Featured Post

WALEMAVU KISARAWE KUPATIWA BIMA YA CHF ILIYOBORESHWA

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI Selemani Jafo  akizungumza na wananchi wa Kisarawe.
baadhi ya watu wenye ulemavu  waliokabidhiwa vifaa wezeshi.
 
 Baskeli za watu wenye ulemavu walizokabidhiwa.
 Baadhi ya wananchi wa Kisarawe walio hudhuria mkutano wa ugawaji wa vifaa wezeshi vya walemavu.

……………………………………………….
Wilaya ya Kisarawe huenda ikawa wilaya ya mfano hapa nchini kwa wananchi wake wote wenye ulemavu kupatiwa bima ya afya iliyoboreshwa.  
Neema hiyo kwa walemavu imetokea leo wakati wa zoezi la ugawaji wa vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu vilivyo tolewa na shirikisho la watu wenye ulemavu nchini(SHIVYAWATA).
Katika hafla hiyo ya ugawaji vifaa saidizi,  Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI Selemani Jafo  ambaye pia ni mbunge wa wilaya hiyo ya Kisarawe ametangaza neema hiyo kwa walemavu hao kwa kumtaka Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kisarawe kufanya utaratibu wa kupata Sh.milioni 6 kutoka mapato ya ndani ili kuwalipia CHF iliyo boreshwa kwa vikundi 207 vya walemavu.
Amesema lengo ni walemavu wote wa wilaya hiyo wawe na uhakika wa kupata huduma ya afya ambapo kwasasa wilaya ya Kisarawe ina jumla ya watu wenye ulemavu  wapatao 1608. 
Waziri Jafo ametoa msisitizo kwamba kwa Halmashauri ya wilaya ya Kisarawe haiwezi kushindwa kupata sh.milioni 6 ili kuwalipia walemavu.
Baada ya maelekezo hayo,  Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kisarawe Mussa Gama amethibitisha Waziri Jafo kuwa watahakikisha wanatekeleza agizo hilo kabla mwezi Juni 2018. 
Katika hatua nyingine, Mkuu wa mkoa wa Pwani Eng. Ndikilo amemuagiza Katibu Tawala wa mkoa wa Pwani  Zuberi Samataba  awaandikie wawekezaji wote wa viwanda wa mkoa wa Pwani waone namna watakavyoweza kuchangia vifaa saidizi cha walemavu ili walemavu wengine waliobaki waweze kusaidiwa vifaa hivyo wezeshi. 
Naye, Mkuu wa wilaya ya Kisarawe Mhe. Happiness Seneda ameitaka jamii kushirikiana ili kuwasaidia watu wenye ulemavu wilayani Kisarawe.

Comments