- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Malugala Mwamuyinga (kulia) akimsimulia mmiliki wa blogu hii, Bw. Daniel Mbega, historia ya ukoo wa Chifu Mkwawa.
Na Daniel Mbega, Iringa
MAANDIKO
kadhaa yamekuwepo kuhusiana na historia ya Wahehe na hasa ukoo wa Mtwa
Mkwavinyika Munyigumba Mwamuyinga, maarufu kama Mkwawa, lakini yote hayo hayakunizuia
kuisaka historia hiyo.
‘Jicho
halishibi kuona na Sikio halikinai kusikia!’ hivyo nikaamua kufunga safari hadi
Lungemba, yaliko makaburi ya Mtwa Munyigumba na ndugu wengine wa ukoo huo,
yapata kilometa 62 kutoka Iringa Mjini.
Wapo
walioandika kwamba chimbuko la Mtwa Mkwawa ni Ungazija, lakini simulizi
ninazokutana nazo hapa ni tofauti, maana zinatoka katika vinywa vya wanaukoo wa
Muyinga, ambao nao wameipata ama kurithishwa kutoka kizazi na kizazi kutokana
na simulizi za mababu zao.
Wale
waliopata kuandika kwamba asili ya akina Mkwawa ni Ungazija wanaeleza kuwa
mtawala wa Ngazija aliyeitwa Yusuf Hassan ambaye alikuwa Mwarabu, alizaa watoto
wawili wa kiume, Hassan ‘Mbunsungulu’ na Ahmad.
Wanasema
kwamba Mufwimi alikuwa mmoja wa watoto watatu wa Mbunsungulu aliozaa na
mwanamke wa Kikaguru.
Ndugu zake
wengine walikuwa Ngulusavangi na Ngwila, kwa maelezo yaliyo kwenye baadhi ya
maandishi ambayo yanatoweka kutokana na Watanzania kukosa utamaduni wa
kutembea, kujifunza na kudadisi.
Rungemba
ni kijiji ambacho hakijasikika sana katika historia kama lilivyo jina la
Mkwawa, lakini hapa ndipo kwa kiasi kikubwa lilipo chimbuko la Chifu huyo wa
kabila la Wahehe na ndipo lilipo kaburi la Mtwa Munyigumba.
Ignas
Pangiligosi Muyinga, maarufu kama Malugila Mwamuyinga (67), ambaye ni kitukuu
wa Msengele Kilekamagana, mdogo wake Mkwawa, anaona fahari kuisimulia historia
ya ukoo huo maarufu.
“Shina la
ukoo wetu linaanzia kwa mtu aliyeitwa Mufwimi (yaani Mwindaji), ambaye mababu
zetu walitusimulia kwamba alitokea Ethiopia,” Malugala anaanza kueleza. “Mufwimi
alipita akiwinda kutoka Ethiopia, Kenya kabla ya kuingia Tanganyika na kujikuta
yupo Usagara na hatimaye eneo la Nguluhe-Dabaga akipitia Ikombagulu, himaya ya
Chifu Mwamduda. Wengi walimfananisha na mtu wa kabila la Wakamba kutoka Kenya
kutokana na umbile lake kubwa.”
Wakati huo
eneo ambalo sasa linaitwa Iringa lilikuwa na makabila mbalimbali. Walikuwepo ‘Wahafiwa’
katika Bonde la Milima Welu, Luvango, Wutinde, Lugulu, Makongati, Kalenga,
Kipagala, Kihesa, Tambalang’ombe, Ibanagosi, Tipingi, Ikolofya, Nyambila,
Kibebe na Isanzala.
‘Vanyategeta’
wao waliishi Udzungwa, Kitelewasi na Lundamatwe ya sasa, ambao walikuwa wahunzi
hodari.
‘Vanyakilwa’
walilowea Mufindi wakitokea Kilwa; ‘Vasavila’ waliishi milima ya Welu huko
Makungu (Kihanga ya sasa), Magubike na Malangali; na ‘Vadongwe’ waliishi kando
ya milima ya Uhambingeto, Ipogolo, Nyabula na Luhota.
Mufwimi
alikuwa mwindaji mkubwa wa nyati ambapo aliichoma nyama yake kwa kuipaka chumvi
ambayo ilikuwa haifahamiki kwa wakazi wa himaya hiyo, alimpelekea zawadi ya
nyama-choma Chifu Mwamduda aliyeipenda mno kwa ladha yake.
Alipendwa na
kukaribishwa na Mwamduda kuishi kwake, lakini akaanzisha mapenzi ya siri na Semduda,
binti wa Chifu huyo, ambaye alikuwa amewakataa wachumba wengi. Binti huyo
akapata ujauzito. Mufwimi akaogopa kwa kuona amefanya kosa kubwa ambalo pengine
adhabu yake ingekuwa ni kifo chake.
Jioni moja
akamwita Semduda na kumweleza kwamba yeye anaondoka, lakini akampa maagizo,
ikiwa atajifungua mtoto wa kike amwite Mng’anzagala na akiwa wa kiume amwite
Muyinga Mufwimi (maana yake ni Mhangaikaji Mwindaji).
Mufwimi
alitoroka kwa hofu ya kuuawa na Mwamududa. Akaendelea kuwinda huko na huko hadi
Itamba alikouawa na nyati. Hakuna ajuaye lilipo kaburi lake.
Lakini
kumbe mtawala huyo alifurahi kusikia bintiye ana mimba ya Mufwimi, maana alijua
sasa angekubali kuolewa.
Hata hivyo,
wapi angempata Mufwimi ambaye tayari alikwishatoweka? Hili lilimhuzunisha Chifu
Mwamduda.
JUMAPILI IJAYO: Uchifu
waingia rasmi.
Imetayarishwa na www.maendeleovijijini.blogspot.com.
Simu: +255 656 331974.
Comments
Post a Comment