- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Akinamama wa Kinyakyusa wakiwa wamevaa nguo za asili.
Na Innocent Nganyagwa
NDUGU zangu, leo nawakaribisheni kwenye
safu yetu hii ambapo tunawatembelea Wanyakyusa wanaopatikana kwenye nchi yenye
neema ya vyakula mbalimbali kama maparachichi, ndizi na matunda mengine matamu.
Wanyakyusa wanapatikana kwenye eneo pana
sana.
Ndugu zetu hawa ambao kwa majina mengine huitwa pia Wasokile, Wangonde au
Wankonde, jamii zao zinapatikana kuanzia maeneo ya kaskazini mwa nchi jirani ya
Malawi hadi kusini mwa nchi yetu huko Mbeya.
Ndugu zetu hawa ambao huzungumza lugha yao
ya Kinyakyusa ambayo ni sehemu ya
lugha za Kibantu, eneo la nchi yao ndilo linalowapa majina tofauti na
tulivyozoea kuwaita.
Tumezoea kuwaita Wanyakyusa, lakini
kutokana na nchi yao yenye milima na mabonde inayoanzia Malawi na kupitia Ziwa
Nyasa kuwagawanya kwenye pande mbili, hiyo ilisababisha wawe na majina kadhaa.
Wale wanaoishi kuanzia mto wa Rukuru
kaskazini, Karonga, huko Malawi, hufahamika kama Wangonde au Wankonde.
Lakini watu hao hao wa jamii hiyo hiyo moja
walio upande wa pili wa nchi ya Unyakyusa, yaani maeneo ya Mbeya, hasa katika
wilaya za Rungwe na Kyela, ndiyo hufahamika zaidi kama Wanyakyusa.
Lugha ya ndugu zetu hawa ni Kibantu, japo
ina miundo tofauti ndani yake, yaani haina ule mfumo wa moja kwa moja kwa lugha
hiyo hiyo moja.
Lugha yao inatofautiana kimatamshi na hata
silabi zake, na lugha nyingine za Kibantu za jamii wanazopakana nazo.
Ukikuta Wanyakyusa wanaoongea lugha yao
kama inavyopaswa, utadhani kama aina fulani ya wimbo au shairi kwa jinsi matamshi
yao yanavyotoka.
Japo kwa sasa kuna Wanyakyusa wengi ambao
huongea lugha yao kwa kunyoosha matamshi ya silabi, kana kwamba wanaongea
Kiswahili.
Maingiliano ya jamii na lugha huathiri
lugha nyingi za kijadi na kuzibadili.
Japo si wengi wenu mnaofahamu hivyo, maana
hata salamu na baadhi ya majina hubadilika na yakishatumika kwa muda mrefu
hukubalika kwa mazoea na kuonekana ya kawaida.
Tukirudi kwenye jamii za Wanyakyusa, hapo
zamani wakati wakiwa huko ‘Nyasaland’ kwenye eneo la kandoni mwa Mto Songwe,
walifahamika zaidi kama Wangonde.
Lakini upande wa pili wa mto huo
walishaanza kuitwa Wanyakyusa, ila utamaduni na lugha zao zilikuwa zinalandana
kwa kiasi kikubwa, hali iliyowachanganya hata wageni (wakoloni) waliokuwa
wanatawala pande hizo mbili.
Huu upande wa pili ulikuwa chini ya
Wajerumani, walioamua kupaita Konde kutokana na kule kufanana kwa watu wa
upande huo na ule wa kwanza, uliokuwa chini ya Waingereza.
Lakini kitu kimoja kitakachokushangaza
kuhusu ndugu zetu hawa, ni kwamba ukirudi nyuma zaidi kwenye chanzo chao
utagundua kuwa wanatokana na Malkia mwenye asili ya Kinubi, aliyeitwa Nyanseba.
Malkia huyu alipinduliwa na mpiganaji mmoja
na kundi lake la wafugaji wazururaji, kisha wakahamisha utawala kutoka kikeni
kwenda kiumeni kwa maana ya Wafalme badala ya Malkia.
Lakini hiyo haikusaidia kufuta nguvu na
uwakilishi wa kikeni, ndani ya jamii za baadaye zilizozalisha kabila la
Wanyakyusa.
