Featured Post

TAHADHARI KUELEKEA KIPINDI CHA MSIMU WA MVUA ZA MASIKA

Kamishna wa Usalama dhidi ya moto wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji (CF) Jesuald Ikonko. 

    
TAARIFA KWA UMMA
Kufuatia uwepo na muendelezo wa mvua kubwa, ambazo zitaambatana na upepo mkali katika maeneo mbalimbali hapa nchini kama ilivyolitolewa taarifa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA). Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Tanzania Bara, linawatahadharisha wananchi kuwa makini katika suala zima la Kuokoa Maisha na Mali zao.
Kutokana na mvua hizo Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linawataka wananchi wote wanaoishi kwenye mazingira hatarishi (Mabondeni) kuwa makini na kuchukua hatua mapema ya kuyahama maeneo hayo kabla mvua hizo zinazotabiriwa hazijaanza kuleta madhara makubwa.
Hata hivyo, Jeshi lipo timamu na tayari kwa kukabiliana na majanga yoyote yatakayotokana na mvua hizo. Tunawaomba wananchi wote kuwa wepesi katika kutoa taarifa pindi wanapoona viashiria vya mafuriko au mtu kuzingirwa na maji.
Aidha, tunawaomba wananchi kutumia namba ya simu ya dharura 114 (bure) kutoa taarifa za matukio ya Moto, Mafuriko, Ajali za barabarani, Tetemeko la ardhi na majanga mengine kwa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.

Imetolewa na;
Kitengo cha Habari na Elimu kwa Umma
Jeshi la Zimamoto na Uokoaji-Makao Makuu.


Comments