- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Akinamama wa Kiiragw wakiwa wenye mkutano.
Na Innocent Nganyagwa
LEO tunakutana kwa mara nyingine kwenye
safu yetu ya mambo ya kijadi ambapo tunamalizia ziara iliyotuchukua takriban
awamu tatu kuwatembelea ndugu zetu Wairaqw.
Basi nawakaribisheni tukamilishe tathmini
ya kabila hili la Kikushi, watu ambao kwa asili wanatokea mahali palipofahamika
kama Messopotamia hapo zamani (kwa sasa ni Iraq).
Kama ulikuwa nami tangu
tulipoanza kuwatembelea hawa Wairaqw, nadhani utakuwa umefaidika kwa
kufahamu mambo mengi yanayowahusu ndugu zetu hawa.
Tumeona mambo yao kadhaa, ambapo jana
tuliona baadhi ya nyimbo zao za sherehe za harusi, maombi na shukurani kwa
Mungu kwa mafanikio ya mavuno ya mazao. Pia tuliona juu ya ufundi wao wa
kujitengeneza mavazi yao ya asili, zana za kivita na kilimo na ujuzi wa
kuhifadhi nafaka kwenye maghala yao ya asili bila kuharibiwa na wadudu.
Kati ya mambo tuliyoyaona ambayo ya kuvutia,
ni kufahamu kuwa wanaoitwa Wambulu kwa asili ni Wairaqw waliotengwa.
Maana jina hilo la Wambulu mara nyingi
husababisha mhemko wa hisia kali kidogo baina ya jamii hizo mbili zenye asili
moja.
Tulifahamishana kuwa Mbulu
ambayo kwa sasa ni wilaya, ni jina la Muiraqw wa kwanza kufiwa na mkewe katika
mazingira ya kutatanisha. Hivyo basi alihisiwa kuwa na mkosi na ilibidi
atengwe, huyu ndiye alienda kuanzisha mji wa Mbulu. Baadaye alifuatiwa na
Wairaqw wengine, waliofiwa na wake na waume zao katika hali za kutatanisha pia.
Niliwatahadharisheni kuwa jina hilo la
Mbulu inawezekana linatokana na matamshi ya kimazoea tu, lakini pengine kuna
jina la matamshi yao ya asili ya Kiiraqw, maana ndugu zetu hawa lugha yao ya
Kimessopatamia, ni tofauti sana na lugha za wengine tulizozizoea.
Jina halisi la huyo mtengwa wa kwanza
aliyekwenda kuanzisha mji wa Mbulu, kitu kilichosababisha watokee watu
wanaojiita Wambulu ni Imboru.
Kwa hiyo, usishangae ukikutana na wenyeji
halisi wa huko wakakutajia mji huo kwa jina hilo, pia usishangae nikisema mji
wa Mbulu wakati wewe unapafahamu sehemu hiyo kama wilaya. Licha ya wilaya kuwa
na mji wake lakini pia kwa lugha yetu ya kijadi ya safu hii, huwa tunatumia
matamshi yenye kutupa tafsiri muafaka kijadi.
Mathalan, tukisema nchi ya Wairaqw
tunamaanisha eneo linakopatikana zaidi kabila hilo.
Kwa msingi huo huo, hata makabila mengi
yamepata majina kutokana na sifa tanzu za jamii zake za awali.
Mathalan, Wahehe tulianza kuitwa hivyo
karne ya 18 tulipokuwa chini ya utawala wa Munyigumba.
Huyu ni baba yake Mkwawa aliyeziunganisha
jamii za kwetu huko Lilinga (Iringa), katika mapigano dhidi ya maadui wa himaya
yetu.
Maneno ya morali wa kivita tunapowavamia
maadui tukipiga kelele, ndiyo yalitupa jina la kabila letu.
Kama ulikuwa hufahamu basi napenda
nikufahamishe kuwa mimi ni Mhehe, ninayejivunia mno asili yangu.
