- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
NA ALOYCE NDELEIO
UMUHIMU wa vyama vya ushirika katika kuboresha maisha ya
mamilioni ya wakulima wadogo na familia zao hauwezi ukapingika kwani
umewawezesha kujiunga na kuunda kundi kubwa linaloweza kujadiliana katika suala
zima la uzalishaji endelevu.
Hatua hiyo ndio inaoufanya ushirika kuitwa kuwa ni ushirika
ni fimbo ya mnyonge.
Vyama vya ushirika kuanzia vyama vidogo hadi vikubwa vyenye
mitaji ya mamilioni ya fedha duniani vimekuwa vinaendeshwa kwenye sekta zote za
uchumi.
Vimekuwa vinahesabika kuwa vina zaidi ya wanachama milioni
800 na vinamudu kutoa fursa za ajira milioni 100 kiwango ambacho ni zaidi ya
asilimia 20 ya fursa zinazotolewa na
makampuni ya kimataifa.
Kutokana na hali hiyo wakulima wadogo wanaweza kuishi maisha
endelevu, kuboresha uhakika wa chakula ndani ya jumuia zao na kutoa mchango mkubwa katika ongezeko la
mahitaji ya chakula kwenye masoko ya ndani, kitaifa na kimataifa.
Mkombozi wa maskini
Katika warsha ya uwezeshaji wa vyama vya ushirika vya ngazi
za chini, iliyoandaliwa hivi karibuni na Mpango wa Utafiti na Elimu ya
Demokrasia Tanzania (REDET), Dar es Salaam, mmoja wa wataalam na mwanataaluma
wa masuala ya ushirika Mkuu wa Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi, mstaafu Profesa
Suleiman Chambo, alisema, vyama vya ushirika pekee ndivyo vyenye uwezo wa
kufika sehemu za vijijini tofauti na taasisi nyingine za fedha.
Profesa Chambo alisema kutokana na vyama vya ushirika kuwa
nguzo muhimu vijijini, ingekuwa vyema serikali kuangalia uwezekano wa kuvifufua
upya vyama hivyo ili wananchi waishio vijijini waweze kutoa mawazo yao badala
ya kuwatilia mkazo kutumia njia za taasisi nyingine.
Mwanataaluma huyo alisema iwapo ushirika utatiliwa mkazo
katika mikoa mbalimbali, hususani maeneo ya vijijini, utafufua uchumi wa taifa
kutokana na maeneo hayo kuwa na idadi kubwa ya wakulima ambao hawajui ni wapi
wanaweza kuwekeza.
Si jambo lililofichika kuwa wakati wa uhai wa vyama vya
ushirika wanachama waliweza kupata huduma za viwango vya juu hususan katika
suala la masoko ya mazao yao na hivyo kuwa nguzo yao ya karibu zaidi kuliko
vyombo vingine.
Kwa kiwango kikubwa vyombo hivyo vilikuwa ni swahiba mkubwa wa wakulima hasa
waliojishughulisha na kilimo cha mazao ya biashara kama vile kahawa na pamba na
si siri kuwa neema ilikuwa inawashukia.
Pamoja na hali hiyo, vyama hivyo katika miaka ya hivi karibuni
vimepitia katika kipindi kigumu kutokana na ubadhirifu uliofanywa na baadhi
ya walafi wachache ambao kwa kiasi
kikubwa walivihujumu.
Profesa Chambo alibainisha kuwa ushirika umezorota kwa sasa
kutokana na kuingiliwa na masuala ya siasa, hivyo kuvifanya vyama hivyo
kushindwa kujitawala kama ilivyokuwa awali.
Hapa jambo linalojiweka wazi ni kwamba masuala ya siasa
yalivizorotesha vyama vya ushirika kutokana na siasa zenyewe kujikita mno ndani
ya vyama hivyo na masuala hayo kuupa kisogo mchango uliokuwa umetolewa navyo
katika wakati wa mapambano ya kutafuta uhuru wa Tanganyika.
Ushirika ulichangia
kudai uhuru
Haiyumkiniki kuwa mchango wa vyama hivyo katika mapambano ya
kupatikana uhuru wa Tanganyika ni mkubwa na kwamba ni moja ya silaha
iliyotumiwa na waasisi wa Chama cha TANU kuwaunganisha wananchi.
Kwa wafutaliaji wa masuala ya historia ya mapambano ya
uhuru, hakuna atakayebeza mchango uliotolewa na Shirikisho la Vyama vya
Ushirika Kanda ya Ziwa (Victoria
Federation of Cooperative Unions (VFCU) chini ya uongozi wa Hayati Paulo
Bomani.
Aidha, ni kupitia ushirika huo, Chama cha TANU, kiliweza
kuzoa wanachama wengi katika kanda hiyo na hivyo kukiongezea nguvu katika
harakati zake za kuikomboa Tanganyika.
Ni wazi kuwa haikuwapo njia nyingine rahisi ya kuwafikia
watu walioishi ndani vijijini na kuwawezesha kupokea sera zilizokuwa
zinasambazwa na TANU, tena kwa siri kama si ushirika huo.
Kwa vyovyote vile kufufua vyama hivyo itakuwa ni kuendeleza
historia na kuthamini mchango wake katika kumkomboa mwanajamii wa leo ambaye
anajivunia kuwepo kwa Tanzania huru.
