- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
JASON NYAKUNDI NA ANTHONY IRUNGU, BBC SWAHILI
UNAMILIKI suti ngapi, viatu jozi ngapi, kofia ngapi, mashati
mangapi na mikanda mingapi na soksi pea ngapi? Ukihesabu bila shaka hautakosa
kugundua kuwa ni mavazi ya kukuwezesha kusukuma wiki moja au mbili hivi bila
kurudia.
Lakini kwa mwanamume mmoja mwenye makao yake jijini Nairobi,
Kenya hilo si tatizo.
Ana mavazi mengi ajabu, yanayojumlisha suti kamili za rangi
tofauti, viatu, kofia, mikanda, saa, pete na hata mifuko ya simu, mavazi ambayo
anaweza kuyavaa kwa zaidi ya siku mia moja bila kurudia.
Kila ukikutana naye kwenye mkusanyiko wa watu, hutakosa
kumtambua kutokana na mtindo wake wa kipekee wa kuvalia.
James Maina Mwangi ni mzaliwa wa Muranga kati kati mwa Kenya
anasema aliondoka nyumbani kwao na kuelekea jijini Nairobi kutafuta riziki
akiwa na umri wa miaka 12 baada ya kusoma hadi darasa la sita.
Anasema alipata changamoto kubwa za kuweza kupata mavazi ya
kutosheleza haja yake, hasa utotoni.
"Nikiwa mdogo nilikuwa na shati moja tu nililokuwa
nikilivua likikauka ninalivaa tena, na kuna wakati nilikuwa nikiazima nguo
kutoka kwa marafiki kama ninataka kwenda kutembea mahali, nikimuomba rafiki
ananijibu vibaya labda ananitusi au ananicheka," anasema.
"Ndipo nikamuomba Mungu anipe taji ambayo watu wengine
hawana, ndio wajue kuna Mungu tofauti na yule walikuwa wanamjua," anasema
Mwangi
Hadi sasa Mwangi anasema anamiliki zaidi ya suti 150, zaidi
ya jozi 200 za viatu na kofia zaidi ya 300 mavazi ambayo amekuwa akiyanunua nchini
Kenya na kuagiza mengine kutoka nchini za kigeni zikiwemo Afrika Kusini,
Italia, Uhispania, Ufaransa na Ujerumani.
Anasema anamiliki suti za kila rangi inayopatikana duniani
na huwa kawaida anavaa rangi moja kuanzia kofia, miwani, shati, tai, suti yenyewe,
viatu, soksi, saa, rangi ya simu na hata nguo za ndani.
Mwangi anasema suti moja inaweza kumgharimu kati ya shilingi
za Kenya 10,000 au dola 100 na shilingi 80,000 au dola 800.
"Mimi ni kama kioo kwa wananchi, watu wakiniona nimevaa
hivi hufurahi sana, wao hunisimamisha, hunisalimia na kuzungumza nami na kunipa
moyo kuendelea kuvaa hivi, na pia kuniombea mema, nafikiri ni mimi ndiye mtu
maridadi zaidi Afrika," Mwangi anasema.
Anasema kuwa kuvaa nadhifu lilikuwa ni ombi alilomuomba
Mungu tangu utotoni na anasema kuwa atazidi kuvalia hivyo hadi ile miaka Mungu
atamruhusu kuishi ulimwengu huu.
Miradi kwa vijana
Kando na mavazi ambayo yamechangia Mwangi kujulikana sehemu
tofauti duniani, amekuwa pia kiongozi wa vijana katika miradi mbali mbali
ambayo imewasaidia vijana tangu mwaka 1993.
Amesema ameongoza kuanzishwa kwa miradi ya vijana tangu
uongozi wa rais mstaafu Daniel arap Moi, ikiwemo ya uchukuzi wa mijini maarufu
kama 'matatu' iliyowaajiri vijana wengi.
Amechangia pia miradi mingine ya kuosha magari.
Mwangi pia anasema alipendekeza kuanzishwa kwa miradi ya
ujenzi wa masoko sehemu tofauti za nchi likiwemo soko maarufu la Muthurwa
lililo mjini Nairobi, na pia mradi wa umeme ambao uliwawezesha watu kupata
umeme sehemu za mashambani maarufu kama Rural Eletrification Project wakati wa
utawala wa rais mstaafu Mwai Kibaki.
"Nilipendekeza kuwepo miradi ya kujengwa barabara za
mashambani na hadi sasa miradi hii imewaajiri vijana na vijana wako na
kazi."
Mwangi anatoa ushauri kwa yeyote ambaye angependa kuiga mfano
wake kumheshimu Mungu Kwanza.
"Ukimheshimu Mungu na kufanya yanayostahili, Mungu
atakuinua na kukupa taji kushinda watu wengine na utakuwa mfano na kielelezo
kwa dunia."
Changamoto ambazo Mwangi anasema anakumbana nazo ni kuweza
kupata mavazi ya rangi sawa kwa wakati mmoja.
"Mara nyingi inachukua muda mrefu kuweza kupata mavazi
yote kwa pamoja kwa sababu ninaweza kupata suti na kofia lakini viatu viwe
vimechelewa kutokana na kukosekana kwa rangi ifaayo, kwa hivyo inanilazimu
kusubiri muda mrefu," anasema.
Kuna tofauti kati ya mtindo wa kuvaa wa Mwangi na ule wa
Sapewa Afrika ya Kati?
Mwangi anasema kuwa hajaiga mtindo wa kimavazi maarufu sana
nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na maeneo ya Afrika ya Kati kwa
jina Sape.
Mambo yalibadilika nchini DRC muda mfupi baada ya uhuru na
wakati Joseph Mobutu alichukua uongozi, alibadilisha jina la nchi hiyo na
kuiita Zaire na kuanzisha mtindo wa mavazi usio ule wa nchi magharibi.
Hata hivyo mwanamuziki Papa Wemba alionekana kulipinga hilo
lakini si kupitia kwa muziki.
Kwa hivyo alibuni mtindo wa kuvaa unaofahamika hadi sasa
kama Sepe unaomaanisha jamii ya watu nadhifu au wa kupendeza.
Kwa kuvisha bendi yake mavazi ya mtindo wa Sape watu nchini
DRC nao wakaufuata mtindo huo.
Tangu wakati huo na kutokana na vile mtindo huo umewapa watu
uhuru wa kujieleza, umewavutia wafuasi wengi eneo la Afrika ya kati na hata
mbali.
Mtindo wa Sapeur kwa sehemu fulani ni kama utamaduni na kwa
sehemu kubwa ni wa kuonyesha mavazi hasa yale ya nembo maarufu na ghali kutoka
nchi za ng'ambo na wale wanaovaa mtindo huo hawatili sana maanani kulinganishwa
kwa rangi mavazi yote kama suti, kofia na hata viatu.
Basi tofauti iliyowazi katika mtindo na Sape na wa Mwangi ni
kwama Mwangi hujaribu kwa vyovyote vile kulinganisha kwa rangi mavazi yake yote
yaliyo kwenye mwili wake kwa wakati mmoja.
BBC
Comments
Post a Comment