Daktari wa mifugo katika kiwanda hicho akitoa maellekezo ya sehemu mbali mbali za kiwanda hicho mbele ya Naibu waziri wa muungano na mazingira Kangi lugora jana jijini hapa
Na Mahmoud Ahmad Dodoma
Kiwanda cha nyama cha Tanzania (TMC) kimepigwa faini ya Milion 5 baada ya kukiuka kanuni za uhifadhi wa mazingira na kuchelewa kutekeleza agizo walilopewa kuhakikisha wanafanyiakazi maagizo
waliyopewa juu ya kufanyiakazi kanuni za utunzaji wa mazingira ikiwemo kufanya
tathmini mazingira kabla ya kuanza kazi.
Akizungumza wakati akikagua machinjio hayo na kiwanda hicho cha nyama Naibu waziri wa nchi Ofisi ya makamu wa Rais Muungano na Mazingira Kangi Lugola ambapo Ameelezea kutoridhishwa na hali ya mazingira kiwandani hapo.
Akitoa tamko hilo ,Naibu waziri Lugola alisema kuwa kulingana na sheria za usimamizi na usafi wa mazingira ni sharti kiwanda hicho kitozwe faini ili iwe fundisho kwa viwanda vingine kufuata taratibu ikiwa ni pamoja na kufanya tathmini ya mazingira kabla ya kuanza shughuli za
uzalishaji.
Pamoja na mambo mengine Lugola alikiagiza kiwanda hicho kuelekeza taka ngumu kwenye dampo la jiji lililopo Chidaya -Ntyuka ili kuepuka madampo yasiyo rasmi yanayozagaa katikati ya jiji na kukuta mizoga ya nyama ikiwa imezagaa maeneo mbali mbali.
Awali akisoma taarifa kwa naibu waziri Lugola,Mtendaji Mkuu wa kiwanda hicho Aron Luziga alizungumzia changamoto zilizopo kiwandani hapo kuwa ni pamoja na mfumo wa maji taka usio rasmi kutokana na gharama kubwa ya ujenzi pamoja na upatikanaji wa umeme wa uhakika
hali inayokwamisha shughuli za uzalishaji .
Alisema,hali ya kukatika katika kwa umeme kiwandani hapo inakwamisha shughuli za uzalishaji hivyo kuiomba serikali kuangalia namna ya kuboresha miundombinu ya umeme ili kukidhi mahitaji .
“Lengo la kiwanda hiki ni kuwa kinara katika uzalishaji wa nyama na kusafirisha nchi nyingi zaidi duniani hii ikiwa ni pamoja na uchakataji wenye kiwango kuendana na soko La kimataifa,” alisema Luziga.
Wakati huo huo Naibu waziri Kangi Lugola ameliagiza Baraza la usimamizi wa mazingira la Taifa (NEMC) kushirikiana na uongozi wa jiji la Dodoma kukagua kwa undani mifumo ya maji taka ya kiwanda cha kukamua mafuta ya alizeti cha Sunshine kilichopo katika
kijiji cha Zuzu.
Hatua hiyo imekuja kutokana na kushindwa kuibaini mifumo ya majitaka kiwandani hapo kutokana na kuwa kiwanda kimesitisha uzalishaji kutokana uhaba wa malighafi kiwandani hapo.
Kutokana na hayo Naibu waziri Lugola ameutaka uongozi wa kiwanda hicho kuingia mkataba na wakulima ili waweze kupata malighafi ambazo zitawezesha kiwanda hicho kuwa na uzalishaji wakati wote.
“Ni kweli tunahitaji Tanzania ya viwanda,lakini viwanda hivyo vije kwa kuzingatia sheria za mazingira ili kuyahifadhi na kwa manufaa ya vizazi vijavyo,” alisema.
Hata hivyo alisema viwanda vinapaswa kuchochea wananchi kuondokana na umaskini hivyo ni wajibu kushirikiana na wananchi bega kwa bega kupata solo la uhakika.
|
Comments
Post a Comment