Vyama vya ushirika havikuishia kwenye utando wa kusukuma
mbele mapambano ya kupatia uhuru bali pia viliangalia nyanja ya uchumi na
uwezeshwaji wa wanachama wake kwa njia ya mikopo.
Kwa vyovyote vile, ndivyo vilikuwa vyanzo vya awali vya
kutoa mikopo miongoni mwa wakulima waliokuwa wanachama wake, ikiwa ni njia moja
ya kuhakikisha kuwa uzalishaji wa mazao yao unakuwa endelevu kwa upande mmoja
na kwa upande mwingine wakiwa wanakidhi mahitaji yao muhimu ya maisha.
Miongoni mwa vyama vya ushirika vikongwe barani Afrika na
ambacho ni cha kujivunia leo hii hapa nchini ni Chama cha Ushirika cha Wazawa
Kilimanjaro (Kilimanjaro Native Cooperative Union (KNCU)), ambacho kimekuwa
kinashughulika na wakulima wa zao la kahawa aina ya Arabica.
Kikiwa kimeanzishwa mwaka 1924 pamoja na vyama vingine vya
ushirika, vilivunjwa mwaka 1976 lakini mwaka 1984 vilianzishwa tena na hivi
sasa KNCU ina vyama vya msingi 90.
Aidha, chama hicho kilipata tuzo ya uthibitisho wa kushiriki
ya Shirika la Maonyesho ya Biashara (FLO) mwaka 1993. Lakini muhimu ni kwamba
wanachama wamekuwa wanashiriki katika kuchagua viongozi wa chama kwa njia ya
kidemokrasia na kuwa na wawakilishi kutoka kila chama cha msingi.
Kikiwa ni chama kilichojizatiti, kilianzisha mfuko wa elimu
ambao wanachama wake wamekuwa wanachangia kwa hiari na umetumika kujenga na
kuendesha shule kwa ajili ya watoto wa wakulima na hata kulipia baadhi ya
watoto wa wakulima wa zao hilo ada za masomo yao.
Moja ya shule zilizojengwa na kusimamiwa na KNCU ni Shule ya
Sekondari ya Lyamungo, ambayo ni moja ya shule kongwe hapa nchini.
Haiyumkini Profesa Chambo pia aliguswa na hali kwamba chuo
kikuu hicho ambacho yeye alikuwa ni mkuu wake ni moja ya matunda ya kazi za
Chama cha Ushirika cha KNCU.
Hadi miaka ya hivi karibuni kabla ya kuingia kwa soko huria
na kampuni za watu binafsi kuanza kununua zao hilo wanachama wake walikuwa
wameridhia kukatwa kiasi fulani cha fedha kwa kila kilo moja ya kahawa
waliyouza kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa shule mbalimbali za sekondari mkoani
humo.
Makato ya fedha hizo pale ilipotokea kuwa shule
inayochangiwa ipo katika kata ambayo ndani yake kuna chama cha msingi cha
ushirika hayakuwa na ubishi bali yalikuwa ni jambo lisilopingika.
Hali hiyo ikawa ni mvuto kwa vyama vingine vya msingi
kuchangia shule na hivyo kuwa moja ya sababu zilizochangia kupanuka kwa elimu
mkoani humo.
Kutokana na kuingia kwa kampuni na watu binafsi katika
ununuzi wa zao hilo, basi michango iliyokuwa inapatikana kwa ajili ya maendeleo
ya ujenzi wa shule hizo nayo ikawa imefikia ukomo kama si kifo.
Chama hicho pia kina Benki ya Ushirika Kilimanjaro
(Kilimanjaro Cooperative Bank (KCB) ambayo imewezesha wakulima kupata mikopo
kutoka kwenye huduma ya kuweka na kukopa.
Hata hivyo licha ya kufikia kiwango cha kuanzisha benki, ni
vyema kuangalia ni vipi ushirika ulikuwa karibu na mkulima wa kijijini katika
kumwezesha kupata mikopo.
Awali ilikuwa ni rahisi kufanya sensa ya miche ya kahawa
ambayo mkulima alikuwa nayo na ilikuwa rahisi kufanya makadirio ya mazao
atakayovuna kwa msimu.
Takwimu hizo zilitumika katika kutoa mikopo, na kwa hali
hiyo amana aliyokuwa nayo mkulima ilikuwa tayari imeshafanyiwa tathmini.
Aidha, mikopo mingine ilikuwa ni endelevu kwa sababu
ilimzalishia mkulima. Mfano mkulima aliweza kupata mkopo wa ng’ombe wa maziwa
na gharama yake akawa anailipa kwa kukatwa kwenye mauzo ya kahawa taratibu na
alipomaliza aliweza kuomba mkopo mwingine kwa ajili ya shughuli nyingine.
Kwa namna moja au nyingine, ni dhahiri kuwa vyama vya kuweka
na kukopa (SACCOS) vilikuwa tayari vimo ndani ya Chama cha Ushirika Kilimanjaro
(KNCU).
Ni dhahiri kuwa amana aliyonayo mkulima ni mazao anayolima
na hiyo ndiyo ilikuwa inamwezesha kupata mikopo kutoka kwenye chama chake cha
ushirika ambacho ndicho kinafahamu fika hali ya uzalishaji ndani ya amana yake.
Kwa maana hiyo taasisi nyingine za fedha si rahisi kufikia
misingi hiyo, kwa kuwa zenyewe zinaweza zisione amana kama dhamana
zitazowawezesha wakulima kupatiwa mikopo.
Comments
Post a Comment