- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
NA EMMANUEL J. SHILATU
NI takriban miaka miwili na nusu tangu Dkt. John Pombe
Joseph Magufuli ale kiapo mnamo Novemba 5, 2015 cha kuwa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania.
Lakini katika kipindi hiki cha nusu muhula, tumeyaona haya
yakitokea na kufanyika;-
1. Mapambano ya wazi wazi ya Serikali ya Rais Magufuli ya
vita dhidi ya rushwa na ufisadi nchini. Leo hii Tanzania imepanda kwa nafasi 13
katika mwaka 2016 na 2017 na pia ikishika nafasi ya pili (2) kwa nchi za
Jumuiya ya Afrika Mashariki.
2. Serikali ya Rais Magufuli imefanikisha zoezi zima la
Serikali kuhamia Dodoma.
Ni vyema tukakumbuka zoezi la kuhamia Dodoma liliasisiwa na
kushindwa kufanyika toka enzi ya utawala wa awamu ya kwanza wa Rais Mwalimu
Nyerere, lakini ndani ya kipindi kifupi cha miaka miwili tu Serikali ya Rais
Magufuli imeweza kuuvunja mfupa huu mgumu.
3. Ujenzi wa miundombinu ya kipekee na ya kisasa. Kupitia
Serikali hii ya awamu ya 5 ya Rais Magufuli tumeshuhudia ujenzi wa flyovers na
ujenzi wa reli ya kisasa kwa kiwango cha standard gauge inayotumia umeme na
inayokwenda kwa kasi. Hii haijawahi kutokea tangu Tanzania iumbwe.
4. Serikali ya awamu ya 5 ya Rais Magufuli hutumia Shilingi
bilioni 23 kila mwezi kulipia gharama za ELIMU BURE kuanzia elimu ya msingi
mpaka kidato cha nne.
Mara ya mwisho Tanzania kushuhudia elimu ikitolewa bure ni
katika utawala wa awamu ya kwanza ya Mwalimu Nyerere.
5. Mafisadi Papa, wala rushwa Papa wamepandishwa mahakamani
na wengine wanasota magerezani mpaka kesho. Katika miaka ya nyuma lilikuwa
suala gumu sana kwa watuhumiwa “Mapapa” kuguswa tu, achilia mbali kupandishwa mahakamani.
6. Tumeshuhudia akisimamia kwa vitendo kauli yake ya
Tanzania ya Viwanda.
Tangu Rais Magufuli aingie madarakani, zaidi ya viwanda
vikubwa na vidogo 3,000 vimezinduliwa na vinafanya kazi. Uwepo wa idadi kubwa
ya viwanda unasaidia sana kupunguza tatizo la ajira nchini.
7. Uwajibikaji na uadilifu kwa watumishi wa umma umeongezeka
na kuimarika vilivyo. Leo hii mtumishi wa umma hana majivuno, kiburi wala
dharau kwa wale anaowahudumia.
Siku hizi watumishi wa umma wanawahi makazini, wanachapa
kazi nyakati zote na wanazingatia ubora na umakini wa kazi.
8. Suala la matabaka ndani ya jamii linazidi kupungua kwa
kasi tangu utawala wa awamu ya 5 uingie madarakani.
Leo hii watoto wa maskini nao pia wanakwenda shule kupitia
sera ya elimu bure; hakuna tena ubabe wa dhuruma mahakamani, kwenye masuala ya
ardhi; leo hii hakuna tena zile kauli kandamizi za “unanijua mimi nani” ama
“Kijana kaa mbali, nitakupoteza”.
Hakika watu wanyonge maskini nao pia wanafurahia maisha
vilivyo, hakuna tena ubabe wala matabaka.
9. Serikali ya Rais Magufuli imeimarisha na kuzingatia suala
la amani na uhuru wa kidemokrasia ndani ya nchi. Mathalan Machi 5, 2018 tumesikia
Umoja wa Mataifa (UN) ukimpongeza Rais Dkt. Magufuli kwa kudumisha amani na
usalama ndani na nje ya Tanzania.
