- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Na Innocent Nganyagwa
KAMA kawaida, leo tunakutana tena kwenye
safu yetu ya utopevu wa kijadi na kujivunia asili zetu.
Basi nawakaribisheni nyote, ambapo leo tunapata
fursa ya kusogea hadi kwa ndugu zetu Warangi, kabila linalopatikana kwenye eneo
lililopo kati ya Babati na Kondoa, lakini hasa wakiwa kwa wingi huko Kondoa.
Ndugu zetu hawa kwa sasa wengi wetu
tunawaita Warangi na wanaongea lugha yao ya Kirangi,
lakini kwa asili wao wenyewe wanajiita ‘Valangi’ kwa matamshi yao halisi na
lugha yao ni ‘Kilangi’ au ‘Kilaangi’.
Kutokana na historia yao na namna
walivyofika eneo walilopo, ndugu zetu hawa wanatangamana na makundi kadhaa ya
makabila mengine yakiwemo yale ya kizururaji, lakini wamefaulu kulinda
utambulisho wao na kubaki kama walivyo.
Baadhi ya majirani zao ambao kihistoria
wameshawahi kuwepo na wengine bado wapo mkabala nao kwenye eneo hilo ni
Wamasaai ambao ni Wanailotiki, Wasandawe ambao ni Wakhoisan, Wairaqw,
Waburunge, Wasi na Wagorowa makabila yanayotokea mbari ya Kikushi na Wambugwe
ambao ni Wabantu.
Lugha ya Warangi imeathiriwa na makabila
haya wanayotangamana nayo kwenye eneo moja, lakini ina ukaribu zaidi na
Kimbugwe kuliko lugha za yale makabila mengine.
Ndugu zetu hawa wametoka mbali kabla
hawajafika eneo walilopo, japokuwa unaweza kuwa umeshazisikia historia nyingine
zinazoeleza maeneo mengine tofauti waliyotokea.
Jamii za awali za mababu wa Warangi kwa
asili zinatokea kaskazini na mashariki mwa bara hili, walisafiri kutoka upande
huo na kupitia eneo la Bonde la Ufa hadi Kenya wakipita Ethiopia kwanza.
Walipofika hapa nchini walilowea Babati
kwanza, kabla ya kujisogeza kwenye maeneo mengine ya pembezoni.
Katika safari zao, ndugu zetu hawa walipita
maeneo mengi kwa misimu tofauti ya hali ya hewa ukiwemo wakati wa ukame.
Kutokana na maeneo waliyopitia nyakati za
kiangazi, walikuwa na kawaida ya kutafuta maji kwa mbinu mbalimbali.
Wakifanikiwa kupata maji katika eneo
husika, basi huamini mahali hapo panawafaa kuishi na huamua kulowea na
kuanzisha makazi yao.
Kwa kawaida walikuwa wakichimba mashimo
marefu na kutumbukiza vyombo ndani ya mashimo hayo, kisha waliendelea na safari
zao.
Wakirudi kwa mara ya pili katika eneo hilo
na kukuta vyombo hivyo walivyoviweka kwenye mashimo vimejaa maji, huamini
sehemu hiyo ina neema na wanaweza kuishi mahali hapo.
Katika historia ya misafara yao,
waligawanyika makundi mawili walipofika Babati. Kundi la vijana walikwenda
kuwinda ndege aina ya kanga pembezoni mwa maeneo waliyokuwepo ya Babati,
waliporudi hawakuwakuta wenzao waliowaacha na kuendelea na safari ya kutafuta
nchi mpya ya kuishi.
Kanga kwa Kirangi huitwa ‘mbuwe’, basi wale vijana walioachwa
mahali pale waliamua kuendelea kuishi pale na kuwa sehemu ya Wambugwe.
Hiyo ndiyo sababu inayofanya lugha zao ziwe
na namna fulani ya maingiliano ya karibu zaidi, kuliko lugha za yale makabila
mengine wanayotangamana nayo tuliyoyataja hapo awali.
Lile kundi lingine lililowaacha wale
wenzao, lilielekea kusini zaidi na kufika hadi eneo la Haubi. Sehemu hiyo
waliikuta ina kile walichokitafuta, maana maji yalipatikana kwa wingi na
hayakuwa yakikauka kwa misimu yote, basi wakalowea mahali hapo.
