- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Nyumba za asili za Wanyiramba.
Na Innocent Nganyagwa
NDUGU zangu, leo tunawaangalia ndugu zetu Waniramba
au maarufu kama Wanyiramba. Ndugu zetu hawa wanapatikana mkoani Singida, hasa
huko Iramba, ambako wako kwa wingi. Wanyiramba ni Wabantu ambao kwa asili
wanatokea pembezoni mwa himaya ya Bahima, magharibi mwa Ziwa Victoria kwenye
mpaka wa Rwanda na Uganda.
Kutoka huko, jamii zao za awali ziliingia
mkoani Mara miaka 200 iliyopita na kuacha urithi wa majina yao, yanayofanana na
yale yaliyoko kwenye makazi yao ya sasa.
Wanyiramba walifika Iramba kutokana na
kukimbia vita huko walikotokea, walishapigana na Wakurya na kuwa watani
baadaye.
Katika msafara wao wakagawanyika makundi
mawili, kundi moja likaelekea kaskazini mashariki, kundi lingine likaenda
kusini magharibi.
Kundi la pili lililoelekea kwenye Bonde la
Mto Sibiti liligawanyika tena katika makundi madogo mawili, wengine wakaenda
kusini mwa Ziwa Kitangiri na wengine wakaenda Karatu.
Wale walioenda kaskazini mashariki,
walisogea hadi kwenye uwanda wa milima ya Usambara na Upare. Wakalazimika
kugeuza mwelekeo na kwenda kusini magharibi, kupitia eneo la katikati la
Kondoa.
Wakaenda hadi pembezoni mwa mpaka na Mkoa
wa Iringa, lakini wakalazimika kubadili tena mwelekeo na kwenda kaskazini.
Kilichowafanya wageuze kwa mara nyingine ni
kukumbana na wababe wengine wa kivita, Wahehe.
Walikuwa radhi kuzurura ili kutafuta amani,
kuliko kupigana na jamii za kibabe.
Kutoka hapo waliingilia kusini na kupitia
kwenye eneo la Ukimbu, wakaishi kwa muda maeneo ya Ushora na Usure huko Ukimbu.
Kisha wakaelekea kaskazini zaidi,
walikokutana tena na wenzao walioachana nao awali pale Kitangiri.
Lakini pia historia yao nyingine inasema,
walitokea mashariki huko Usambara mpakani na Upare wakaelekea kusini na kuishi kwa
muda maeneo ya Mkoa wa Morogoro.
Wana kumbukumbu ya makazi hayo kwenye
nyimbo zao, kwa kuimba majina kama ‘Munangulu’
lililotokana na kukaa kwa muda huko Uluguruni.
Wakaingilia Ugogoni na kujaribu kwenda tena
kusini, iliposhindikana wakaenda kusini magharibi.
Wakapitia Itigi na kukaa Tyumba huko
Ukimbu, kutoka hapo wakageuza na kwenda kaskazini zaidi kupitia misitu ya
Tyumba na kwenda kuishi kwenye Msitu wa Kungu.
Safari zao hazikuishia hapo, walielekea
kaskazini zaidi na kulowea huko Mwalu, kusini mwa Ushora, kisha baadaye
wakaenda Mangula.
Muda wote huo walipokuwa wakizurura,
hawakuwa na machifu bali viongozi wa muda waliotokana na matukio.
Hadi walipofika uwanda wa Iramba, walikuwa
wamegawanyika katika makundi ya koo mbalimbali.
Kila kundi la ukoo likalowea mahali
lilipoona panafaa, japokuwa makundi mengine kutokana na kuwa madogo mno, hayana
kumbukumbu zinazoonesha mahali yalikofikia awali.
Mengi ya makundi hayo yalilowea eneo la
Kisilili, yalipo makazi ya Chifu na mpakani na vilima vya Kinakumi, kaskazini
mwa Kiomboi na vilima vya Sekenke.
Baadhi ya koo hizo za Wanyiramba
zilizolowea maeneo hayo ni Wanambwa
(mbwa) waliolowea Nsimba huko Kisilili, na Wanisungu
(upepo) waliolowea Pazu.