Mfumo wao wa utoaji majina ya watoto katika
ujadi wao wa zamani, ni kwamba mtoto wa kiume huchukua jina la ukoo wa mama na
wa kike la ukoo wa baba, hiyo ilifanyika ili kuendelea kulinda ile hadhi ya
kikeni kwa vizazi vya baadaye.
Pia kuna mambo mengine kuhusiana na majina
ya Wanyakyusa, ngoja nikutaarifu kitu kinachoweza kukuchekesha kidogo.
Kama ni mgeni kwenye nchi yao ya Unyakyusa,
unaweza kustaajabishwa na utopevu na ufuasi mkubwa wa imani za kidini.
Hata ukipanda mabasi yanayoelekea mkoani
Mbeya, basi burudani ya nyimbo itakayotawala ndani ya vyombo hivyo vya usafiri
iwe kwa sauti au taswira, ni nyimbo za kidini.
Endapo mhudumu wa basi atajaribu kuweka
aina nyingine ya burudani, basi huenda akakumbwa na malalamiko ya abiria
wanaosafiri.
Lakini kama ukifikiri kuwa utopevu huo wa
imani umeanza siku za karibuni, utakuwa umekosea sana.
Ukitaka kuthibitisha utopevu wao wa
kiimani, basi tazama maana ya majina mengi kati ya yale wanayopewa watoto wa
Kinyakyusa.
Ngoja nikutajie baadhi ya majina hayo na
maana zake kwenye mabano, Ambidwile (Mungu ameshawishi), Ambilikile (Mungu
ameniita), Ambokile (Mungu ameniokoa), Ambonisye (Mungu ameniponya), Andalwisye
(Mungu ameniongoza), Andondile (Mungu amenihitaji) na Andongwisye (Mungu
ameniongoza).
Mengine ni Andwele (Mungu amenileta),
Tuponile (Tumeokolewa) na Tusajigwe (Tumebarikiwa).
Majina yote hayo ni ya kiume isipokuwa kwa
hili la mwisho, ambalo mara nyingi kwa ufupisho huitwa Tusa. Wasichana wengi wa
Kinyakyusa wenye jina hilo huitwa hivyo.
Tukirudi kwenye zile jamii zao za awali
zilizogawanywa na mito na majina, wale walioitwa Wangonde waliokuwa kusini
walitangulia kimaendeleo.
Hawa waliokuwa upande wa pili waliojulikana
zaidi kama Wanyakyusa, kwanza waliishi kwenye vijiji vidogo vidogo huku wakiwa
na tawala nyingi ndogo ndogo za Kichifu, zilizotawanyika kwenye eneo lao.
Lakini licha ya kuwa na tawala nyingi ndogo
ndogo, waliweza kuwashinda maadui waliowashambulia kwa nia ya kuwatawala,
maadui hao walitoka kwenye makabila ya Wasangu na Wangoni.
Katika eneo la nchi yao lenye uwanda wa
milima, Wanyakyusa waliwahi kuwa na muingiliano wa kijamii na Wakinga
waliosambaa upande wa magharibi wa nchi yao wakiwa wahamiaji.
Magharibi mwa nchi ya Ukinga, ndipo nchi ya
Unyakyusa ilipopakana nao.
Mchanganyiko wa jamii hizo mbili ndiyo
uliozalisha baadhi ya kanuni na mila, zilizowahusu machifu wa awali wa
Kinyaksyusa hasa kwa zile himaya nyingi ndogo ndogo nilizozitaja hapo awali.
Watawala hao waliishi katika hali ya
kujitenga, walikuwa na nguvu za kimiujiza lakini pia walidhibitiwa upeo wa
mamlaka yao na mabaraza ya utawala.
Kama mtawala akizeeka sana au akiumwa mno,
ili kuepusha himaya anayotawala isikumbwe na mkosi utakaosababisha kukosekana
kwa mvua na mavuno bora, basi aliuawa kwa kunyongwa na hao wajumbe wa baraza
lake.
Nitakuja kuwaeleza mauaji kama hayo ya
Machifu wakati nitakapowasimulia mambo ya ndugu zetu Wanyamwezi na mfumo wao wa
utawala.
