- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
MKOA
wa Tabora umedhamiria na kuweka mikakati ya kupambana kuhakikisha unaondokana
na utumikishwaji wa watoto unaosababisha utoro shuleni, mimba na ndoa za
utotoni.
Matukio
hayo ndiyo yanayodaiwa kusababisha mkoa huo kuongoza kwa utoro kitaifa na hivyo
kupoteza dira ya watoto hao.
Mkuu
wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi
na Usalama ya Mkoa, alieleza hayo juzi wakati akifungua rasmi warsha ya Mkakati
wa Taifa wa kutokomeza utumikishwaji wa watoto nchini iliyoandaliwa na Shirika
la Kazi Duniani (ILO) kwa kushirikiana na asasi ya ARISE ya mjini hapa kwenye
ukumbi wa Georges Complex uliopo Kata ya Cheyo A mjini hapa.
Mwanri
alisema kuwa, mkoa huo umedhamiria kuondokana na utumikishwaji wa watoto kwa
kuorodhesha majina ya watoto wote wanaotumikishwa, watoro, wenye mimba na
walioolewa ikiwa ni pamoja na majina ya wazazi ama walezi wao ili hatua kali za
kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi ya wahusika wote.
Alieleza
kuwa, amewaagiza viongozi na watendaji wote kuanzia ngazi ya vijiji, vitongoji,
kata na wilaya zote kuorodhesha majina yote ya walengwa na kuyapeleka ofisini
kwake na yeye atamkabidhi Kamanda wa Polisi (RPC) mkoani humo, ambaye
atawakabidhi wakuu wa polisi wa wilaya zote ili kuwakamata wahusika wote na hatua
za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yao.
“Haiwezekani mkoa huu uwe unaongoza kwa
matukio mabaya tu, utumikishwaji wa watoto, utoro, mimba na ndoa za utotoni, mauaji
ya watu kwa imani potofu za kishirikina, yote haya tunaongoza wakati viongozi
tupo na wahusika wanafahamika.
"Nasema
sasa basi na hakuna jiwe litakalobakia juu ya jiwe na nitahakikisha Tabora
inaondokana na yote hayo na kuwa Taa Bora na itabakia historia,” alieleza mkuu
huyo wa mkoa.
Kwa
upande wake, Askofu Mkuu wa Dayosisi mpya ya Magharibi na Kati ya Kanisa la Kiinjili
la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dkt. Isaack Leizer Kissiri, akitoa salamu zake
kwa niaba ya madhehebu yote, alieleza
kuwa, wao kama watumishi wa Mungu watafundisha kwa vitendo na kusimamia msimamo
wa serikali katika kutokomeza utumikishwaji wa watoto nchini.
Askofu
Kissiri alisema kuwa, watapambana kutoa elimu kwa waumini wao na jamii nzima na
kuhakikisha wanapatikana raia wema wenye maadili yanayoendana na Taifa pamoja
na kuiunga mkono serikali kuhakikisha inaboresha maisha ya wananchi na serikali
kwa ujumla.
Naye
Kamishna Msaidizi wa Kazi wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Watu
wenye ulemavu), Hawa Wenga, alisema serikali itaandaa sera na sheria kwa
kuwashirikisha wadau mbalimbali katika kupingana na utuimikishwaji wa watoto
nchini.
Wenga
alisema kwamba, serikali itaendelea kushirikiana na asasi mbalimbali katika
kupambana na utumikishwaji huo wa watoto na kuhakikisha kunakuwapo na kizazi
salama chenye afya bora kama ilivyo kauli mbiu ya Taifa ya siku hiyo ya kupinga
utumikishwaji huo.
Mratibu
wa Taifa wa asasi yenye mradi wa kutokomeza utumikishwaji wa watoto katika
jamii ya wakulima wa tumbaku mkoani Tabora (ARISE), Dkt. Gerson Nyadzi, alisema
kuwa mradi huo unatekelezwa katika wilaya za Uyui na Urambo mkoani humo tangu Julai
2016 ambapo wameweza kuwaibua zaidi ya watoto 94 waliokutwa wakitumikishwa
katika mashamba ya tumbaku.
Dkt.
Nyadzi alisema, kati ya watoto hao, wa kiume ni 61 na wa kike ni 33 wanatoka
katika Kijiji cha Migungumalo, Kata ya Usagali, Wilaya ya Uyui mkoani hapa
ambacho kinakadiriwa kuwa na watoto 1,145 wakiwemo wasichana 582 na wavulana
563, kwa mujibu wa Ofisa Mtendaji wa Kijiji, Azizi Makungu.
Alisema,
asasi hiyo imeweza kuwaelimisha wazazi na walezi wa watoto hao pamoja na watoto
wenyewe na baadhi yao wamerejea shuleni, wengine wamepatiwa elimu ya
ujasiriamali wa kutengeneza bidhaa mbalimbali kama batiki na sabuni za maji
kupitia asasi ya JIDA na wengine watapatiwa mifugo ya kuku, mbuzi na nguruwe
ili familia zao ziwafuge hadi watoto hao watakapofikisha umri wa kujitegemea
ndipo watakabidhiwa ili kujikomboa kiuchumi.
Comments
Post a Comment