuu wa Mkoa wa
Sindiga, Dkt. Rehema Nchimbi.
Wabunge waliotajwa kwenye orodha hiyo ni pamoja na Husna
Mwilima wa Kigoma Kusini (CCM), Mbunge wa Shinyanga Mjini, Steven Maselle (CCM)
na Mbunge wa Singida Magharibi, Elibariki Kingu (CCM).
Wabunge wengine waliotajwa ni Ignas Malocha wa Jimbo la
Kwela (CCM), Mbunge wa Kilolo (CCM), Venance Mwamoto, Mbunge wa Korogwe Mjini
(CCM), Mary Chatanda, Mbunge wa Mtera (CCM), Livingstone Lusinde na aliyekuwa
Mbunge wa Songea Mjini (CCM), marehemu Laurence Gama.
Kwenye orodha hiyo pia wamo wabunge waliopita akiwemo
aliyekuwa Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila na aliyewahi
kuwa Mbunge wa Mbeya Mjini (CCM), Benson Mpesya (2000-2010).
Wabunge wengine waliopita waliotajwa ni aliyekuwa Mbunge wa
Manyoni Magharibi (CCM), Paul Lwanji, aliyekuwa Mbunge wa Afrika Mashariki
(CCM), Sylvia Kate Kamba, aliyekuwa Mbunge wa Mbarali (CCM), Modestus Kilufi na
aliyewahi kuwa Mbunge wa Kigoma Kusini (CCM), Manju Msambya.
Mwingine aliyetajwa ni aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa
Vijana wa CCM na mwanachama wa Chadema sasa, John Guninita.
Kwenye orodha hiyo pia ametajwa aliyewahi kuwa Mkuu wa Mkoa
wa Kigoma, Issa Machibya na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, marehemu Said
Mwambungu.
Taasisi za umma zinazodaiwa ni Wizara ya Afya, Maendeleo ya
Jinsia, Wazee, na Watoto, Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Wizara ya
Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Wizara ya Fedha na Mipango.
Nyingine ni Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida) Dar es
Salaam, Chuo cha Madini - Nzega, Stamigold - Biharamulo na Chuo cha Serikali za
Mitaa - Hombolo, na Halmashauri za Wilaya za Kasulu, Kibaha na Geita.
Wizara nne ni sehemu ya wadaiwa wa Suma JKT Guard Ltd ambapo
inaelezwa kwamba, hadi mwezi Mei 2018, deni lililokuwa limelipwa ni Shs.
bilioni 3.451 kati ya Shs. bilioni 4.057.
Halmashauri tatu ni miongoni mwa wadaiwa sugu waliokopa
matrekta kutoka Suma JKT ambao mpaka sasa deni lao limefikia Shs. bilioni 40.
Mnamo Juni 4, 2018, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Job Ndugai, alisema alikuwa amepokea orodha ya wabunge wanaodaiwa
fedha za matrekta na Suma JKT na walitakiwa kuwa wamelipa kabla ya Juni 23.
Baada ya kumalizika kipindi cha maswali na majibu.
Mei 17, 2018, Rais John Magufuli alitoa mwezi mmoja kwa
taasisi za Serikali na watu binafsi wanaodaiwa na Suma JKT deni la Shs. 41.4
bilioni kuhakikisha wanalipa.
"Wizara ya Ulinzi na JKT imewasilisha orodha kwa Ofisi
ya Spika ya wadaiwa wa fedha za matrekta na mnatakiwa kulipa madeni haya haraka
iwezekanavyo kabla ya Juni 23, 2018," alisema Spika Ndugai.
"Nina orodha ndefu hapa, sijui niisome? Kuna wengine
nimejaribu kuangalia basi hata wakatwe juu kwa juu kwenye fedha hizi tunazopata
pata, lakini hawana hata fedha kabisa... sina pa kukata, sasa kwa kweli
jitahidini tu," alisema Ndugai.
Mnamo Februari 27, 2013, Rais (mstaafu) Jakaya Kikwete
alilitaka Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMA JKT)
kulipa deni la Shs. 42 bilioni linalotokana na mkopo kutoka Serikali ya India
kwa ajili ya ununuzi wa matrekta ya 'Kilimo Kwanza'.
Serikali za India na Tanzania ziliingia mkataba wa mkopo wa
Shs. 40 bilioni kwa ajili ya ununuzi wa mtrekta ambayo yalikabidhiwa kwa Suma
JKT ili iyauze chini ya Mpango wa Kilimo Kwanza. Mkataba wa mkopo huo
ulisainiwa mwaka 2010 na ulipangwa kudumu kwa miaka mitano huku Tanzania
kupitia Suma JKT ikitakiwa kulipa Shs. 42 bilioni na riba.
JK alisema lengo la Serikali lilikuwa kuidhamini Suma JKT
kupata mkopo huo, ili kuendeleza Mpango wa Kilimo Kwanza ambao ulifanikiwa kwa
kiasi kikubwa.
CHANZO: FAHARI YETU
Comments
Post a Comment