Featured Post

KOCHA WA PSG, RASMI ACHUKUA MIKOBA YA ARSENE WENGER NDANI YA ARSENAL

Unai Emery ametambulishwa rasmi kuwa kocha mpya wa Arsenal akichukua nafasi ya Arsene Wenger.
KOCHA Unai Emery amesema kwamba amepewa heshima ya kujiunga na klabu kubwa baada ya kutangazwa kuchukua nafasi ya Arsene Wenger klabu ya Arsenal kwa mkataba wa miaka mitatu wenye thamani ya Pauni Milioni 15.
Kocha huyo wa zamani wa Paris Saint-Germain amempiku kiungo wa zamani wa Arsenal, Mikel Arteta katika kuwania nafasi hiyo ya kazi Uwanja wa Emirates.
Emery sasa anakwenda kuchukua mikoba iliyoachwa na Wenger, ambaye amekuwa kazini Kaskazini mwa London kwa zaidi ya miaka 22.
Arsenal imefichua habari hizo Saa 3 asubuhi ya leo kwa mumtangaza Emery: “Mpya ametua. Zama mpya. Ukurasa mpya,”. Mspaniola huyo atatangazwa rasmi katika mkutano na Waandishi wa Habari mchana wa leo.
Historia ya Emery inaanzia alipokuwa mchezaji wa Real Sociedad ambako alicheza mechi tano za La Liga wingi ya kushoto kabla ya kuhamia Toledo ya Daraja la Pili.
Mwaka 2005-2006 akageukia ukocha akianza na klabu ya Lorca Deportiva aliyoipandisha Daraja la Pili kwa mara ya kwanza, kabla ya mwaka 2006-08 kwenda Almeria ambayo aliipandisha Ligi Kuu kwa mara ya kwanza kwenye historia ya klabu hiyo.
Mwaka 2008 akaenda Valencia ambako alidumu hadi 2012 akiiwezesha kushika nafasi ya tatu mara tatu mfululizo katika La Liga, kabla ya kuhamia Spartak Moscow, ambako hata hivyo hakudumu, kwani baada ya kupoteza mechi 11 katika miezi sita alifukuzwa baada ya kufungwa 5-1 nyumbani na Dynamo Moscow. 
Akaenda Sevilla ambako alishinda mataji matatu mfululizo ya Europa League kati ya 2013 na 2016 kabla ya kujiunga na PSG mwaka 2016 ambako alishinda mataji yote matatu ya nyumbani na sasa anaingia Arsenal. 

WASIFU WA KOCHA UNAI EMERY  

Kuzaliwa: Hondarribia, Hispania Novemba 3, 1971
MCHEZAJI
Alianzia Real Sociedad, akacheza mechi tano za La Liga wingi ya kushoto kabla ya kuhamia Toledo ya Daraja la Pili.
KOCHA
2005-06 Lorca Deportiva Akaipandisha Daraja la Pili kwa mara ya kwanza 
2006-08 Almeria
Akaipandisha Ligi Kuu kwa mara ya kwanza kwenye historia ya klabu
2008-12 Valencia
Wakashika nafasi ya tatu mfululizo katika La Liga 
2012 Spartak Moscow
Akapoteza mechi 11 katika miezi sita. Akafukuzwa baada ya kufungwa 5-1 nyumbani na Dynamo Moscow. 
2013-16 Sevilla
Akashinda mataji matatu mfululizo ya Europa League 
2016-18 Paris Saint-Germain
Akashinda mataji yote matatu ya nyumbani 
Matokeo ya Ukocha
Amecheza mechi 719, ameshinda 385, sare 155, amefungwa 179 na asilimia ya ushindi 53.5 
MATAJI
Sevilla
Europa League (x3): 2014, 2015, 2016
Paris Saint-Germain
Ligue 1: 2017-18
Kombe la Ufaransa (x2): 2017, 2018
Kombe la Ligi Ufaransa (x2): 2017, 2018
Super Cup ya Ufaransa (x2): 2016, 2017

Comments