- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Lilian Joseph Tungaraza, maarufu Lilian Internet, akiwa anamtazama mtoto wa sungura mwenye miezi
miwili katika shamba lake lililoko Bunju jijini Dar es Salaam. PICHA ZOTE NA DANIEL MBEGA/MAENDELEOVIJIJINI BLOG.
Lilian akiwa amembeba jogoo wa jamii ya Kuchi ambao ni miongoni
mwa kuku wa kkienyeji anaowafuga.
Lilian akiangalia kuku wake aina ya Saso ambao ni maalum kwa
uzalishaji wa mayai ya utotoleshaji.
Hapa anaangalia mazao mbalimbali kwenye shamba lake.
Na Daniel Mbega, MaendeleoVijijini Blog
TAKRIBAN kilometa mbili kutoka kituo cha
Mianzini, Bunju A kwenye barabara kuu ya kutoka Dar es Salaam kwenda Bagamoyo
katika eneo la Mkanada utakutana na manzari ya pekee kutokana na miti ya
matunda iliyostawi vyema.
MaendeleoVijijini ilishuhudia kwamba, mingi kati ya miti hiyo ni mipapai, ambayo
licha ya ufupi wake, lakini tayari imeanza kuzaa katika upande mmoja wa eneo
hili lenye ukubwa wa takriban ekari mbili.
Nyumba kubwa ambayo bado haijaezekwa
itakulaki sawia huku pembeni kukiwa na nyumba nyingine chini ya miti yenye
kivuli.
Hapa nakaribishwa na dada ambaye amevalia
gauni la kumbwaya – wenyewe wanaita ‘Dela’ – la rangi ya manjano.
Tangu nimemfahamu dada huyu takriban miaka
20 iliyopita akiwa na bendi za Diamond Sound ‘Wana Dar es Salaam Ikibinda Nkoi’
na African Stars ‘Twanga Pepeta’, ndiyo kwanza namuona akiwa amevalia vazi la
aina hii, na kwa hakika ndiyo mara ya kwanza kumkuta katika mazingira kama haya
maana siku zote nimekuwa nikimuona jukwaani akinengua kwa ustadi wa juu kiasi
cha kujipatia umaarufu mkubwa.
“Naitwa Lilian Joseph Tungara, mashabiki
wangu wamezowea kuniita Lilian Internet,” ndivyo anavyojitambulisha kwangu huku
akitabasamu.
Ingawa kuna kivuli, lakini ananikaribisha
moja kwa moja nyuma ya nyumba ambako anasema alikuwa na shughuli za kufanya –
na ndizo zilizonipeleka huko.
Ninalakiwa na kelele nyingi za kuku walio
katika mabanda matatu tofauti, lakini kwanza ananipeleka kwa banda dogo la
pembeni na kufungua mlango mmoja mdogo.
“Hili ni banda langu la sungura, nawapenda
sana, na ninataka kufuga kibiashara zaidi,” anasema huku akimtoa sungura mmoja
mdogo na kumshika kwa makini ili asimuumize.
“Muziki ni fani yangu, upo kwenye damu,
ninaupenda na siwezi kuuacha kwa sababu ndio ulionifanya nijulikane, lakini
hapa ndiyo maisha yangu – ujasiriamali. Nimeamua kujikita katika ujasiriamali,
hasa katika sekta ya kilimo na mifugo, kwa sababu naamini ndiyo pekee inayoweza
kunipa tija.
“Hapa nimepata uzoefu – japo naendelea kujifunza
– na kwa kutumia shughuli hizi ninafanya biashara pia. Malengo yangu ni kuona
kwamba hapa panakuwa shamba darasa ili
niweze kuwafundisha na wengine, ingawa mimi mwenyewe bado naendelea kujifunza,”
anasema kwa furaha.
Kwanini sungura?
Anasema kwamba ameamua kufuga sungura kwa
sababu anaamini ni biashara ambayo inaweza kuwa na tija siku za usoni.
“Ujue sungura ni mnyama rahisi wa kufuga kwani hana gharama kubwa sana, huhitaji
kuwa na mamilioni ndipo uanzishe mradi kama huu, tena sungura akitunzwa vyema
inavyostahili haugui kwa urahisi na pia lishe yake ni rahisi kupatikana.
“Kama
unavyoona hapa, nawalisha nyasi, mboga kama vile sukuma wiki, spinachi,
kabichi, karoti, mchunga, bado sijaanza kuwanunulia pellets na wanaendelea
vizuri kabisa,” anafafanua.
Anasema
kwamba, kwa kuwalisha vyakula hivyo vibichi sungura wanakojoa mara kwa mara, na
mkojo wake ni mali unaweza kumpatia kipato kikubwa hapo baadaye kwa sababu
unatumika katika maabara na viwandani kwa utengenezaji wa mbolea (follier
fertilizer) na dawa za kuulia wadudu kwenye mazao.
Anaongeza
kwamba, sungura hapati magonjwa ya mara kwa mara tofauti na wanyama wengine,
lakini ikiwa tu utadumisha usafi na kuwapatia lishe bora.
