Featured Post

KAMPUNI YA PREMIUM AGRO CHEM LTD YASAMBAZA MBOLEA MASAA 24 KUTEKELEZA AGIZO LA RAIS MAGUFULI

 Meneja Biashara na Masoko wa  Kampuni ya Premium Agro Chem Ltd, Brijesh Barot (kulia), akiangalia upakiaji mbolea uliofanyika katika maghala ya kampuni hiyo, Vingunguti jijini Dar es Salaam leo asubuhi.
Mbolea ikipakiwa katika malori tayari kwa safari ya kupelekwa mikoani.

Na Dotto Mwaibale
KAMPUNI ya Premium Agro Chem Ltd imeendelea kutekeleza agizo la Rais Dkt. John Magufuli kwa kusambaza mbolea kwenda mikoani kwa masaa yote bila ya kujali mapumziko ya Sikukuu ya miaka 54 ya Mapinduzi ya Zanzibar inayofanyika leo nchini kote.

Akizungumza na waandishiwa habari wakati akisimamia upakiaji wa mbolea hiyo kwenye maghala ya kampuni hiyo yaliyopo Vingunguti jijini Dar es Salaam leo, Meneja Biashara na Masoko wa kampuni hiyo, Brijesh Barot, alisema kwamba kwa jana wamesambaza mifuko 20,563,000 sawa na tani 1,028 na kuwa mbolea hiyo inasambazwa   kupitia kwa mawakala wao.

"Tunaendelea kusambaza mbolea kwa mikoa yote, Njombe, Ruvuma, Mbeya, Iringa, Rukwa, Songwe na Katavi, kupitia kwa mawakala pamoja na kuwatumia maafisa wetu walio katika vituo vya matawi yetu huko kwa ajili ya kuharakisha upatikanaji wa mbolea kwa wakulima vijijini," alisema Barot.

Barot alisema kuwa kwa leo watasambaza mifuko 1,200 sawa na tani 600 na hiyo ni kwa mbolea aina ya Urea ambapo alisema usambazaji unaendelea vizuri.

Alisema kampuni yao inafanyakazi kazi hizo kizalendo ndiyo maana wamekubali kuuza kwa bei elekezi mbolea ambayo wao walikuwa wameinunua muda mrefu kabla ya kutolewa kwa maagizo ya kununua kwa mfumo maalum wa serikali, na hili linafanywa kwa kumuunga mkono Rais Dkt Magufuli na Waziri Mkuu Majaliwa Kassim Majaliwa.


Comments