Mfumo huo unalandana sana na mfumo huu na
hii haishangazi, maana Wanyamwezi nao ni Wabantu kama hawa Wanyakyusa
tunaowazungumzia leo.
Kama ambavyo huwa tunaainisha mara nyingi
kwenye safu yetu, kwamba makabila au jamii zitokanazo na mbari moja hulandana
kwa mambo mengi.
Basi tukiendelea na mambo ya wale Machifu
wao, ni kwamba kwenye baraza lao la utawala walikuwa na washauri lakini
hawakupaswa kuwa na undugu wowote na Chifu, ili iwe rahisi kwao kumdhibiti.
Licha ya huu mfumo wao wa utawala, lakini pia
Wanyakyusa waliishi kwenye jamii yenye mafungu ya madaraja ya umri.
Japo mengi ya mafungu hayo ya jamii
yalitokana na koo tofauti tofauti si koo zenye undugu.
Ukiuangalia mfumo wao kwa juu juu, unaweza
kuhisi kama walikuwa na jamii dhaifu.
Lakini ukweli ni kuwa jamii yao iliweza
kujilinda vyema, ndiyo maana hawakuwahi hata kufanywa watumwa japo kwenye
maeneo ya Konde na Karonga kulikuwa na utumwa.
Nikukumbushe tena kuwa utumwa si lazima uwe
ule wa wageni dhidi ya wenyeji kama Waraabu walivyowafanyia babu zetu.
Zamani kulikuwa na utumwa hata ndani ya
jamii na makabila mbalimbali, kiasi kwamba kuna baadhi ya jamii zilivikwa sifa
ya utwana.
Tukiendelea na ndugu zetu Wanyakyusa, wao
ni wakulima mahodari wa mazao ya aina mbalimbali kwa zamu za misimu yake.
Baadhi ya mazao hayo ni maharagwe, ufuta,
mtama, viazi vya aina mbalimbali, huku migomba ya ndizi ikichukua sehemu kubwa
ya kilimo chao.
Zamani kulima kutokana na mfumo wao wa jadi
lilikuwa ni jukumu la baba na wanawe wa kiume, au tuseme kuwa kulima ilikuwa ni
shughuli ya wanaume.
Mazao hayo hutumika kwa chakula,
kutengenezea pombe na hata kukirimiana pamoja na kuuzwa.
Kwa kuwa kilimo kilikuwa jambo la msingi,
umri haukuwa sababu ya kukwepa jukumu hilo hata kama mtu akizeeka, labda pawepo
sababu nyingine itakayomfanya ashindwe kabisa kulima.
Kutokana na kujizoesha sana kilimo na neema
ya kupata vyakula vinavyotokana na mavuno, ilikuwa vigumu sana kwa Wanyakyusa
kuhama au kuondoka eneo lao la asili linalowapatia neema hiyo ya vyakula
walivyovizowea.
Na kilimo kilikuwa muhimu sana kwao, basi
kila msimu wa mvua unapoanza walikusanyika kwa Chifu wao aliyeiita mvua.
Waliamini kuwa hata kama msimu wa mvua
umewadia, lakini ili ianze kunyesha ni lazima ikaribishwe kwa kuitwa na Chifu.
Mathalan, wakazi wote wa himaya ya Chifu
Kyungu walikusanyika Chikungu kwa Chifu wao, kwenye tambiko la mvua.
Watu hao hawakutakiwa kuwasha moto
majumbani mwao asubuhi hiyo ya tambiko la kuita mvua.
Wote walipaswa kusubiri ule moto unaowashwa
kwenye tambiko ili ugawanywe nao wawashe moto kutokana na moto huo.
Haya ndugu zangu, bado mengi ya kuzungumzia
kuhusu ndugu zetu hawa, lakini kwa leo tuishie hapa katika awamu hii ya kwanza
baada ya kuwapigia hodi.
Tutaendelea tena na simulizi za Wanyakyusa kesho.
Makala haya yamehaririwa,
yalichapishwa kwa mara ya kwanza katika gazeti la Tanzania Daima Juni 20, 2009.
Comments
Post a Comment