- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Mmiliki wa blogu ya MaendeleoVijijini, Bw. Daniel Mbega, akiwa katika maingilio ya mfereji mkubwa wa umwagiliaji katika Mto Ruaha ambao unatumika kumwagilia Mradi wa Umwagiliaji wa Mlambalasi mkoni Iringa.
Na Daniel Mbega, Iringa
WANANCHI wa Kijiji na Kata ya Kiwere mkoani
Iringa sasa wanalia. Na kwa bahati mbaya hakuna anayeweza kuwafariji.
Kilio chao kinatokana na uzembe wa viongozi
wao ambao ulisababisha wakauza kienyeji ardhi ya kijiji yenye ukubwa wa ekari
250.
Kweli “…kila
mchuma janga hula na wa kwao!”
Wakati serikali sasa imewajengea Skimu kubwa
ya Umwagiliaji ya Mlambalasi katika Mto Ruaha, wananchi wengi hawana ardhi ya
kutosha kunufaika na kilimo cha umwagiliaji kwa sababu ardhi yote iko mikononi
mwa mwekezaji tangu mwaka 2003.
Kwa bahati
mbaya ama nzuri, ekari hizo 250 zinapitiwa na skimu hiyo ya umagiliji na haziwezi
kurudi tena mikononi mwa kijiji kwani zilipata pia baraka za wanakijiji wote
katika vikao halali.
Wananchi hao walizinduka mwaka 2013 (miaka
1o baada ya kuuza ardhi), baada ya serikali kujenga skimu hiyo ya umwagiliaji
yenye uwezo wa kumwagilia jumla ya hekta 500, kwa makadirio ya kuzalisha tani
2,500 za mpunga kwa awamu moja.
MaendeleoVijijini
ilitembelea eneo hilo na kujionea mfereji
wenye urefu wa kilometa 6.5 kutoka maingilio kwenye Mto Ruaha ambao una ukubwa
wa meta moja na uwezo wa kupitisha meta moja ya ujazo ya maji kwa sekunde (sawa
na lita 1,000 kwa sekunde), ambao ulijengwa na kampuni ya APE Engineers ya
mjini Iringa.
Mmiliki wa blogu ya MaendeleoVijijini, Bw. Daniel Mbega, akipewa maelekezo kuhusu mfereji mkubwa wa umwagiliaji Mlambalasi katika Kijiji cha Kiwere mkoani Iringa.
Baadhi ya
wananchi wa kijiji hicho wanalalamika kwamba serikali ya kijiji ilifanya makosa
kumpatia eneo hilo mfanyabiashara wa mjini Iringa, Abdallaziz Salum Hezhez, kwa
madai kwamba hakustahili kupewa eneo kubwa kiasi hicho, hivyo kutafuta namna ya
kutaka mfanyabiashara huyo anyang’anywe na lirudishwe kwa wananchi.
Tayari
mwekezaji huyo amekwishalikatia Hati Miliki shamba hilo ya miaka 99 chini ya
usimamizi wa Kamishna wa Ardhi.
Presha za
wananchi hao zinadaiwa kusababisha Mwenyekiti wa Kijiji, Ramadhan Ng’anguli,
kujiuzulu uongozi mwishoni mwa mwaka 2012 wakimtuhumu yeye na viongozi wenzake
wa wakati huo kuwahadaa wananchi.
Shamba
linalolalamikiwa na wananchi hao lipo katika eneo la Muhunga, mpakani na Kijiji
cha Luganga, ambalo hata hivyo kwa miaka yote ulikuwa msitu mkubwa ambao
haukuwa ukitumiwa na wananchi hao kwa shughuli zozote za uchumi.
Taarifa
zinaeleza kwamba, wananchi wa kijiji hicho kwa ridhaa yao ndio waliotoa eneo
hilo kwa Hezhez ambaye aliomba ukaazi kijijini hapo tangu Aprili 9, 2003 kwa
barua ya utambulisho iliyosainiwa na Ofisa Mtendaji wa Kata ya
Kitanzini/Miyomboni, Lucas Wikes.
