Featured Post

OSCAR MILAMBO MKURUGENZI MPYA WA UFUNDI TFF



NA MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM
ALIYEKUWA kocha wa timu ya taifa ya vijana chini ua umri wa miaka 17, Oscar Milambo ameteuliwa kuwa Mkurugenzi mpya wa Ufundi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Uteuzi huo umefanywa na Kamati ya Utendaji ya TFF, baada ya kumhamishia Salum Madadi aliyekuwa Mkurugenzi wa Ufundi katika nafasi ya Mkurugenzi wa Mashindano.

Uamuzi huo umetolewa sambamba na maamuzi ya kumthibitisha Kidao Wilfred kuwa Katibu Mkuu wa TFF katika kikao kilichofanyika Julai 12, mwaka huu makao makuu ya TFF Karume, Ilala mjini Dar es Salaam.
Rais wa TFF, Wallace Karia, aliwasilisha suala la Kidao kwenye kikao hicho na wajumbe kulipitisha na kuthibitisha rasmi Kidao katika nafasi hiyo.
“Kamati ya utendaji pia imemthibitisha Salum Madadi kuwa Mkurugenzi wa Mashindano wa TFF. Nafasi ya Madadi aliyekuwa Mkurugenzi wa Ufundi iliyobaki wazi kamati ya utendaji imemthibitisha Kocha Oscar Mirambo kukaimu,” imesema taarifa ya TFF.
Katika hatua nyingine kikao hicho cha kamati ya Utendaji kimemuondoa Clement Sanga aliyekuwa mwenyekiti wa Bodi ya Ligi (TPLB) kwenye nafasi hiyo kwa kukosa sifa baada ya klabu ya Yanga kuwasilisha barua iliyokuwa na maelezo ya kwamba Yusuph Manji ndio mwenyekiti wa klabu hiyo.
Kamati ya Uchaguzi imeelekezwa kuandaa uchaguzi wa kuziba nafasi hiyo kamati ya utendaji imekubaliana kamati ya uchaguzi kuelezea mchakato mzima wa uchaguzi ulivyokuwa wakati Sanga anaingia Bodi ya Ligi.


Comments