Ni sawa na Waluguru ambao kiongozi wao wa
mwisho aliyewafikisha ilipo nchi ya Uluguru hivi sasa, alikuwa Luguru, yaani
mwenye ulemavu wa mguu. Luguru ni Kiguru kwa tafsiri ya Kiswahili, kwa hiyo
kuwaita ‘Wa-luguru’ ni sawa na kusema wale wafuasi wa yule mtu mwenye kilema
cha mguu.
Au Wameru, jina ambalo kimsingi lilitokana
na watu wa kabila hilo kukwea Mlima Meru kukwepa mapigano.
Lakini kiini hasa ya kabila hilo ni jamii
ya Varwaa, walioitwa hivyo hapo awali kabla ya kuitwa Wameru. Kurwaa kwa lugha
yao ina maana ya kukwea, lakini hadi kufikia sasa kabila hilo linaundwa na
mchanganyiko wa jamii za hao Warwaa wenyewe wanaotokea uwanda wa Milima
Usambara, Wachagga wa Kimachame, Wapare na Wapalanjo.
Kwa hiyo nadhani unanielewa vyema kuhusu
Wambulu, japo tofauti yao na haya makabila mengine yaliyopata sifa za majina
tofauti na jamii zao za awali, ni kwamba wao mambo yao mengi bado ni ya
Kiiraqw. Hivyo, inakuwa vigumu hasa kuchukuliwa kama kabila kamili, japo kwa
huku mijini kuna baadhi yao hujitambulisha kama Wambulu. Lakini ukweli ni kuwa
wao ni wale wale Wairaqw kutokea Mbulu, mji wa mtengwa wa Kiiraqw.
Naam, baada ya kueleweshana vyema juu ya
jambo hilo, tuendelee na simulizi ya leo kuhusu hawa Wairaqw.
Kama
tulivyoona jana juu ya nyimbo zao za harusi, basi nikufahamishe kidogo juu
ya ndoa zao.
Ndugu zetu hawa wana ndoa za aina kama tatu
hivi, ambapo aina ya kwanza ni kwa familia mbili za wanandoa kukutana na
kupanga kuwaozesha vijana wao sanjari na kiwango cha mahari na utaratibu wa
sherehe husika.
Aina nyingine ya ndoa ni ile inayotokea kwa
binti ‘kutekwa’ na kijana aliyempenda, tuliwahi kuona aina hii ya kuoana kwenye
baadhi ya makabila tuliyoyatembelea siku zilizopita.
Utekaji huu wa kumvizia msichana njiani
unaofanywa na marafiki wa mtekaji kwa maagizo yake, mara nyingi haukufanywa na
watu wa kawaida. Maana kama unavyoona, ni kuridhisha matakwa ya upande mmoja
zaidi hata kama yule binti kimsingi hajampenda huyo anayemteka.
Uoaji huo mara nyingi ulitumiwa na watu
waliohofiwa kwenye jamii zao, mathalan wanaweza kuwa viongozi wa madaraja
mbalimbali au waganga.
Binti anayesombwa kwenye ndoa ya aina hii
akishajamiiana tu na yule aliyeagiza asombwe, basi hachukuliwi tena kuwa na
hadhi ya msichana bali ni mwanamke. Maana hadhi yake inakuwa imeshavushwa
daraja kwa mbinu hiyo, nadhani unanielewa nikikueleza hivyo.
Lakini ndoa hizi za kutekana baadaye
ziliachwa na watu wengi, waliobaki kuendelea na mchezo huo ni waganga wa mvua.
Na hata hao hawakutumia nguvu bali kwa
kutumia uwezo wao wa uganga, kwa kufanya ulozi wa kumwagia matone ya mafuta au
kumgusa binti kigoli na mafuta hayo. Naye humfuata kwa hiari yake, kutokana na
nguvu ya ulozi wa ile dawa ya kijadi iliyochanganywa kwenye mafuta hayo.
