- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Na Innocent Nganyagwa
KARIBUNI kwa mara nyingine tena kwenye safu
yetu ambapo bado tuko kwenye eneo la makabila yanayotofautiana na mengine kati
ya makabila kadhaa tuliyowahi kuyatembelea awali kwenye safu hii.
Leo tunaingia katika sehemu ya pili ya
simulizi za Wakimbu, kabila ambalo liko kwenye eneo lililomega mikoa sita kwa
sasa, lakini halikugubikwa na makabila makubwa ya mikoa ambayo maeneo yake
yamemegwa.
Hiyo ndiyo tofauti ya kimsingi niliyoitaja
awali, ya makabila yanayopatikana eneo hilo na yale mengine tuliyowahi
kuyatembelea.
Labda nikukumbushe ndugu kama hukuwa
nasi kabla hatujawapigia hodi Wakimbu, tuliwatembelea Wanyiramba ambao nao wako
kwenye eneo hilo hilo. Bado hatujawatembelea Wanyisanzu kwenye eneo hilo.
Ni makabila yenye muingiliano wa namna
fulani, maana tutakapokuwa kwa Wanyisanzu tutakumbana na fungamano za
Kinyiramba na za Kikimbu.
Kufika kwa Wanyiramba tukakumbana na
fungamano za Kikimbu na hata baada ya kuingia kwa Wakimbu, tumekumbana na
fungamano nyingine japo hizi za sasa zinatokana na maeneo waliyoyamega ili kuwa
na nchi ya Ukimbu.
Fungamano hizo ni za Kisangu na Kibungu,
makabila yaliyoko maeneo mkabala na mpaka wa eneo la Wakimbu ambayo tutayaona
baadaye.
Basi sasa tuendelee kutathmini mambo ya
hawa ndugu zetu Wakimbu, nikukumbushe kuwa ndugu zetu hawa wako kwenye eneo
lililo katikati ya mikoa ya Singida, Tabora, Iringa, Katavi, Songwe na Mbeya.
Eneo hilo linaanzia Sikonge, kupitia Uyuyi
mashariki mwa Tabora, Igaluli (Igalula), Tura, Kizengi hadi Singida magharibi
na Manyoni.
Kwa upande wa mikoa ya Songwe, Mbeya na
Iringa, eneo lao linaanzia Idodi, Pawaga, Mbarali, Chunya hadi huko Mpanda
mkoani Katavi.
Tuliona kuwa walikuja eneo hilo kwa
mafungu, wakitokea kaskazini zaidi mwa nchi yetu.
Kundi lao la kwanza kuingia hapo ni
Wanyisamba, walioingia kutokea upande wa Unyangwila, yaani Ugogoni.
Wakaanzisha himaya ya Wikangulu chini ya
uongozi wa Mbela, aliyewagawia nduguze pia maeneo ya kuweka himaya zao.
Nduguye Magulunjega alianzisha himaya ya
Mwendo huko Lukwati, wa pili alianzisha himaya ya Mweli katika eneo lenye
vilima virefu la Igululilu, himaya ya tatu ilikuwa ya Ilasi.
Himaya hizo zilizokuwa ndani ya eneo pana
la Ukimbu litokalo Chunya hadi Sindiga kwa upande mmoja, pia Iringa hadi Mpanda
kwa upande wa pili, zilizaa himaya nyingine.
Mweli alianzisha himaya ya Kasekela, himaya
ya Mwendo ikasababisha himaya nyingine ya Isote na Ilasi alianzisha himaya
nyingine ya Nkila.
Himaya nyingi kati ya hizo ziligawiwa kwa
maridhiano, hata wageni wa jamii na makabila mengine walimegewa sehemu za
pembezoni.
Hiyo ilisaidia kuhifadhi ukubwa wa eneo la
Ukimbu, ambalo hata hivyo awali lilipatikana kwa vita.
Wakati Wanyisamba wanaingia mahali hapo
waliwakuta Wapantama, watu waoga na wafupi wenye maumbo madogo.
Waliwapiga na kuwanyang’anya eneo na
kuhodhi mamlaka kwa kujitwalia ardhi, ndipo walipoanzisha himaya zilizotawaliwa
na machifu wao.
Wakalazimika kubadili mfumo wa kurithiana
madaraka ya uchifu, ambapo awali watoto ndiyo walirithi.
Lakini kutokana na watoto hao kuuawa kwa
kijicho, wakaamua kurithisha watoto wa dada wa machifu. Hapo ndipo Wakimbu
ambalo ni kabila la kiumeni, lilipokuwa na mifumo miwili ya kiukoo.