Koo nyingine ni Wanankali (jua na chui) waliolowea Kulu, ambayo maana yake ni
Ufalme, Wanakumi (nge), waliolowea
kwenye miamba ya Nsamile, Wanampanda
(kondoo), walilowea ‘Nzuki’ ambayo
kwa Kiswahili ni nyuki, kutokana na eneo hilo kuwa na wadudu hao kwa wingi.
Koo nyingine ni Wanambala (kuku), waliolowea Mukiloga kusini mwa Kisilili. Pia kuna
Wanishanga (kuku), waliolowea eneo
lililopewa jina la kiongozi wao hapo Kisilili.
Koo nyingine zilizosalia ni Wanangili (nungu) waliolowea Kimaguwe,
eneo la kati ya Kiomboi na Ruruma, Wanalilya
(kilio) waliolowea Mangola karibu na miamba ya Nkuu.
Kuna makundi mengine yaliyolowea hapo
Iramba lakini hayakuja kwa ile misafara ya kuzurura.
Hao ni Wanakili
(simba) waliotoka magharibi na kulowea Mwagala, Wanambala nao pia walitokea magharibi, kama Wammbeu (mbegu) ambao nao walitoka magharibi.
Hao Wammbeu
ndiyo ambao wanashikilia Uchifu wa sasa wa Wanyiramba. Kundi la mwisho ambalo
ni dogo kabisa ni Wazigo (Zigua),
waliotokea magharibi mwa eneo la Wazigua.
Ndugu zangu, tutambue kuwa majina yaliyo
kwenye mabano ni alama za majina yanayotumika kutambulisha koo hizo.
Kama ambavyo tulivyoona hapo mwanzoni,
ndugu zetu hawa hapo awali hawakuwa na machifu. Lakini baadaye walikuwa na
mfumo huo wa uongozi, baadhi ya machifu muhimu wa kabila hilo wanaokumbukwa ni
Makala, Shango, Mizuzu, Kitandu, Nganguli, Leme, Mulumba na dada zake Nsili na
Shamba.
Wengine ambao hawakuwa na nguvu sana ni
Gelema, Magili, Kimalangombe, Nzoe, Shila na Kingu Kingu. Huyu wa mwisho
alipokewa utawala na Mazila, ambaye naye baadaye alipokewa na mwanaye Lutheri
baada ya kufariki.
Kama nilivyowafahamisha mambo ya ndugu zetu
hawa yanataka kuyafukua kweli kweli, maana yamejificha.
Kutokana na hali hiyo, hata simulizi za
machifu wao ni adimu kiasi kupatikana, ila wapo wawili ambao kuna kumbukumbu
nzuri ya simulizi zao.
Hao ni mtu na mwanaye, Mizuzu na Kitandu,
ambapo Mizuzu alikuwa akipata dawa za kijadi kutoka kwa mmoja wa machifu wa
Unyamwezini wa wakati huo.
Huyo chifu wa Kinyamwezi aliitwa
Limampindi, yaani mtu alimaye jioni. Yule Mizuzu kila mwaka alikwenda kwa
Limampindi, kujifunza ufundi wa dawa za kutengeneza mvua na za kulinda watu
wake.
Kila mara katika safari hizo alikuwa
akiambatana na mwanaye Kitandu, na walipofika huko, wakati Mizuzu akipata
mafunzo Kitandu alikwenda kwa mtoto wa Limampindi kumsaidia kuchunga.
Lakini yule Mizuzu akaona kama ametosheka
na mafunzo, hivyo basi muda mwingi aliutumia kunywa pombe na mwenyeji wake.
Lakini yule mtoto wa Limampindi ambaye
alikuwa rafiki wa Kitandu, yaani mtoto wa Mizuzu, alizifahamu vyema dawa za
baba yake na alimfundisha Kitandu walipokuwa wanachunga.
Kitandu akaondokea kuzijua vyema sana dawa
zile kuliko baba yake. Kuna siku Mizuzu na Kitandu walipokuwa wanarudi kutoka
huko Unyamwezini, mvua kubwa sana ilinyesha.