MaendeleoVijijini imeziona nyaraka
zinazoonyesha kwamba, mkutano wa hadhara uliofanyika Juni 26, 2003 na
kuhudhuriwa na wananchi 319, pamoja na wajumbe 14 wa Halmashauri ya Kijiji,
chini ya uenyekiti wa Ramadhan Ng’anguli, ndio ulioridhia kutolewa kwa eneo
hilo na kukabidhiwa kwa mwekezaji huyo kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji.
Muhtasari
wa mkutano huo ulioandikwa Juni 27, 2003 na kusainiwa na Mwenyekiti Ng’anguli
na Ofisa Mtendaji wa Kijiji Fedinanti Sungu unaonyesha kwamba, agenda ya shamba
hilo ilikuwa ya 5.
Agenda
hiyo inasomeka hivi: “Shamba la Muhunga: Mwenyekiti aliwaeleza wananchi kuwa
ndugu Abdallaziz S. Hezhez aliomba shamba kwa ajili ya kuanzisha kilimo cha
umwagiliaji, sisi kama serikali tuliamua kumpa eneo hilo kwa sababu
amekaribisha kilimo cha umwagiliaji. Sisi kama serikali tulitoa eneo hilo,
nyinyi wananchi mnasemaje? Wananchi wote walitoa eneo hilo kwa pamoja na kwa
mikono miwili…”
Mkutano
huo wa hadhara ulikuwa umetanguliwa na kikao cha Serikali ya Kijiji
kilichofanyika Juni 14, 2003, ambacho pamoja na mambo mengine, kilijadili suala
hilo lililokuwa katika agenda namba 6, ambapo iliamuliwa kwamba apewe eneo
hilo.
Mfereji wa umwagiliaji Mlambalasi ukiwa umepita juu kwa juu na kutengeneza daraja.
Aidha,
taarifa zinaonyesha kwamba, Juni 29, 2003, yaani siku tatu baada ya mkutano wa
hadhara uliotoa eneo hilo kwa kauli moja, Kamati ya Huduma za Jamii ya Kijiji
cha Kiwere iliyokuwa na wajumbe watano na wajumbe wawili wa Kamati ya Maliasili
(Mema) walikwenda kuonyesha mipaka ya shamba hilo huku Mwenyekiti na Ofisa
Mtendaji wa Kijiji wakiwa ndio viongozi wa msafara.
Wakati
huo, Kamati ya Huduma za Jamii ilikuwa na Yustin Lipita (Mwenyekiti), Abdul
Chang’a (Katibu) na wajumbe Ajentina Mpogole, Waridi Luvanda na Jose Nkenja,
wakati wajumbe wa Kamati ya Mema walikuwa Samson Fuko (Katibu wa Maliasili wa
Kanda) na Zuhura Mpagama (Katibu wa Maliasili Kijiji cha Kiwere).
Wakati
ambapo aliyekuwa mwenyekiti wa kamati ya huduma za jamii, Lipita, alikiri
kutambua umiliki wa Abdallaziz katika shamba hilo, katibu wake, Abdul Chang’a
alisema yeye ndiye aliyeongoza wenzake katika kutambua mipaka ya shamba pamoja
na kuandika muhtasari wake.
Viongozi
hao wa zamani walisema, kwa nyakati tofauti, kwamba wakati huo walikuwa
wanatimiza wajibu wao tu na kwamba Sheria ya Ardhi ya Vijiji (Sheria Namba 5 ya
1999), ambayo hata hivyo haikuwa inafahamika na wengi, haikuweka kikomo kwa
serikali ya kijiji katika ugawaji wa ardhi.
“Wengi
hatukuwa tunafahamu thamani ya ardhi wala sheria za ardhi wakati huo hazikuweka
kikomo, zaidi sisi tulikuwa tunatimiza wajibu kama viongozi, kwa sababu
wananchi wenyewe ndio hasa walioitoa ardhi hiyo,” alisema Lipita katika
mahojiano.
Kwa upande
wake, mwenyekiti wa kijiji hicho aliyejiuzulu, Ramadhan Ng’anguli, alisema
aliamua kuachia madaraka kwa sababu mbalimbali, ikiwemo hiyo ya shamba la
Muhunga, lakini akabainisha kwamba, wananchi wenyewe ndio waliolitoa eneo hilo.
