- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
NA MWANDISHI WETU
LUGHA ya Kiswahili inazungumzwa katika nchi za Afrika
mashariki. Kiswahili hutumika nchini Tanzania, Kenya, Uganda, Burundi, Jamhuri
ya Kidemokrasia ya Congo, Msumbiji na Rwanda.
Kiswahili ndiyo lugha ya taifa katika nchi nne za Afrika
Mashariki ambazo ni Tanzania, Kenya, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya
Congo.
Zaidi ya watu milioni 15 hutumia lugha hiyo kama lugha ya
kwanza huku wengine 150 kutoka nchi nyingine wakitumia Kiswahili kama lugha ya
pili au ya tatu. Ni lugha pekee ya Kiafrika ambayo ni rasmi ya Umoja wa Afrika
pamoja na Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Lugha ya Kicomoro inayozungumzwa katika Visiwa vya Comoro wakati mwingine hufananishwa na lafudhi ya
Kiswahili, ingawa wengine wanaoiona kama ni lugha isiyoshabihiana.
Kiswahili sanifu ya kisasa kimeegemea zaidi katika lafudhi
ya Kiunguja inayozungumza Unguja, lakini kuna lafudhi mbalimbali za Kiswahili,
baadhi ambazo zinawiana.
Lafudhi za zamani zinazorandanda na Kiswahili ni Kimwani (inazungumzwa
Visiwa vya Kerimba katika pwani ya kaskazini ya Msumbiji), Chimwiini kinazungumzwa
na baadhi ya wakazi wa mji wa Barawa katika pwani ya kusini ya Somalia, Kibajuni
kinazungumzwa na Wabajuni kwenye Visiwa vya Bajuni kwenye mpaka wa Kenya na
Somalia ambapo pia kinafahamika kama Kitikuu au Kigunya.
Lafudhi nyingine za Kiswahili ni kama cha Mombasa-Lamu
ambako kuna Kiamu, Kipate, Kingozi, Chijomvu, Kimvita, na Kingare.
Kiswahili ya Kimrima kinazungumzwa zaidi Pangani, Vanga, Dar
es Salaam, Rufiji na Kisiwa cha Mafia wakati Kiunguja kinazungumzwa zaidi
Unguja na Kitumbatu kinazungumzwa Kisiwani Pemba kama ilivyo kwa Kipemba.
Kwa ujumla, lugha ya Kiswahili imekuwa kinara wa lugha
nyingine za Kiafrika na inazungumzwa katika nchi hizi zifuatazo:
KENYA
Kiswahili nchini Kenya ni lugha rasmi na pia ni lugha ya
Taifa. Rais wa kwanza wa taifa la Kenya hayati Mzee Jomo Kenyatta alitoa kauli
kwamba Kiswahili kinafaa kutumika kama lugha rasmi ya Kenya mwaka 1969. Mwaka
1975 Kiswahili kilianza kutumika bungeni.
Serikali ya Kenya ilianzisha somo la Kiswahili katika Idara
ya Lugha za Kiafrika na Isimu ya Chuo Kikuu cha Nairobi.
Kuanzia miaka ya themanini mwishoni, takriban vyuo vikuu
vyote vilivyoanzishwa na Serikali vilifundisha masomo ya Kiswahili kwa lugha ya
Kiswahili.
TANZANIA
Kiswahili nchini Tanzania ni lugha rasmi na lugha ya Taifa.
Ni lugha ya utambulisho kwa Mtanzania na inatumika kama lugha ya kuimarisha
uelewano, ushirikiano na umoja wa kitaifa.
Katika kuiendeleza lugha hiyo, juhudi za usanifishaji
zimefanyika kwa kuwatumia wataalam wa fasihi na isimu, wadau wengine na
wachapishaji vitabu.
Vyombo mbalimbali vianzishwa kama Baraza la Kiswahili
Tanzania (Bakita), Baraza la Kiswahili Zanzibar (Bakiza), Taasisi ya Kiswahili
na Lugha za Kigeni (Takiluki), Taasisi ya Elimu, Umoja wa Waandishi wa Vitabu Tanzania
(Uwavita) na Usanifu wa Kiswahili na Ushairi Tanzania (Ukuta).
Pia vyuo vikuu mbalimbali vya Bara na Visiwani vilianza
kusomesha Kiswahili kuanzia shahada ya kwanza, ya uzamili na uzamivu.
RWANDA
Kiswahili ni lugha rasmi nchini Rwanda. Kabla ya mwaka 1994,
wakati wa mauaji ya kimbari lugha ya Kiswahili ilizungumzwa kwenye miji
tofauti.
Lugha ya Kiswahili ilisambaa baada ya Wanyarwanda kuwaruhusu
Wajerumani nchini mwao kama watawala karne ya 19.
Mwaka wa 1976 -1977 lugha ya Kiswahili ilianza kufundishwa
katika shule za upili (sekondari) na Chuo Kikuu Cha Rwanda.
UGANDA
Mwaka 1960, Serikali ya Uganda iliruhusu na kulazimisha
Kiswahili kitumike nchini humo; Kiingereza na lugha za kikabila zilikuwa tayari
zinatawala mawasiliano Uganda nzima.
Lugha ya maandishi ya Kiswahili yalianza kutumika katika
Baraza la Kifalme la Buganda na Bunyoro, hata kabla ya ukoloni (1862).
Kiswahili hutumika katika shughuli za biashara, dini na
mila.
Nchini Uganda Kiswahili kilifikiriwa kwamba ni lugha ya
watumwa. Lakini Kiswahili kilitumiwa zaidi na Polisi na Wanajeshi.
Katibu mtendaji wa Kamisheni ya Kiswahili ya Afrika
Mashariki, Keneth Cimara, aliipongeza serikali ya Uganda kwa juhudi ya
kuendeleza Kiswahili tofauti na ilivyokuwa miaka ya nyuma.
Mapema mwezi huu ilifanyika warsha ya siku mbili katika
hoteli ya Imperial Royal mjini Kamapla iliyowajumuisha walimu wa vyuo vikuu,
shule za upili na taasisi mbalimbali nchini Uganda.
Keneth Cimara amesema miaka ya themani raia wengi wa Uganda
walikiona Kiswahili kama lugha ya wahalifu ikitumiwa na askari kuwanyang'anya
mali zao, aidha kuwatendea uhalifu.
Cimara ameongeza kwamba, sasa Serikali ya Uganda ni miongoni
mwa mataifa ya Jumuia ya Afrika mashariki ambayo yameweka mikakati ya
kuendeleza matumizi ya lugha ya Kiswahili.
JAMHURI YA KIDEMOKRASIA YA CONGO
Kiswahili kiliingia nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
kuanzia karne ya 19.
Kiswahili kilianza kuenea kutoka Mashariki mwa nchi hiyo,
kuelekea kandokando ya Mto Congo.
Comments
Post a Comment