Koo za kawaida zilikuwa za kiumeni, lakini
koo za kichifu zilikuwa za kikeni kwa majina ya utambuzi wa koo hizo.
Tulitoa mifano kadhaa ya makabila mengine,
ili kubainisha mfumo wa koo za kikeni na kiumeni. Tuliwataja Waluguru,
Wazaramo, Wakurya na Wahehe.
Hapo ndipo tulipoishia jana kwenye ziara
yetu kwa ndugu zetu Wakimbu.
Sasa basi tukiendelea kutoka hapo ni
kwamba, kuna himaya nyingine za wale Wanyisamba, kundi la awali la Wakimbu,
ambazo zilitokana na misigano na si kwa amani na maridhiano kama zile
tulizoziona pale awali.
Hizo ni pamoja na Ikokolo, Ipito na Ilamba,
msigano ulianza baada ya mtu mmoja kutoka maeneo ya Uyumbu aliyejulikana kama
Kuti, ambaye alikuwa mfanyabiashara alipopita kwa nia ya kwenda kwenye biashara
zake huko Mwera Lindi.
Usishangae, maana wengi wetu tunadhani kuwa
kutokana na vyombo vya usafiri kuwa vingi kwa sasa duniani, basi tunasafiri
umbali mrefu kuliko watu wa zamani.
Lakini ukweli uko tofauti, zamani watu
walisafiri na kutembea kwa maili nyingi hata kama iliwachukua siku nyingi. Siku
tukipata fursa hapa kwenye safu yetu, nitawadokeza jinsi ambavyyo vizazi vya
Kiajemi na Kishirazi vilivyoko Mashariki ya Kati na Arabuni, vilivyotoka Yemen
na pembezoni mwa Afrika.
Kisha watu wa jamii hizo wakaenda sehemu za
Iran na Iraq, pamoja na Aussian ambako kwa sasa kunajulikana kama Saudia.
Kutoka kule wakazunguka na kwenda Ngazija
na baadaye kuja tena pwani ya Afrika Mashariki, wakakamilisha mzunguko wao kwa
kufika tena pembezoni mwa Afrika, huko Benadir, Barawa, Somalia.
Ni historia ya kina, ndiyo maana makabila
kama Wairaqw wanatokea Iraq, kule kwa Saddam ambako zamani kulijulikana kama
Messopotamia.
Wahehe ni mchanganyiko wa Wahabeshi,
Wangazija na Wabantu, wakati Wadigo ni Wagiliama, jamii ya Wasomalia wa
pembezoni karibu na Kenya.
Tuachane na hayo kwa sasa, tuendelee na
hawa Wakimbu kwanza.
Basi katika safari mojawapo, Kuti alipofika
Igululilu katika sehemu iitwayo Mbaraga, aliweka kambi ya muda mrefu.
Kwa bahati mbaya akafariki, lakini hakuweza
kuzikwa mahali pale alipofia maana alikuwa ni kiongozi wa kigeni.
Wafuasi wake walipotaka kumzika, Chifu wa
pale aliwakatalia, wakakaidi maagizo yake na kumzika, yule Chifu akaghadhabika
na kuanzisha vita ya kuwaondoa.
Lakini alishindwa, hao wafuasi wa Kuti
wakajiimarisha na baadaye wakaenda kujieleza kwa chifu wa himaya ya Wikangulu,
ambaye alikuwa Mbela.
Walienda kwake kwa kuwa ukumbuke kwamba
hiyo ndiyo himaya kuu iliyozalisha zile nyingine.
Yeye aliwaruhusu wabakie na kuishi mahali
pale. Basi kutokana nao ndipo zikazaliwa zile himaya nyingine za Ipoto, Ikokolo
na Ilamba.
Sasa turejee kwenye yale makundi ya
Wakimbu, maana mpaka hapa tulipofikia tumeona kundi moja tu la Wanyisamba,
ambalo kimsingi ndilo lilianza kuingia nchi ya Ukimbu.
Lakini kwa ujumla kulikuwa na makundi
manne, kundi lingine ni Wanyitumba waliokuwa na eneo lao la Kipembawe ndani ya
nchi hiyo ya Ukimbu.
Hawa waliingia eneo hilo kwa kufuatana na
Wanyisamba, walipishana kidogo tu muda wa kufika hapo.
Hao nao walianzisha himaya zao za Igunda,
Ilumwe na Nyamnyam. Lakini zamani kabla ya hapo walijulikana kama Wanyampanda,
isipokuwa walinyang’anywa himaya kwa hila.
