- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Bango linaloonyesha tamasha la sanaa za Wabembe lililofanyika kwama 2017 huko Marekani
Na Innocent Nganyagwa
NDUGU zangu, karibuni kwenye safu yetu ya
kijadi inayoangalia Asili na Fasili yetu, inayotufanya tujivunie ujadi wetu wenye
asili ya Kiafrika.
Baada ya kutoka kwa Wairaqw, sasa tunatua
mkoani Kigoma, tunapiga hodi kwa ndugu zetu Wabembe, ambao kwa asili wanatokea
kwenye eneo lenye msongamano wa makabila.
Kabla hatujaanza kuwatembelea ndugu zetu
hawa, nikufahamishe tena dira ya ramani yetu.
Tukitoka kwa Wabembe tutapiga hodi kwa
Waha, ambao watafuatiwa na Wakimbu, lakini hadi kuwafikia hao Wakimbu, tutakuwa
tumeshaanza mwendo wa taratibu kuelekea tena kaskazini mashariki, tukipitia
eneo la katikati mwa nchi yetu.
Katika njia hiyo tutakayopitia, kuna ziara
za kuyatembelea makabila ya Wanyisanzu, Wanyiramba, Warangi na Wasi.
Safu hii ni kwa ajili yetu sote, hivyo basi
unapowasilisha ombi la kutembelewa kabila lako kimakala, huwa nalijumuisha
kwenye orodha ya maombi ninayoyapokea awali.
Nikufahamishe kuwa, nilianza kupokea maombi
siku nyingi sana zilizopita, kiasi kwamba kuna muda yalikuwa mengi mno, ikabidi
nisitishe kwa muda kupokea maombi hayo. Nilifanya hivyo, ili nipate nafasi ya
kupunguza mzigo mkubwa wa maombi niliokuwa nao.
Lakini, kuna ombi moja kwenu ndugu zangu,
nawasihi mfuatilie kwa karibu ziara zetu na kusoma kwa makini uchambuzi wetu.
Ndugu zetu hawa Wabembe wanaoongea lugha
yao ya Kibembe ambao wakati mwingine jina lao hutamkwa ‘Wabeembe’, wanapatikana
mkoani Kigoma, huko wapo zaidi kwenye Wilaya ya Kigoma Vijijini.
Ndugu zetu hawa wanawiana na idadi kadhaa
ya makabila. Wanatangamana na Wamanyema, Wabangubangu, Wagenya, Wagoma, Wakusu,
Warege, Wahoholo, Wambwari nakadhalika.
Lakini hawa ndugu zetu Wabembe huko
wanakotokea, wanatangamana na makabila mengi mno kuliko unavyoweza kufikiria.
Takwimu za mwisho za idadi ya makabila hapa
nchini, ziliainisha kuwa tuna makabila yapatayo 120. Lakini, tarakimu hizo za
makabila zinatatanisha kutokana na ukweli kwamba kuna makabila yaliyopoteza
utambulisho kwa kumezwa na mengine, yapo pia yanayojitambulisha kwa majina ya
makabila mengine yakiwa mbali na maeneo yao ya asili.
Yapo pia makabila yanayopotea kutokana na
mbari kuingiliana, au makabila ya ‘mbari’ tofauti yanayochanganyika na
kuzalisha jamii nyingine ya watu, ambao huamua kujitambua kama kabila.
Pia usisahau makabila yaliyotengwa au
kujitenga na makabila yao ya asili, kwa namna hiyo si rahisi kuwa na idadi ya
makabila 120 tu hapa nchini.
Pengine inabidi tufanye kazi ya ziada kuanza
kuorodhesha makabila yetu, kazi ambayo tukiianza hatujui tutaimaliza lini, hiyo
ni kama tukiamua kufanya hivyo.
Maana ya kukueleza yote hayo ni kwamba,
kuna makabila ya maeneo ya pembezoni mwa mipaka ya nchi yetu yanayotokea nchi
jirani. Makabila mengine yamesababishwa yaonekane yanatokea nchi jirani,
kutokana na mgawanyiko uliosababishwa na mipaka iliyochorwa na wakoloni.
