- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Na Innocent Nganyagwa
NI siku nyingine tena ninapokukaribisha
kwenye mambo yetu ya mila, utamaduni na desturi zetu Waafrika na Watanzania kwa
ujumla. Leo tunaingia kwenye sehemu ya pili ya ziara yetu kwa ndugu zetu
Wanyisanzu, ambao tulianza kuwatembelea jana.
Nikukumbushe kidogo japo kwa ufupi, baadhi
ya mambo tuliyoyaona kuhusu ndugu zetu hawa, kwenye sehemu hiyo ya kwanza. Kama
ulikosa sehemu hiyo, basi utaweza kwenda nasi sawa baada ya muhtasari huu, tutakapoendelea
kutokea pale tulipoishia. Hawa Wanyisanzu wako zaidi mkoani Singida, kule
Iramba, eneo la Kirumi linalopakana na Maswa, Meatu, Mbulu na Karatu.
Hapo walipo wanatangamana na Wasukuma,
Wairaqw, Wamang’ati, Watindiga na Wasandawe. Huo ni upande wa katikati kidogo,
kwa kuelekea kaskazini magharibi mwa nchi yetu.
Wanyisanzu ambao ni Wabantu, si miongoni
mwa makabila makubwa hapa nchini, kwa hiyo ndugu Mjadi kama hujalisikia kabila
hili, usishangae. Lakini wapo na wana mambo yao ya kuvutia kuyafahamu, wao ni
wakulima, mazao yao yanajumuisha ufuta, mtama na mahindi.
Lakini pia wanafuga, wanapendelea maziwa na
samaki wa kukaushwa kama mboga.
Mfumo wao wa kuishi na kujitosheleza kwa
chakula, ni kutokana na eneo walilopo, ambalo lina hali isiyotabirika kwa
vipindi vya mvua na ukame.
Mazingira ya hali ya hewa ya eneo lao,
yamewapelekea wawe mafundi wa kutengeneza mvua. Hufanya hivyo kwa kutumia
waganga na matambiko ya kuomba mvua, wakitekeleza hayo kwa kutegemea mizania ya
kijinsia.
Wao wanaamini kuwa, hakuna chochote
kinachoweza kuzaliwa bila jinsia, kwa hiyo, kwao, chochote kinachozalishwa
lazima kitokane na jinsia mbili – ya kike na kiume.
Imani hiyo si kwa viumbe hai tu, hata kwa
mambo yanayotengenezwa na binadamu.
Licha ya kuzingatia jinsia, lakini kuna
mivutano, ambapo kama kawaida jinsia dume hutaka kuikiritimba ya kike.
Kwenye mambo ya utengenezaji mvua kwa
matambiko, huchinja wanyama hususan kondoo na kutoa kafara kwa mababu, ambao
hujibu kwa kuleta mvua.
Matambiko, huambatana na maneno ya ibada za
kijadi, lakini ili utekelezaji huo ufanikiwe, lazima kuwe na nguvu ya utatu.
Najua unaweza kustuka, maana utatu unaweza
kuwa umeusikia kwenye imani fulani za kigeni, lakini hata wao wana nguvu ya
utatu.
Kwamba, jinsia mbili na mizimu huleta
matokeo tarajiwa, hasa katika kutengeneza mvua.
Lakini, licha ya hizo jinsia kuvutana
kwenye mambo mengine, zinaheshimiana kwenye matambiko, hasa yale ya kutengeneza
mvua na kila moja hukubali nafasi yake.
Uhodari wao mwingine ni kwenye mambo ya
uganga, ni kabila lenye waganga wenye uwezo mkubwa usio wa kibabaishaji. Kwa
kifupi hayo ndiyo tuliyoyaona jana.
Sasa basi tuendelee mbele kutokea hapo. Ni
kwamba, licha ya wale majirani niliokutajia awali wa Wanyisanzu, lakini pia
zamani, Wahdazabe walikuwa majirani zao wa karibu.
Hao Wahadzabe hawakuoleana na makabila
mengine, isipokuwa hawa Wanyisanzu, ambao walifika kwenye eneo hilo tangu
mwanzoni mwa karne ya 18, katika kule kujitanua kwa Wabantu kwenye ukanda wa
kusini mwa Afrika.
Wanyisanzu ndiyo wanaowafahamu vyema Wahadzabe,
kuliko makabila mengine, hata watalii na wavumbuzi wengi wa mambo ya miji ya
kale waliwatumia wao ili kusikilizana na hao Wahdazabe.
Kutokana na jambo hilo, kuna Wahadzabe
wenye mchanganyiko wa damu na Wanyisanzu, japo kwa asilimia ndogo tu ya idadi.
Ufundi wa uganga na utengenezaji wa pombe,
waliutoa kwa Wanyisanzu, ambao walionekana kuwa na maarifa mengi yaliyoyavutia
makabila mengine.
Kwa ujumla wao Wanyisanzu, waliambukiza
utamaduni wao kwa makabila mengine yaliyowazunguka, japo eneo lao lilionekana
dogo, hasa kutokana na kutangamana na makabila mengi ya jirani nao.
Mathalan, hata yale mapambo ya kutoga
masikio yanayopatikana kwa Wahdazabe, wameyatoa kwa Wanyisanzu.
Hata ufundi wa mambo ya uganga, waliutoa
kwao, kama tulivyoona pale awali kuwa wao ni mahodari katika fani hiyo.
