- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
NA WAANDISHI WETU
SERIKALI
imewasilisha Makadirio ya Bajeti ya Shilingi trilioni 32.48 kwa Mwaka wa Fedha
2018/2019 yenye vipaumbele vikubwa vinne huku ikilenga kulinda viwanda vya
ndani kwa kutopandisha ushuru wa baadhi ya bidhaa.
Mbali ya
kutopandisha ushuru wa bidhaa zinazozalishwa na viwanda vya ndani, Serikali pia
imefuta baadhi ya ushuru, ukiwemo wa taulo za kike, lengo likiwa kulinda afya
za wanawake na wasichana.
Akiwasilisha
makadirio hayo bungeni jijini Dodoma jana, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt.
Philip Mpango, alisema bajeti ya matumizi katika mwaka 2018/19 itaweka mkazo
zaidi katika uendelezaji wa miradi ya kielelezo, kufungamanisha maendeleo ya
watu, na ujenzi wa mazingira wezeshi kwa ajili ya uwekezaji na uendeshaji
biashara.
Alisema
kwamba, Serikali imeyaangazia maeneo manne ya kipaumbele - kilimo, viwanda,
huduma za jamii, na miundombinu wezeshi - ambayo wachambuzi wa masuala ya
uchumi wanasema, bajeti hiyo inaendana na azma ya Serikali ya kuifanya Tanzania
kuwa nchi ya viwanda na yenye uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.
Kuhusu kilimo, Dkt. Mpango alisema kwamba, fedha zitaelekezwa zaidi kuboresha
miundombinu ya umwagiliaji, maghala na masoko, kuimarisha upatikanaji wa pembejeo na zana za kilimo, kupanua huduma za
ugani, kuboresha mfumo wa utafiti na utoaji wa matokeo ya utafiti kwa wananchi,
na uendelezaji wa sekta ndogo za uvuvi na mifugo.
"Mkazo umewekwa
katika sekta hii kwa kuzingatia kuwa inategemewa na wananchi wengi na ndiyo
itakayotupatia malighafi kwa ajili ya viwanda, kutuhakikishia usalama wa
chakula na kuongezeka kwa kipato cha wananchi," alisema.
Aidha, alisema, katika
kuchochea ukuaji wa viwanda nchini, Serikali itaelekeza nguvu zake kwa
kutekeleza Mpango wa Kuboresha Mfumo wa Udhibiti wa Biashara ili kuvutia uwekezaji
wa sekta binafsi hususan viwanda vya nguo, ngozi na nyama, samaki, mafuta ya
kula, madawa na vifaa tiba, vyakula vya binadamu na mifugo, na katika sekta ya
madini.
Katika huduma za
jamii, bajeti hiyo imelenga maeneo ya maji, elimu na afya.
"Eneo lingine
muhimu ni kuongeza upatikanaji na usambazaji wa maji safi hasa vijijini na
uondoshaji wa majitaka, uchimbaji wa visima katika maeneo kame nchini na ujenzi
wa mabwawa makubwa ya kimkakati.
"Serikali
itaendelea kugharamia elimu msingi bila ada, kuongeza idadi ya
wataalam katika fani adimu kwenye maeneo ya madini, mafuta na gesi, madaktari
bingwa (moyo na figo) pamoja na utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya
juu," alisema.
Kuhusu afya, Dkt.
Mpango alisema, rasilimali fedha zitaelekezwa kuongeza usambazaji wa dawa, vifaa tiba, vitendanishi na uboreshaji wa huduma katika vituo vya afya, zahanati na hospitali za rufaa.
Aidha, alisema,
Serikali itaelekeza fedha zaidi za LGCD
kwenye miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Halmashauri, hususan miradi ya
elimu na afya.
"Serikali itaweka
msukumo kuimarisha upatikanaji wa lishe
bora kwa mama na mtoto hususan katika siku 1,000 za mtoto tangu kutungwa kwa
mimba ili kuondokana na changamoto ya kuwa na watoto wenye udumavu na hivyo kukua
vema kimwili na kiakili.
"Aidha, mahitaji
ya makundi maalum katika jamii yetu
(wanawake, vijana, watoto, watu wenye ulemavu na wazee) yataendelea kuangaliwa
kipekee," alisema.
Bajeti hiyo pia
inalenga kujenga na
kukarabati miundombinu wezeshi
hususan kuongeza uzalishaji wa umeme kwa kutumia vyanzo mbalimbali, kuendelea
na ujenzi wa reli mpya ya kati kwa kiwango cha kimataifa (standard gauge), ujenzi wa barabara za kuunganisha mikoa na zile za
vijijini, na kuimarisha usafiri wa anga na majini.
Alisema maeneo mengine ya kipaumbele ni
kurahisisha umiliki wa ardhi, kuimarisha
huduma za mawasiliano, kifedha na utalii
na kuimarisha ulinzi, usalama, utawala bora, na utoaji haki.
Ushuru wa Bidhaa
Waziri Mpango alisema
kwamba, kwa mujibu wa Sheria ya Ushuru wa Bidhaa Kifungu cha 124(2),
marekebisho ya viwango maalum vya Ushuru wa Bidhaa (specific duty rates) zisizo za petroli yanaweza kufanyika kila
mwaka ili kuviwianisha na mfumuko wa bei na viashiria vingine vya uchumi jumla.