Kwenye karne ya 18, wafanyabiashara kutoka
Usagara waliiteka Kipembawe kwa kisingizo kidogo sana. Walipokuja eneo hilo
walibeba mbegu za maboga wakawapa wenyeji, kisha wakawafundisha namna ya
kupanda maboga hayo.
Lakini waliwapa sharti kuwa maboga
yakikomaa wale, lakini wabakize mbegu ili watakaporudi kutoka safari zao za
kibiashara wazikute mbegu zao.
Tuseme ni kama waliwaazima tu, lakini wale
wenyeji wakanogewa na kula yale maboga kabla hayajakomaa vizuri pamoja na zile
mbegu zake, bila kuzibakisha.
Wasagara waliporudi hawakukuta mbegu kama
walivyokubaliana, wakadai wapewe nchi kama fidia.
Kutokana na kuwa na silaha bora, mtawala wa
Wanyitumba aliisalimisha himaya yake kwa Wasagara waliohodhi mamlaka.
Kuanzia muda huo wakajitambulisha kama
Wanyitumba (yaani watu kutoka huko Usagara) na wakaeneza utawala wao hadi
Iswangala, huko maeneo ya Sikonge na ndani ya eneo hilo ndipo zile himaya za
Igunda, Ilumwe na Nyamnyam zilikuwemo.
Kundi lililofuatia kati ya yale manne ni la
Wanyangwila, ambalo Chifu wake alikuwa Mkugansi (Mkuga Nsi – mvumbuzi wa nchi),
yaani kwa tafsiri ya jina lake ni ‘Mtu aliyevumbua au kuokota nchi’.
Huyu alikuwa kwenye himaya ya Unyangwila
ambayo baadaye ilizaa himaya za Ngulu, Unyanyembe, Kisalusalu, Kihwele, Itumba
na Kipili.
Watu wa maeneo hayo wote ni
Wakimbu-Wanyangwila. Najua kuna majina mawili ya himaya zao yatakutatiza
kidogo.
Nitakufafanulia, Wanyanyembe ambao wengi
tunawafahamu kama Wanyamwezi kwa asili ni Wakimbu.
Kabla hata ya Uhuru wa Tanganyika kulikuwa
na shirikisho la Ukimbu, ambalo Mwenyekiti wake alikuwa Chifu Haruna Lugusha wa
Sikonge.
Huyo alifariki mwaka 2007, akiwa na umri wa
zaidi ya miaka 80.
Hiyo ina maana kuwa, kwenye hilo shirikisho
lao himaya kama hizo za Unyanyembe na nyingine zilizotokana na vita, au urithi
wa uchifu kwa watoto wa machifu zilikuwemo ndani ya shirikisho hilo.
Mathalan, aliyeanzisha himaya ya Unyanyembe
na Itetemwa, aliitwa Swetu, mtu ambaye alisigana na kupigana na nduguze.
Ile himaya nyingine ya Kihwele, ambayo
najua Wanyalukolo wengi watashtuka kusikia ilikuwa Ukimbu, ufafanuzi wake ni
rahisi hasa ukizingatia jiografia ya Uhehe na Ukimbu.
Nadhani tunaelewana, na kwa kumalizia
kutathmini makundi yao kuna kundi dogo la mwisho la Wanyikungu ambalo nalo
lilitokana na Wanyangwila.
Hawa eneo lao linaishia hadi kwenye msitu
wa Wanyiramba, huko Tarafa ya Ndago, mkoani Singida.
Watoto wa Ikugansi, Mnyangwila mwinda tembo
pamoja na Wanyangwila wenzie, walipigana kwa sababu ya biashara ya ndovu.
Kisha walihamia Usumbwa na kuanzisha himaya
za Uyogo na Ukuni, walifanya hivyo ili wapate uhuru zaidi wa kuwinda tembo.
Lakini kwa asili wametokea Ukungu kwa
Wanyikungu, ambao kimsingi ni Wanyangwila, kundi dogo na la mwisho kati ya
makundi yanayounda kabila la Wakimbu.
Simulizi zinanoga lakini nafasi yetu
inatubana.
Kwa kuwa yamebakia mambo machache
yanayowahusu hawa Wakimbu, yanayojumuisha imani zao, matambiko na rasilimali
walizozitegemea kiuchumi, basi tutamalizia simulizi zao wakati mwingine kwa
kutazama mambo hayo.
Kama ilivyo kawaida ya miadi yetu, nakusihi
usikose kuungana nami kesho ili tutopee zaidi kwenye kina cha ujadi.
Makala haya yamehaririwa,
yalichapishwa kwa mara ya kwanza katika gazeti la Tanzania Daima Februari 28, 2009.
Comments
Post a Comment