Ng’anguli
alisema kwamba, ujinga wa kutojua thamani ya ardhi wakati huo ndio uliowafanya
wananchi wakatoa eneo hilo kubwa, lakini baada ya marekebisho ya sheria ya
ardhi yaliyofanywa mwaka 2007 na serikali kubainisha thamani ya rasilimali
ardhi ndipo baadhi ya wananchi walijitokeza kuanza kuhoji suala hilo.
Hata
hivyo, marekebisho ya mwaka 2007 Sheria ya Ardhi hayawapi mamlaka viongozi wa
vijiji kugawa eneo lenye ukubwa wa zaidi ya ekari 50, bali mamlaka hayo anayo
Kamishna wa Ardhi.
“Tatizo
lilikwishamalizika muda mrefu, halmashauri yenyewe ilikwishatoa tamko lake,
lakini inaonekana kuna baadhi tu ya vijana ambao wanakwenda kumtishia mwekezaji
(Abdallaziz Hezhez) kwa lengo tu la kutaka wapate chochote.
“Kimsingi
hakuna mgogoro, wananchi wenyewe ndio waliotoa eneo hilo, ingawa sasa
wanatulaumu sisi viongozi kwamba huenda tulipewa rushwa na mwekezaji huyo ndipo
tukampatia, jambo ambalo siyo kweli,” alisema Ng’anguli.
Ng’anguli
alibainisha kwamba, suala hilo limekwisha kitambo na kama kuna makosa
yalifanyika, basi wanapaswa kujilaumu wananchi wenyewe.
Aidha,
alikanusha madai kwamba mojawapo ya masharti aliyopewa mwekezaji huyo ni
kuwajengea mfereji kwa ajili ya umwagiliaji.
“Siyo
kweli, hakuna mahali popote tulipokubaliana. Huyu mwekezaji shamba lake lipo
mbali kutoka mahali ambapo alitaka kuchukulia maji ya umwagiliaji, hivyo
akasema kwa kuwa anataka kuanzisha kilimo cha umwagiliaji na kwamba atachimba
mfereji, basi maji hayo yatawanufaisha na wananchi wengine mahali mfereji huo utakakopitia,”
alifafanua.
Hati ya kibali cha utumiaji wa maji.
Hata
hivyo, suala hilo ambalo liliibuliwa tena na baadhi ya wananchi mwaka 2012,
lilifafanuliwa vyema na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa kwa barua
yenye Kumb. Na. IDC/D.30/8/32/59
iliyosainiwa kwa niaba yake na G. R. Kaluwa.
“Kwa
mujibu wa sheria za Ardhi za wakati huo (2003) (mwekezaji) alifanya upimaji na
kupewa Hati ya kumiliki kwa miaka 99… kwa maana hiyo Serikali ya Kijiji haina
mamlaka juu ya shamba hilo (kwani ilishalitoa) na kuwa Ardhi ya Kawaida
(General Land).
“Kwa hiyo
wananchi wawe waangalifu pale wanapotoa ardhi kwa watu ambao ni wageni kutoka
nje ya kijiji. Waheshimu maamuzi yaliyofanywa na serikali zilizopita kwani ni
halali na yanasimama kisheria. Ni vyema wananchi wakafuata kanuni, taratibu na
sheria zinazolinda upatikanaji na ugawaji wa ardhi,” ilisema barua hiyo ya
Mkurugenzi.
Kwa upande
wake, Hezhez alisema anashangazwa na watu wanaomchafua na kusema amepora ardhi
yao wakati ambapo anamiliki shamba hilo kisheria na alilipata kwa njia halali.
“Ninazo hati
zote, na niseme ukweli mbele za Mungu, sikutoa rushwa ya aina yoyote kwa
serikali ya kijiji ama mwananchi yeyote ili nipatiwe shamba hilo. Niliomba kama
wanavyoomba wananchi wengi, tena ilichukua muda mrefu kupata,” alisema Hezhez.
Mfanyabiashara
huyo alisema kama kuna mtu yeyote anayedhani kwamba shamba hilo alilipata
isivyo halali na akawa na ushahidi, basi ni vyema akaenda kwenye vyombo vya
sheria badala ya kuendelea kumzushia kwamba amepora ardhi yao.
Comments
Post a Comment