Lakini ndoa iliyo tofauti zaidi, ni ile
ambayo familia isiyo na mtoto wa kiume inapomnunua binti na kukodi wanaume wa
kujamiiana naye ili azae watoto.
Ndoa hiyo ambayo kwa jina jingine
hujulikana kama ‘ndoa ya kivuli’ hutumika zaidi na familia ambazo licha ya
kutokuwa na mtoto wa kiume, lakini pia labda baba ameshafariki dunia.
Familia husika hufanya hivyo ili
kujiongezea uzao, maana watoto watakaozaliwa si wa wale wanaume wanaojamiiana
na yule binti kwa kuwa wao wameshalipwa ujira wao kwa kazi hiyo.
Kama hujawahi kusikia mambo kama hayo
unaweza kushangaa, lakini makabila mengi yanayotokana na mbari ya Kikushi au
mbari tanzu zenye mchanganyiko wa Kikushi yana kawaida hiyo.
Wakati tutakapowatembelea Wamaasai kwenye
safu yetu, nitawaeleza juu ya tabia yao ya kumkirimu mgeni mke alale naye.
Japokuwa ni kwa hiyari ya mke mwenyewe atayeambiwa na mumewe afanye hivyo,
maana kwa kawaida wao huoa wake wengi.
Basi endapo kwa ule usiku mmoja yule mgeni
aliyekaribishwa, mke akijaamiana naye na kumpa ujauzito, mtoto si wake bali wa
yule mwenyeji aliyemkirimu mkewe alale naye.
Ni moja ya mastaajabu ya kijadi, lakini
hizo ni baadhi ya mila za baadhi ya makabila ambazo nyingi zimeanza kutoweka
kutokana na hali halisi ya sasa.
Lakini kama ilivyo kwa makabila mengi,
mambo haya ambayo labda wanaharakati wa sasa wa haki za akina mama wanaweza
kushangazwa nayo, kwa Wairaqw ni mambo ya kawaida yaliyozoeleka kwenye kabila
lao tangu zamani.
Kwa hiyo, hata kama mwanamke anapata
matatizo kwenye ndoa yake kama vile kupigwa, wao huchukulia kuwa mume anaonesha
ukuu wake kwenye kaya.
Kama mume huyo ataadhibiwa basi zaidi
atatozwa faini tu, ila mwanamke atakayepigwa akikimbilia kwa wazazi wake na
kudai talaka atachekwa na familia yake.
Familia hiyo itamtaka arudi kwa mumewe,
maana ni kawaida kwa mume kuonesha nguvu ya mamlaka yake kwenye familia. Lakini
yule mume hata kama utaratibu unamruhusu kumuadhibu mkewe kwa kumpiga, anapaswa
kuwa mwangalifu sana kwa kutompiga kichwani. Kama akimpiga mkwe kichwani na
kumjeruhi kiasi cha kumtoa damu, basi atatozwa faini ya kulipa ng’ombe wengi.
Ndugu zetu hawa wana mfumo wao wa uongozi
kwa ngazi mbalimbali, kuanzia kifamilia, kiukoo na jamii nzima ya kabila lao.
Kiongozi mkuu wa jamii ni ‘Kahamusmo’ ambaye husaidiwa na ‘Yaabusmo’ hayo ni majina ya hadhi za
vyeo vyao.
Mfumo wao huwezesha kila kiongozi kutimiza
wajibu wake ipasavyo kwa ngazi yake, bila maingiliano yoyote yanayoweza kukwaza
mfumo wenye ushirikiano unaoeleweka.
Ukiondoa hao viongozi, watu wengine muhimu
ni waganga wa jadi ambao wana hadhi inayokubalika kwenye kabila hilo.
Nadhani bado unakumbuka uwezo wao wa
uganga, kama tulivyosimulia
kiongozi wao Haymu Now Hatype alivyohamisha ziwa Manyara ambalo wenyewe
huliita ‘Tlawta Mooya’ ili kupata nchi ya kuishi na kulima.