Mipaka ya kijadi ni ile ya himaya za
kichifu za makabila mbalimbali, kwa maeneo yao husika waliyoyatumia kuendeshea
maisha yao ya kila siku.
Basi hawa Wabembe nao wana hali kama hiyo,
kwa asili wanatokea huko Kongo, ndiyo maana wanapatikana zaidi kule Kigoma.
Kama unaifahamu vyema jiografia kwa jinsi
ramani ya nchi yetu ilivyo, sina shaka unanielewa nikikutaarifu hivyo.
Hata baadhi ya makabila mengine yanayowiana
nao kwenye maeneo waliyopo, yanatokea huko, mfano mzuri ni Wamanyema, Wahoholo
na Warege.
Huko wanakotokea, Wabembe ni kundi dogo,
yaani si kabila kubwa kulinganisha na makabila mengine ya Kongo.
Najua utakuwa unajiuliza mbona nataja Kongo
tu bila kuainisha ni Kongo ipi kati ya zile mbili? Ile ambayo ni Jamhuri ya
Kongo au Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), ambayo wakati wa Mobutu
iliitwa Zaire?
Wabembe wanapatikana kwenye Kongo zote
mbili, ile yenye mji wake mkuu Brazzaville na ile yenye mji mkuu wa Kinshasa,
ambazo hapo zamani zilikuwa himaya moja.
Wabembe waliishi kwenye uwanda ulio
kaskazini mwa Mto Zaire, ambapo majirani zao walikuwa Wateke na makabila
mengine.
Ndugu zetu hawa wenye utajiri mkubwa wa
utamaduni, hasa wa uchongaji, kama tutakavyoona hapo baadaye, huko walikotoka
kuna makabila mengi kwa kweli kulinganisha na hapa kwetu.
Inasemakana Kongo ya DRC ambayo ni kubwa
kwa eneo, ina makabila makubwa na madogo yanayokaribia 420 kwa idadi.
Nikutajie baadhi tu ya makabila ya huko
Kongo (ya Brazaville) kuna makabila kama vile ya Wateke, ambao ni majirani wa
Wabembe. Makabila mengine ni pamoja na Wababochi, Wakuyu, Wakongo, Wakwele,
Wavili, Wamboshi, Wasanga na Wasundi.
Inavyoelekea, katika ule mgawanyiko
uliozalisha nchi mbili za Kongo, DRC ilibakiwa na makabila mengi zaidi. Huko
kuna makabila ya Wayaka, Walar, Wapakibeti, Wazande, Wabaali, Wababyeru,
Wakongo, Wabakuba, Wabushongo, Wambuti, Walega, Wali, Walwalwa, Wambole,
Wangba, Wango, Wapende, Warambo, Warambu, Wasala, Wasalampasu, Wasongye, Wasuku
na Wateke wapo huko pia.
Makabila mengine ni Wati, Watsioko,
Watchokwe, Wabeke, Wabemba, Wabena Wiembe, Wabena Luluwa, Wawila, Wawinja,
Wawinza ambao moja ya jamii zake tanzu ilizalisha Wasukuma na Wanyamwezi
waliopo hapa nchini.
Wawira, Waboa, Wabobangi, Wabodo, Waboenga,
Wabolia, Waboloki, Wabombo, Wabopgandi, Waboyela, Wabua, Wabudu, Wabuja,
Washongo, Wawuyu, Wawaka, Wayeru.
Hayajaisha, pia kuna Wandengese, Wadongo,
Wakonda, Wagenya, Wagoma, Wagyeli, Wahamba, Wahemba, Wahoholo, Wahungana,
Wahutu, Wajonaam, Wakanu, Wakela, Wakomo, Wakusu, Wakwame, Waleka, Waleku,
Walengola na Walese.
Mengine ni Walibinza, Walikao, Waliko,
Walobala, Walobo, Waloi, Walokele, Walombi, Walombo, Walomotwa, Waluba, Waluba
Upemba, Walunda na Wamakere.