Ndiyo maana hata sasa kuna Warangi
wanaofahamu na kuamini kuwa kwa asili wao wanatokea hapo Haubi.
Ndugu zetu hawa ambao pia hulima mahindi na
mtama, kiini cha nchi yao ya Kirangi ni kusini magharibi huko Kondoa waliko kwa
wingi.
Nadhani bado unakumbuka kuwa tukisema nchi
ya jina la kabila fulani tunamaanisha nini.
Eneo hilo la kiini cha nchi yao lina vijito
vingi vidogo vidogo, lakini ambavyo kukiwa na kiangazi kikali na ukame hukauka
na kwa nyakati hizo hulazimika kuchimba ili kupata maji.
Tuseme ni kama walivyokuwa wakifanya
mwanzoni, walipokuwa wakizurura kutafuta maji tangu huko kaskazini walikotokea.
Katika eneo hilo la kiini cha nchi ya Kirangi
kuna vijiji kama vile Hurui, Mwaikisabe, Kibaya, Mangoroma, Mafai, Mesanga,
Mnenya (Mnenia), Loo na Iyoli.
Eneo lao hilo la kiini cha nchi ya Urangi
limezungukwa na milima na miinuko ya nchi na uwanda, hali inayosababisha
makundi yao mengi kupatikana kwenye maeneo sawia.
Hiyo inamaanisha kuwa, waliishi kwa makundi
kwenye maeneo hayo na hakukuwa na watu wengine waliotawanyikia kwenye maeneo ya
pembezoni mwa nchi yao, kutokana na jiografia halisi inayowazunguka ilivyo.
Hata yale makabila mengine yaliyo pembezoni
mwao, kama vile Wasandawe, hupatikana mbali kidogo kutoka kwenye kiini cha nchi
ya Urangi, baada ya kupita misitu.
Kwa hiyo, hawa Warangi wenyewe ni kabila
lenye jamii inayopenda kujiweka karibu kwa pamoja kwenye mambo yao.
Kwa hulka hizo basi, utaona kuwa ndugu zetu
hawa wanajivunia sana asili yao na hawagubikwi kirahisi na jamii nyingine na
kuacha mambo yao.
Mathalan, licha ya lugha yao kuwa na
muingiliano na Kimbugwe, lakini wanapokutana Mrangi na Mbugwe, Mrangi akiongea
Kirangi watasikilizana na Mbugwe.
Lakini wao Warangi hawapendi kusemeshwa
Kimbugwe, bali Kirangi. Kuna baadhi ya maneno kama vile jua ambalo kwa Kimbugwe ni ‘ijova’
kwa Kirangi ni ‘ijuva’ ikimaanisha
alama ya uwepo wa Mungu.
Japo kwa sasa kwa Kirangi jua linafahamika
zaidi kama ‘mwaasu’, lakini Mbugwe
akitaja ‘ijova’ Mrangi anamuelewa
kuwa anamaanisha ijuva, yaani jua.
Kujivunia na kuhifadhi lugha yao, ni moja
kati ya mambo yanayowafanya watambulike kuwa wapo.
Hata katika kuoana, mara nyingi wao
hupendelea zaidi ndoa za jamii yao wenyewe.
Na ikitokea wakaoa jamii za pembezoni mwao,
basi watu wa zile jamii ndiyo hutakiwa kufuata lugha na mambo yao na sio wao
kuwafuata wengine.
Lakini hiyo isikusababishe uwaelewe
tofauti, hapana, hawa ni watu waungwana na wapole tu wanaowiana vyema na jamii
nyingine, kwenye maeneo wanayoishi walikochanganyika na watu wa makabila
mengine.
Leo ndiyo kwanza tumewapigia hodi hawa
ndugu zetu Warangi, ambao wao na Wambugwe wana uwiano fulani kwenye lugha yao
kama tulivyoona.
Tutakavyoendelea kuchambua mambo yao kesho,
tutaona uwiano huo na mambo yao mengine.
Basi tukutane tena kesho kwenye safu yetu,
ili tuendelee kutathmini mambo ya ndugu zetu hawa.
Makala haya yamehaririwa,
yalichapishwa kwa mara ya kwanza katika gazeti la Tanzania Daima Machi 14, 2009.
Comments
Post a Comment