Kuna mto waliopaswa kuuvuka ambao ulijaa
sana kutokana na mvua hiyo, Kitandu alipotaka kujua kutoka kwa babake
watavukaje hakuwa na jibu.
Mizuzu alisema kuwa watasubiri mpaka kina
cha maji kipungue. Kitandu alipingana na jambo lile, akabainisha kuwa
watachelewa.
Akachukua mkuki wake na kuchoma kwenye yale
maji, yakagawanyika pande mbili na kuacha njia, wakavuka.
Najua ndugu yangu unaweza kushangaa, maana
mambo haya ya kugawanya maji na kupita katikati yake, wengi wenu mmeyasikia
kwenye maandiko ya imani za kigeni.
Lakini nataka nikuhakikishie kuwa, mambo
kama haya yalikuwepo hata kwenye jadi zetu, mengine bado yapo hata sasa
unaposoma simulizi hii ya Wanyiramba.
Binafsi kutokana na kupenda kuwa mdadisi,
mara kadhaa nikitajiwa eneo lenye maajabu ya aina hiyo, basi huwa najitahidi
kufika ili nishuhudie mwenyewe.
Kule kwetu Iringa nimeshawahi kwenda
kutembelea maeneo mawili matatu, ambayo bado yana mambo hayo ya maajabu ya
kijadi hata sasa.
Basi kama Kitandu kugawanya mto ni maajabu
kwako, soma haya mengine yanayofuata.
Ni mambo tu ya nguvu za kijadi, kama tutavyoona
tutakapowatembelea Wazigua na Wasambaa.
Yule Kitandu na babake walipovuka mto
walikabiliwa na msitu, na kwa mbali mbele yao kulikuwa na Wamaasai
wanawaelekea.
Kama ilivyokuwa mwanzoni, Mizuzu hakuwa na
ufumbuzi, Kitandu akaonesha ubingwa wake wa dawa za kijadi.
Alichukua udongo na kuufinyanga katika umbo
la pembe ya ndovu, akapuliza pembe ile ya bandia.
Baada ya kufanya hivyo walichokiona mbele
yao si Wamaasai tena, bali msafara wa wanyama wa msituni waliopita kwenda
mwelekeo mwingine siyo ule waliokuwa wao, yaani walipishana nao.
Tangu hapo Mizuzu hakupendezewa na uwezo
huo wa mwanaye, maana ulikuwa ni tishio kwa Uchifu wake.
Lakini hakukumbuka kuwa, wakati yeye
anaendekeza pombe, Kitandu alitumia muda wake vyema kujifunza dawa kwa mtoto wa
Limampindi.
Alianza kumfanyia hila mwanaye huyo, kwanza
alimlaani ili apotelee msituni, ikashindikana.
Akajaribu kumlaani ili apotee wakati wa
usiku, ikashindikana pia, alipoona mambo hayamwendei vyema akajaribu hila
nyingine.
Siku moja akaamua kumtumia nyoka amgonge na
kumuua, lakini Kitandu naye alimtuma mwanaye aliyeitwa Makala akaleta aina ya
nzige wanaoitwa ‘malimbo’ hawa
walimuuma yule nyoka aliyeitwa ‘nkungishaka’
mpaka akakimbia.
Mvutano huo haukumalizika vyema, kwani
Kitundu alimvunja mguu babake huko msituni, kisha baadaye akamkata kichwa.
Halafu akajenga kibanda kidogo na kukiweka kichwa hicho, ambacho kiliitwa ‘turnbika’ ambapo chumba kilichowekwa
kichwa hicho kiliitwa ‘kikungu’.
Sehemu hiyo ya kibanda ikawa ndiyo ya
kuabudia, hata mwaka wao mpya uliotegemea hesabu za mzunguko wa mbalamwezi,
ulihesabiwa kuanzia wakati ambao kibanda hicho kilijengwa.
Kwa wakati huo, koo iliyotawala ilitoa
kiapo cha kutooana na Wanangili kutokana na matukio hayo ya Kitandu na babake
Mizuzu.