Wairaqw huwafunza watoto wao maadili mema
ya kijamii tangu wakiwa wadogo, ambapo binti hufunzwa na mama yake hadi pale
anapokaribia kuishi na mume.
Mafunzo hayo ni jinsi pia atakavyoitunza familia
yake, kama ambavyo kijana wa kiume pia hufundishwa na baba yake hadi
anapoanzisha familia yake mwenyewe kwa kuoa.
Katika mafunzo hayo kuna mambo ambayo ni
lazima kwa jinsia husika ya mtoto kuyafahamu, mathalan mtoto wa kiume lazima
ajue kuchunga.
Ndugu zetu hawa wenye mfumo wao wa kuamua
kesi kwa makosa yaliyotendeka, ambapo wazee ndiyo wanahusika na jukumu hilo.
Lakini katika kusikiliza matatizo hayo
huzingatia jinsia, kama mkosaji ni mwanamke, basi shauri lake lilisikilizwa
kwanza na wazee wa kike. Kisha baada ya kupata mustakabali wa uamuzi wao, hukaa
pamoja na wazee wa kiume kwa uamuzi wa mwisho.
Lakini si lazima mtuhumiwa akikutwa na
hatia shauri linaposikilizwa na baraza la wazee wa jinsia yake uamuzi ukabaki
hivyo linapokaa baraza zima la jinsia mbili.
Japokuwa mara nyingi huwa hivyo lakini
maana ya kuanza kupeleka shauri kwa wazee wa jinsia husika ya mtuhumiwa, ni
kutokana na ule mfumo wa wajibu wa malezi ya mtoto kijinsia.
Kwa hiyo, haya mambo ya mahakama na rufani
yapo tangu zama hizo za kijadi, ni mifumo iliyokopwa na kuwekwa kisasa kwenye
maisha yetu ya siku hizi.
Kama mtuhumiwa wa hizo kesi zao za kijadi
za Kiiraqw akikutwa na makosa ya kutozwa faini, hulipishwa faini hiyo ambayo
huitwa ‘dohho’ kwa lugha yao.
Lakini kama ikitokea mtuhumiwa akakutwa na
hatia lakini bado hakubali kukiri makosa yake, basi adhabu yake ni kutengwa
kabisa na jamii yote.
Kwa kesi ambazo ushahidi wake hauko wazi
sana, wahusika wote yaani mlalamikaji na mlalamikiwa huapishwa kuwa
watakayoyasema ni ukweli.
Kama ni ya uongo, basi atakayedanganya
atapata laana kutokana na kiapo alichokula.
Mambo unayoyashuhudia sasa ya kuapishana
mahakamani yasikushangaze, hayakuanza jana wala leo bali yalikuwapo tangu
zamani.
Tena kwa wakati huo ukidanganya unaweza
kusalimika kwenye maamuzi ya shauri husika, lakini ile laana hakika
itakushukia!
Basi kama unavyoona werevu wa ndugu zetu
hawa kwenye mambo yao mengi, basi hata kwa tiba za kijadi ni mahodari sana.
Hutumia dawa za mitishamba za mizizi ambayo husagwa au kuchemshwa mizima kama
ilivyo, kisha mgonjwa hupewa anywe ili kujitibia.
Haya, simulizi za ndugu zetu hawa zinanoga
lakini pia nafasi yetu nayo imetuishia. Sina budi kukamilisha mambo ya Wairaqw licha
ya kwamba kuna mengi yanayowahusu ambayo hatukuyagusia.
Tunalazimika kupeana fursa ya kuwafikia
Wajadi wengine pia wanaosubiri kutimizwa maombi ya simulizi za makabila yao,
ili nao wajitambue kijadi.
Tuweke miadi ya kukutana tena kesho ili kuwafikia
Wajadi wengine.
Makala haya yamehaririwa
na yalichapishwa mara ya kwanza kwenye gazeti la Tanzania Daima Aprili 18,
2009.
Comments
Post a Comment