Pia kuna Wamalele, Wamamvu, Wamangbetu,
Wamanja, Wamayogo, Wamayombe, Wammba, Wambanja, Wambesa, Wambo, Wambole, Wambuti,
Wamedje, Wamituku, Wamondunga, Wamongo, Wamotembo na Wamuserongo.
Kwa kumalizia baadhi ya makabila hayo,
maana tukitaka kuyataja yote tutaishia kutaja makabila tu kutokana na idadi
yake, ni Wamvuba, Wanalu, Wanande, Wandaaka, Wandaka, Wandengese, Wandolo na
Wangala. Pia kuna Wangombe, Wakundo, Wankutu, Wantomba, Wanyali, Wanyanga,
Wanyindu, Waotetela, Wapere, Wapopoi, Washi na Wasonge.
Mengine ni Wasongola, Wasundi, Watabwa,
Watembo, Watopoke, Watumbwe, Watutsi, Wagoma-Babuye, Wawongo, Wawoyo, Wayaka,
Wayombe, Wazande, Wazimba na Wazombo.
Nadhani mnaona jinsi huko walikotokea ndugu
zetu hawa, kulivyojazana makabila mengi. Wabembe ambao utamaduni wao umegubikwa
na mambo ya maeneo yao ya asili, pamoja na majirani zao waliowiana nao, mfumo
wao wa kijamii umeelemea uzao wa ndoa.
Hata kama watu wa familia moja
watatawanyikia maeneo ya mbali, lakini utambulisho wao waliouhifadhi
huwawezesha kutambuana hata kwa vizazi vitatu kabla au baada.
Vijiji vya makazi yao vinasimamiwa kwa
uongozi wa machifu, ambapo chifu husika ‘ngaluba’ ana jukumu la kuwasiliana na
mizimu kwa kuwa wanaamini katika mizimu.
Uwindaji ndiyo shughuli yao kuu, kwa
kawaida kabla ya kwenda mawindoni, kiongozi wao huwasiliana na mizimu. Hutumia
vinyago vilivyochongwa mahsusi, akipiga magoti mbele yake kama mwindaji
anayejitayarisha kumuangamiza mnyama mawindoni.
Licha ya kuamini mizimu, Wabembe pia
wanaamini kuwa kuna Mungu muumba ‘Nzambi’
ambaye kutokana na ukuu wake na uwezo alionao, hawakuweka kitu chochote
kukifananisha naye. Mjadi mwenzangu, tumeshawahi kuona huko nyuma, kuna
makabila ambayo yana alama yanayozichukulia kama taswira ya Mungu.
Alama hizo ni kama jua nakadhalika, lakini
hawa Wabembe hawakujiwekea alama yoyote ya kitaswira kutokana na imani yao juu
ya ukuu wa Mungu. Kwao, Nzambi, yaani
Mungu, ndiye anayedhibiti maisha na kifo, japo wanaamini pia kuwa kifo kinaweza
kutokana na ulozi wa mchawi ‘ndoki’ ambaye anaweza kutumia ushirikina wake
kuroga.
Wao huamini kuwa, mizimu ya mababu zao
inahusiana kwa karibu na watu walio hai, huwatolea mizimu hao sadaka.
Hufanya ibada zinazoongozwa na kuhani,
ambaye hutimiza ibada hizo mbele ya vinyago vinavyoitwa ‘kitebi’ au ‘bimbi’
vilivyochongwa na waganga.
Vinyago hivyo ambavyo huwakilisha taswira
za mizimu, huvishwa kama waganga au wawindaji.
Kusujudu mbele ya vinyago vya mizimu ya
mababu ni jambo walilolianza siku nyingi kwenye kabila lao.
Japokuwa hapo zamani mambo hayo
yalianzishwa na waganga, waliotumia ‘nkisi’ yaani vinyago vyao vya kupigia
ramli.
Tumeshapiga hodi kwa Wabembe na tumeshaanza
kuona mambo yao.
Tukutane kesho.
Makala haya yamehaririwa,
yalichapishwa kwa mara ya kwanza katika gazeti la Tanzania Daima Novemba 29, 2008.
Comments
Post a Comment