Tukiachana na simulizi hiyo ndogo ya Kitandu
na babake, ni kwamba kusongamana kwa Wanyiramba kutokana na kuzaliana
kuliwafanya baadhi yao wajisogeze Kiomboi, Kinisungu, Ulemo na Kinampanda.
Katika maeneo hayo kuna sehemu ndogo ndogo
zinazofahamika kwa wakazi wenyewe tu waliolowea hapo.
Mathalan, Wanisungu waliishi kwenye maeneo
yaliyo ndani ya Kisungu, hawa walikuwa wanapenda sana kupigana dhidi ya koo
nyingine.
Najua utashangaa, kwamba watu waliozunguka
mwendo mrefu kukimbia vita wakaishia kupigana wenyewe kwa wenyewe.
Labda ni kwa kuwa walifahamiana vyema nguvu
zao, kulinganisha na wale wababe wa makabila mengine. Baadaye walikwenda kuishi
Ng’iti wakitokea Mpanzu.
Wanambala waliishi katika eneo dogo la
Monele huko Uwanza. Hawa walipigwa na wale Wanisungu ikabidi wakimbilie
Mukinga.
Wanisungu kwa muda huo walimtegemea sana
nabii wao Kwanwaga, basi Wanishanga nao walipokuja kusini mwa Uwanza kutoka
Kisilili, Wanisungu waliwapiga na kuwafukuza. Wakakimbilia upande wa mashariki,
eneo lililokuwa mbuga na kulowea nchi ya aliyekuwa Chifu Mtali.
Waliofuata kuonja kipigo cha Wanisungu ni
Wanangili, ikabidi wakimbilie tena nchi ya Wakimbu na kuishi Usule. Lakini ukoo
uliokataa kupigwa kirahisi ni Wanankali, hawa walipigana mno na Wanisungu.
Wakati huo Wanisungu walikuwa wanaongozwa
na jemedari wa vita aliyeitwa Shuluwa, mapambano hayo yalivuma kwa miaka mingi.
Damu nyingi sana ilimwagika kutokana na
mapigano hayo, sehemu ambayo mapambano yalikuwa makali ni Ruruma.
Eneo hilo lilikuwa na mto mdogo uliojaa
damu kutokana na mapigano hayo, koo hizo za Wanankali na Wanisungu ziliendelea
kupigana mpaka Wajerumani walipokuja kutawala.
Waniramba, ambao kiini cha makazi yao ni
kwenye maeneo ya Iramba inayojumuisha maeneo ya Kisinungu, Ulemo, Kinambwa,
Kisilili, Kinikili au Kiomboi, ambako Kinyiramba halisi kinazungumzwa.
Tofauti ndogo ndogo za matamshi ya lugha
hiyo kwa Wanyiramba wa Iambi, Isanzu na Ushora, zinatokana na kutangamana na
kuingiliana na makabila mengine.
Ndugu zangu, kuna mengi bado tunayoweza
kuyachambua kuhusu ndugu zetu hawa, lakini la mwisho kwa sasa ni kumbukumbu ya
yule Chifu Kitandu.
Kwenye Kijiji cha Kisana kaskazini mwa
Ruruma, wilayani Iramba, kuna kaburi lake karibu na shule ya Msingi ya Kisana
huko Kinakumi.
Kaburi hilo limezungukwa na miti
iliyopandwa pembezoni mwake, ili kuliwekea alama kwa ukumbusho wa Wanyiramba
wote.
Pamoja na Wanyiramba wengi kupatikana huko
Iramba, lakini wapo ambao kuna nyakati walikwenda Usukumani kufanya kazi za
kuvuna pamba.
Wengine wamelowea Arusha wakijihusisha na
shughuli za uvunaji miwa, huko wanapatikana kwa wingi Arusha Chini pembezoni
mwa mto Usa.
Ndugu zangu, kwa leo tukomee hapa, tukutane
tena kesho tutakapolitembelea kabila lingine kati ya makabila yetu hapa nchini.
Makala haya yamehaririwa,
yalichapishwa kwa mara ya kwanza katika gazeti la Tanzania Daima Februari 07, 2009.
Comments
Post a Comment