Lakini lazima ufahamu kwamba, wakati huo
hawa Wanyisanzu ambao ni Wabantu, walipoingia na kujitanua kwenye eneo hilo,
ndipo madini ya chuma yalipoanza kutumika kutengenezea silaha.
Kwa hiyo, licha ya sasa Wabantu kuonekana
ni wapole kulinganisha na watu wa mbari nyingine, lakini ni wao ambao awali
walikuwa wapiganaji hodari kutokana na zana hizo mpya, kwa wakati huo.
Hizo ni zama za kati ya zile za mawe na
chuma, ambapo kwa walioweza kutumia zana za chuma walikuwa na nguvu kubwa ya
kushinda kivita.
Kwa hiyo haishangazi kwamba, wao walikuwa
katikati ya makabila mengi, huku wakiwa kabila dogo, lakini hawakuweza
kugubikwa.
Kwa hiyo, ushawishi ni moja kati ya mambo
ambayo yaliwezesha makabila ya mbari nyingine. Kuyaiga yale ya mbari zenye
nguvu kama ambavyo tohara ilivyoigwa na baadhi ya makabila jirani na
Wanyisanzu.
Wabantu wengi kwa asili hutahiri, tofauti
na jamii za mbari nyingine.
Katika eneo lao wanalopatikana huko Kirumi,
kuna michoro, japo wenyewe wanadai kutohusika nayo, lakini kwenye mapango ya
mawe inakopatikana michoro hiyo, ndipo ilikuwa sehemu ya kujificha ya shujaa wa
Kirumi ambaye anasemekana alikuwa Mnyisanzu. Huyo aliitwa Nyakidarama, mmoja
kati ya watu maarufu kwenye historia ya kabila hilo.
Lakini, kwa kuwa kwenye eneo lao kuna
makabila mengine pia yaliyojihusisha na michoro ya mapangoni, si ajabu kuwa
hata miongoni mwao kuna ambao wanasema kuwa michoro hiyo haihusiani na kabila
lao. Wanyiramba pia, ambao ni majirani zao, nao wanafahamika sana pia kwa michoro
hiyo.
Pia kuzungukana kwenye eneo moja kwa
makabila yanayotokea mbari tofauti, ndiko ambako mara nyingi husababisha
taswira tata kama ambavyo tutaona kwa Wakamba.
Wabantu kwa asili, lakini wana taswira za
makabila ya Kihamitiki. Wanyisanzu wana makundi ya koo zipatazo takriban 12,
ambazo koo hizo zote huzijichukulia kuwa ndugu.
Koo hizo huzalisha koo nyingine thelathini,
hawa wote huunganishwa kwa kizazi cha kikeni, japo wana muelemeo wa kiumeni.
Nadhani naeleweka, tuliwahi kuona makabila
yenye mfumo huo, pia kuna ile hali ya kutambuana kindugu kwa tofauti ya mbinu
za utambulisho, ambao niliwahi kuzigusia hapa kwenye safu yetu.
Tuone baadhi ya hizo koo zao na koo tanzu
zitokanazo na hizo, kuna Anyampanda wa Kirumi (Anyanzoka – au Wanyanzoka),
Anyampanda wa Kinyakambi (Iyindi, Muhai au Mpilimaigulu), Anyampanda wa Anega,
Anyampanda wa lgomano, Anyampanda wa Ikela, Anyampanda wa Itiili, Anyampanda wa
Ikunguli, Anyampanda wa Matongo, Anyampanda wa Kinyingogo, Anyampanda wa
Nyonyela, Anyampanda wa Magemelo, Anyambilu wa Gudali, Anyambilu wa Kinyankunde
na Anyambilu wa Azigo.
Nyingine ni Anyambilu wa Mumba, Anyambilu
wa Anyankuni, Anyankali wa Ilumba (au Iyaniko), Anyankali wa Ipilinga,
Anyansuli wa Kingwele (au Mukoolo), Anyansuli wa Mukilampili (Itimbwa au
Ng’wamalaga), Anyambeu, Anyambeu, Anyang’walu, Anyambwa, Anyisungu, Anyambala,
Asamba, Anyakumi na Anyikili.
Nchi ya Ihanzu, yaani mahali wanakopatikana
ndugu zetu hawa, kuna misimu miwili tu, ‘kitika’
wakati wa mvua na ‘kipasu’ wakati wa
ukame. Misimu hii miwili imejigawanya katika takriban nusu mwaka kila mmoja,
mvua ziko kati ya Novemba na Aprili hadi Mei.
Kipindi kinachofuata kati ya Juni na Oktoba
ni ukame, hakuna mvua, mabadilishano ya vipindi vya ukame na mvua, ndiyo
yanayosababisha kilimo kuwa kigumu kwenye eneo hilo. Mara nyingine mvua huweza
kuja kwa wingi usiotarajiwa, na kuziondoa mbegu zilizopandwa.
Haiwezekani kulima bustani wala kilimo cha
sehemu nyevu, maana kwa asili hakuna mito inayotiririka kwa mwaka mzima. Lakini
wao kwa mbinu zao, wameweza kudumu na kuishi kwenye eneo lao la asili lenye
hali kama hiyo niliyoitaja.
Kesho tutaona kwa uchache, baadhi ya mambo
yao yaliyobakia.
Makala haya yamehaririwa,
yalichapishwa kwa mara ya kwanza katika gazeti la Tanzania Daima Januari 10, 2009.
Comments
Post a Comment