“Nyama
ya sungura ni tamu na inalingana na nyama ya kuku. Hii ni nyama nyeupe ambayo
haina lehemu (cholesterol) na hiyvo
wataalam wa lishe bora huhimiza matumizi ya nyama ya sungura kwani ni bora kwa
afya,” anasema.
Hata hivyo, anasema anahitaji kuongeza
idadi ya sungura na kupanua mradi wake kabla hajaanza kufikiria kuhusu faida zaidi.
“Kwa sasa ninao sungura 20, wangekuwa
wengi, lakini wengine walikufa wangali watoto kutokana na changamoto ambazo
nilikuwa sijajua namna ya kukabiliana nazo,” anasema.
… Ni sungura tu au?
Anasema hafugi sungura peke yake, bali
anafuga kuku aina ya Saso ambao ni maalum kwa kutaga mayai ya kutotolesha, kuku
wa kienyeji pamoja na njiwa.
“Ninao kuku karibu 500 wa aina ya Saso
ambao wamefikisha miezi minne sasa, bado mwezi mmoja tu waanze kutaga. Nataka
kuweka mashine ya kutotolesha mayai ili niwe ninauza vifaranga,” anasema.
Lilian, ambaye licha ya kustaafu kucheza
shoo mwaka 2016 bado anaendelea na muziki akiwa amegeukia Bongo Fleva, anasema
anao kuku wa kienyeji wapatao 80 sasa wa aina mbalimbali, wakiwemo Kuchi.
Aidha, anasema kwamba, anakusudia kuongeza
zaidi kuku wa kienyeji na kuwazalisha hadi walau wafikie 5,000 ndipo aanze
kuwauza.
“Nataka wafanyabiashara wa kuku wawe
wanakuja hapa kununua badala ya kwenda mikoani, naamini hata ndani ya Jiji kama
hili tunaweza kuzalisha wanyama kwa biashara kwa maeneo tuliyonayo,” anasema.
Ukiacha mifugo hiyo, Lilian ambaye ni mama
wa watoto wawili – Amrock mwenye miaka saba na Bilgis mwenye miaka minne –
anasema ndani ya eneo lake hilo lenye ukubwa wa takriban ekari mbili,
anaendesha kilimo cha bustani pamoja na miti ya matunda.
“Nalima kabichi, spinachi, Chinese,
pilipili hoho, bilinganya, nyanya chungu, mahindi pamoja na mananasi, migomba,
mipera, michungwa na nimepanda mipapai 200 ya kisasa ambayo imeanza kuzaa ikiwa
na miezi mitatu tu,” anasema.
Muumini wa kilimo hai…
Anabainisha kwamba, mazao yote ya shambani
hatumii mbolea za kemikali, bali kinyesi cha mifugo yake pekee, kwani yeye ni
muumini wa bidhaa za kilimo hai.
“Nikitoa kinyesi cha kuku na sungura
napeleka kwenye mazao yangu ya bustani, lakini bado mazao hayo ya shamba pia
yanawafaa wanyama wangu kama sungura na kuku wa kienyeji,” anasema.
Anaongeza kwamba, hakuna kinachotupwa kati
ya mazao ya shamba na mifugo. “Taka za mifugo ni mbolea, mabaki ya mazao ni
chakula cha wanyama!”
Kwanini ujasiriamali?
Lilian anasema kwamba, kwa maisha ya sasa
ni lazima kuwa na mipango mbalimbali ya maendeleo badala ya kutegemea kazi
moja.
Anasema, japokuwa anaendelea na muziki
akipiga Bongo Fleva, lakini ujasiriamali ni ndoto yake ya muda mrefu na kwamba
alishindwa kuifanya kwa kuwa muda mwingi aliutumia jukwaani, tofauti na sasa
ambapo amekuwa na muda wa kutosha unaomruhusu kufanya shughuli nyingine.
“Muda mwingi nilikuwa stejini na bendi,
wakati mwingine nilitakiwa kusafiri nje ya nchi, sikupata nafasi kama
niliyonayo sasa… ukitaka kufanikiwa kwenye ujasiriamali ni lazima mwenyewe
uwepo hata kama unao wasaidizi, na kadiri unavyokuwepo nawe unajifunza na kujua
changamoto zilizopo na namna ya kukabiliana nazo,” anasema.
Anawashauri wanamuziki wenzake, hususan
akinadada, kuwa na mipango mbadala ya maendeleo kwa kuwa hata shughuli hizo za
muziki zina ukomo wake.
“Niko tayari kuwasaidia mawazo vijana na
wasichana wanaotaka kujifunza ujasiriamali, nataka kuwajenga kifikra, kila
mmoja anaweza na tunaweza kubadili uchumi wetu binafsi na taifa kwa ujumla,”
anasisitiza.
Lakini mbali na hilo, malengo yake ni
kuchakata bidhaa zinazotokana na mazao ya mifugo na kilimo ili kuongeza
mnyororo wa thamani.
Imeandaliwa na www.maendeleovijijini.blogspot.com. Simu: +255 656 331974.
Comments
Post a Comment