- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Kipeyo au Lukulu (Kinyisanzu) ni chombo cha kunywea vinywaji mbali mbali kwa kabila la Wanyisanzu.
Na Innocent Nganyagwa
KARIBUNI ndugu zangu, ni siku nyingine tena
tunakutana kupata fursa ya kutopea kwenye ujadi wetu.
Baada ya kuwatembelea ndugu zetu Wakimbu,
leo tunaendelea mbele na ziara zetu za kijadi, zinazotuwezesha kufahamu japo
kwa uchache, baadhi ya mambo mbalimbali ya makabila.
Ndugu zetu Wanyisanzu wanapatikana zaidi
mkoani Singida, Wilaya ya Iramba, Tarafa ya Kirumi, wakipakana na Wilaya ya
Maswa na Meatu kwa Mkoa wa Simiyu (zamani Shinyanga).
Pia kutokana na mahali walipo, wanapakana
na wilaya za Mbulu na Karatu. Kwa uchache, makabila majirani zao ni Wasukuma,
Wairaqw, Wamang’ati, Watindiga na Wasandawe, kwenye eneo hilo la katikati na
kaskazini magharibi mwa nchi yetu.
Wanyisanzu ambao wanatokea mbari ya
Kibantu, si wengi sana kwa idadi, kwa hiyo si moja ya makabila makubwa hapa
nchini.
Naamini kuna baadhi yenu Wajadi hamjawahi
kuwasikia, lakini wapo na wana mambo yao. Kimsingi wao ni wakulima, japo kwa
uchache hufuga pia wanyama kama mbuzi, kondoo na kadhalika.
Wao hulima ufuta, mtama na mahindi, yakiwa
ni baadhi ya mazao wanayoyategemea zaidi kwa chakula.
Maziwa na samaki wakavu ndivyo vitoweo vyao
vikuu, vinavyotumika kwa chakula hicho kitokanacho na mazao hayo.
Eneo wanalopatikana lina utata mkubwa wa
upatikanaji wa mvua, huku likikabiliwa na vipindi vya ukame wa hapa na pale.
Kutokana na hali hiyo, ndugu zetu hawa ni mahodari kwa matambiko na uganga wa
kutengeneza mvua, tangu siku nyingi zilizopita.
Kuzalisha mvua kwao ni kama uzao wa kiumbe mpya,
hivyo kwenye mbinu hizo za kusababisha mvua, jinsia huthaminiwa sana.
Kwao, uzao wa kitu chochote, si kwa
binadamu tu, hutegemea jinsia. Kwa hiyo tunaweza kusema kuwa, wanazingatia sana
ujinsia katika kutenda mambo yao.
Japokuwa kwenye ujinsia huo kama ilivyo kwa
makabila mengi, hakuna usawa, kama inavyofahamika upande mmoja huukiritimba
mwingine.
Utengenezaji mvua kwao hutekelezwa kwa
utoaji sadaka za kuchinja wanyama kama kondoo, ambao ni matoleo ya kafara kwa
mababu wanaotarajiwa kujibu kwa kuleta mvua.
Mambo hayo ya kuamini ujinsia kwao, huvuka
hata kwenye vitu vya kawaida sana, mathalan, uwashaji moto kwa kutumia vijiti.
Kile kisuguacho chenye kitundu ili kutoa mwako, huchukuliwa kuwa dume na
kisiguliwacho jike.
Uwashaji moto wa aina hiyo, kwa ajili ya
kuchoma nyama ya kafara ya mnyama wa sadaka ya kuomba mvua, huambatana na
utamkaji maneno ya kuomba mizimu ijibu maombi.
Nyumba ya asili ya Wanyisanzu
Kwa imani yao, ushirikiano wa jinsia ya
kiume (mtenda) na ya kike (mtendwa), pamoja na nguvu za mizimu, huleta
matarajio yanayotazamiwa.
Huo ni ushirikiano wa nguvu mbili za
kijinsia na moja ya kimizimu, inayoidhinisha kinachotakiwa kutokea kwa
ushirikiano wa zile jinsia mbili.
Japokuwa ni jinsia ya kiume ndiyo
inayoonekana kutaka ukiritimba, kwenye kabila hilo lililoelemea kwenye uzao wa
kikeni.
Misigano ya kutafuta nguvu baina ya jinsia
hizo mbili, hutokea kwenye mambo mengine si kwenye yale mambo ya kutengeneza
mvua, ambapo kila moja hukubali nafasi yake.
Kufanikiwa jambo lolote kwao, ni lazima
kutegemee jinsia mbili, hakuna linalowezekana kutendeka kinyume cha hivyo.
Pamoja na kabila hili kutofahamika na
wengi, lakini ni maarufu si kwa mambo hayo tu niliyoyaeleza, bali pia lina
ufanisi na utajiri mkubwa wa mambo ya uganga.
Kutoka katika kabila hili kuna waganga
wenye uwezo mkubwa wanaojitofautisha na ulaghai, si kama ilivyo kwa baadhi ya
waganga wanaozingatia maslahi yao na si kutimiza matarajio ya wenye shida.
Tayari tumeshawapigia hodi hawa ndugu zetu
Wanyisanzu. Tutaendelea kuchambua kwa kina zaidi mambo yao kesho.
Makala haya yamehaririwa,
yalichapishwa kwa mara ya kwanza katika gazeti la Tanzania Daima Januari 03, 2009.
Comments
Post a Comment