Hata hivyo, alisema, ili
kutekeleza azma ya Serikali ya awamu ya tano ya kujenga uchumi wa viwanda, imependekezwa
kutofanya mabadiliko ya viwango maalum vya Ushuru wa Bidhaa zisizo za petroli
zinazozalishwa nchini na kuongeza viwango vya Ushuru wa Bidhaa zisizo za
petroli zinazoagizwa kutoka nje.
Alisema, Ushuru wa Bidhaa kwenye
vinywaji baridi utaendelea kutozwa kwa kiwango cha shilingi 61 kwa lita.
"Ushuru wa Bidhaa kwenye
maji ya kunywa yaliyosindikwa kwenye chupa yaliyoagizwa kutoka nje utaongezeka
kutoka shilingi 61 kwa lita hadi shilingi 64.05 kwa lita. Aidha, Ushuru wa
Bidhaa kwenye maji yanayozalishwa hapa nchini utaendelea kutozwa kwa kiwango
cha sasa cha shilingi 58 kwa lita,"
alisema.
Alisema kwamba, Ushuru wa Bidhaa kwenye maji ya
matunda (juisi) iliyotengenezwa kwa matunda yanayozalishwa nchini (local juices) hautaongezeka na
utaendelea kutozwa kwa kiwango cha shilingi 9 kwa lita.
Hata hivyo, Ushuru wa Bidhaa kwenye juisi
zilizotengenezwa kwa matunda ambayo hayazalishwi nchini (imported juices) utaongezeka kutoka shilingi 221 hadi shilingi 232
kwa lita.
Ushuru wa Bidhaa kwenye bia inayotengenezwa kwa
nafaka ya hapa nchini na ambayo haijaoteshwa hautaongezeka na utaendelea
kutozwa kwa kiwango cha shilingi 450 kwa lita, wakati bia zinazoagizwa kutoka
nje zitatozwa shilingi 803.25 badala ya shilingi 765 kwa lita.
"Ushuru wa Bidhaa kwenye bia zisizo za
kilevi, ikijumuisha vinywaji vya kuongeza nguvu vinavyoagizwa kutoka nje utaongezeka
kutoka shilingi 561 hadi shilingi 589.05 kwa lita, na bia zisizo za kilevi,
ikijumuisha vinywaji vya kuongeza nguvu vinavyozalishwa nchini utaendelea
kutozwa kwa kiwango cha sasa cha shilingi 561 kwa lita," alisema Waziri
Mpango.
Dkt. Mpango alisema, Serikali itaanzisha Ushuru
wa Bidhaa wa shilingi 200 kwa lita kwenye mvinyo uliotengenezwa kutokana na
usindikaji wa matunda (kama ndizi, rozela/choya, nyanya, nk) yanayozalishwa
hapa nchini tofauti na zabibu kwa kiwango kinachozidi asilimia 75.
Aidha, Ushuru wa Bidhaa kwenye mvinyo
uliotengenezwa kwa zabibu inayozalishwa ndani ya nchi kwa kiwango kinachozidi
asilimia 75 hautaongezeka na utaendelea kutozwa kwa kiwango cha shilingi 200
kwa lita, wakati ambapo kwenye mvinyo uliotengenezwa kwa zabibu inayozalishwa
nje ya nchi kwa kiwango kinachozidi asilimia 25, utaongezeka kutoka shilingi
2,349 hadi shilingi 2,466 kwa lita.
Ushuru wa Bidhaa kwenye vinywaji vikali
vinavyoagizwa kutoka nje utaongezeka kutoka shilingi 3,481 hadi shilingi 3,655.05
kwa lita, na Ushuru wa Bidhaa kwenye vinywaji vikali vinavyozalishwa nchini
hautaongezeka na utaendelea kutozwa kwa kiwango cha shilingi 3,315 kwa lita.
Kwa upande mwingine, Ushuru wa Bidhaa kwenye
sigara zisizo na kichungi zinazotengenezwa kutokana na tumbaku inayozalishwa
hapa nchini kwa kiwango cha angalau asilimia 75, hautaongezeka na utaendelea
kutozwa kwa kiwango cha shilingi 12,447 kwa kila sigara elfu moja.
Ushuru wa Bidhaa kwenye sigara zenye kichungi
zinazotengenezwa kutokana na tumbaku inayozalishwa hapa nchini kwa kiwango cha angalau
asilimia 75, hautaongezeka na utaendelea kutozwa kwa kiwango cha shilingi
29,425 kwa kila sigara elfu moja.
"Ushuru wa Bidhaa kwenye sigara zenye sifa
tofauti na hizo zilizotajwa juu utaongezeka
kutoka shilingi 53,235 hadi shilingi 55,896.75 kwa kila sigara elfu moja ikiwa
ni ongezeko la shilingi 2,661.75 kwa kila sigara elfu moja.
"Ushuru wa Bidhaa kwenye tumbaku ambayo iko
tayari kutengeneza sigara (cut filler)
inayoagizwa kutoka nje utaongezeka kutoka shilingi 26,888 hadi shilingi
28,232.4 kwa kilo, ikiwa ni ongezeko la shilingi 1,344.4 kwa kilo; na Ushuru wa
Bidhaa wa ‘cigar’ unabaki kuwa asilimia 30," alisema.
Comments
Post a Comment