10. Kasi ya viongozi wa upinzani wakubwa kujiunga na CCM imekuwa
mkubwa sana. Tumeshuhudia Madiwani, Wabunge na viongozi waandamizi wa upinzani
wakijiunga na CCM ili kumuunga mkono Rais Magufuli kwa yale mambo mazuri ya
kiutendaji anayoyafanya.
Kujiunga kwa upinzani na dalili tosha ya watu kuridhishwa na
kiwango kikubwa cha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi
2015 – 2020.
11. Kufufuka kwa mashirika ya umma yaliyokuwa taabani.
Tumeona Shirika la Ndege (ATCL), Reli (TRL) na la Simu (TTCL) yakipata uhai
mara baada ya Dkt. Magufuli kuingia Ikulu.
Mathalan, upande wa ndege jumla ya ndege 6 mpya
zimeshanunuliwa, upande wa simu Serikali ya awamu ya 5 ilinunua hisa zote za
shirika za simu na hivyo kuanza kuimiliki kwa asilimia mia na kuanza
kuliboresha shirika. Matokeo yake imeweza kupokea gawiwo la shilingi bilioni
1.5.
12. Tumeshuhudia Serikali ikianzisha na kufanya miradi
mikubwa na ya kihistoria ya kimaendeleo.
Mathalan, tumeshuhudia ujenzi wa reli ya kisasa ya umeme kwa
kiwango cha Standard Gauge; Mradi wa ujenzi wa umeme wa Stiegler's Gorge
utakaokuwa chanzo kingine cha umeme na hivyo kupunguza tatizo la umeme nchini;
Ujenzi wa flyovers za Tazara na Ubungo ambayo itasaidia kupunguza msongamano wa
magari mkoani Dar es Salaam.
13. Kufutwa kwa kodi mbalimbali za kilimo, Serikali
kusimamia masoko ya bidhaa za wakulima na hivyo kufanya kilimo kuwa na tija
nchini.
Wote ni mashuhuda kwa namna gani Wakulima wa Korosho nchini
wanavyonufaika, ambao walikuwa wakiuza korosho kwa bei Tsh. 800 kwa kilo hapo
awali lakini tangu Rais Magufuli aingie Ikulu bei ya korosho imepanda hadi
kufikia bei ya Tsh. 4,000 kwa kilo. Maboresho hayo yapo hadi kwenye mazao
mengine.
14. Tumeshuhudia Serikali ya awamu ya 5 ikipambana vilivyo
na adui maradhi.
Mathalan, vifo vya wajawazito vimepungua kwa wastani wa
kitaifa wa 556/100,000; Idadi ya Wanawake wanaojifungulia vituoni imefika
wastani wa kitaifa wa asilimia; Upatikanaji wa dawa muhimu ni kwa asilimia 89
n.k. Pia tumeona kaya nyingi zikijiunga na mfuko wa afya ya jamii.
15. Tumeshuhudia Serikali ikiweka uwazi kwenye mikataba na
uchunguzi wa rasilimali za Taifa na kuweka makubaliano mapya yenye tija Mathalani
tumeona uwazi wa sekta ya madini ya dhahabu, almasi na Tanzanite ambapo Taifa
tumeona namna ambavyo tulivyokuwa tukiibiwa na Serikali kuweka mikakati mipya
ya kutokuibiwa tena.
Kama haitoshi tumeshuhudia wawekezaji wakibanwa vilivyo juu
ya mikataba isiyokuwa na tija kwa Taifa. Ni Serikali ya Rais Magufuli iliweka
uthubutu wa kuwabana wawekezaji wa madini wa
Acacia iliyozaa matunda kwa Serikali ya Tanzania kumiliki asilimia 16 ya
hisa katika makampuni ya uchimbaji wa madini, Serikali kupata gawio la faida ya
madini ya asilimia 50 kwa 50. Yote haya yamewezekana kwa sababu ya uzalendo
wake Rais Dkt. Magufuli.
Kwa utekelezaji huu unaofanywa na Serikali ya Chama Cha
Mapinduzi inayoongozwa na Rais Magufuli, wapinzani watapata tabu sana kwenye
uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2019 na Uchaguzi Mkuu 2020.
Comments
Post a Comment