- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Mto Ruaha Mkuu ambao ni mto wa pili kwa urefu nchini Tanzania ukiwa na urefu wa kilometa 475.
Na Lilian Mkusa, Iringa
LICHA ya
kuwa na vyanzo vingi vya maji katika Mikoa ya Iringa na Njombe bado maji ni
tatizo katika maeneo mengi.
Katika
vituo vingi vya afya na zahanati kumekuwa na changamoto za kukosekana kwa
huduma muhimu ili kuhakikisha utoaji wa huduma za afya na matibabu unaendana na
mazingira safi yatakayo hakikisha kuwa mgonjwa haondoki akiwa na maradhi
mengine.
Huduma
za msingi kama vile maji huhakikisha kwamba pamoja na kuwa mgonjwa amekwenda
kutibiwa aina fulani ya maradhi, anahitaji huduma nyingine kama binadamu wa
kawaida na pia ni vitu vya muhimu kuambatana na huduma bora ya afya.
Kutokuwepo
kwa rasilimali hii muhimu katika zahanati kumekwamisha utolewaji wa huduma kwa
wajawazito, mfano hutakiwa kubeba maji lita tano kwa ajili ya kuwasaidia wakati
wa kujifungua, hali ambayo ni hatari kwa sababu maji hayo kwanza hayatoshi
lakini pia si salama maana haijulikani wapi yamechotwa.
Vijijini
kuna uhaba mkubwa wa miundombinu ya kutosha ya maji.
Upatikanaji
wa maji siyo wa uhakika na wananchi wengi hutegemea maji ya visima na hata
madimbwi au vijito na chemchemi ambazo nyingi huwa si salama kwa matumizi ya
binadamu.
Kutokana
na kutokuwepo kwa miundombinu ya kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa maji
safi, wananchi wa maeneo ya vijijini hulazimika kutumia vyanzo vya maji
vinavyowazunguka bila kujali usalama wa maji hayo na hivyo kuweka afya zao
katika hatari.
“Tunalazimika
kubeba mashuka na kwenda kuyafulia nyumbani, tena tunayafua mtoni ambako
tunatembea hadi kilometa 9, kwa hali anayokuwa nayo mjamzito akitoka kujifungua
ni hatari kutembea umbali huo,” anasema Selina Mwemile, mkazi wa Kijiji cha
Lundamatwe wilaya ya Kilolo.
Zahanati
hazina mabafu hali ambayo huwalazimu wajawazito na wagonjwa wengine kuoga chooni
ambako hali ya usafi si nzuri. Kutokana na hali hiyo wengi huoga vichakani
mahali ambapo si salama hasa kwa hali wanazokuwa nazo.
“Wakati mwingine mtu anaona ajisaidie
kichakani na sio katika vyoo vya zahanati maana hali ni mbaya sababu tunakutana
watu wa tabia tofauti, sasa kama wote tukijisaidia vichakani hali itakuwaje?”
anasema Maria Nyenza mkazi wa Kijiji cha Idegenda.
Pamoja na
hayo, bado hakuna utaratibu wa kuwepo kwa maji safi na salama ya kunywa katika
zahanati, wakati mwingine mgonjwa hutakiwa kumeza dawa papo hapo lakini badala
yake huambiwa akameze nyumbani au akatafute maji popote ambapo hujikuta akinywa
maji yasiyo safi na salama.
Kitapu kipo lakini maji hayatoki.
Bado
hakuna mfumo bora wa kuvuna maji katika sehemu hizi za kutoa huduma ilhali
kulikuwa na umuhimu wa kutoa elimu juu ya suala hilo pamoja na vifaa maalumu
vya kuhifadhi maji hayo ya mvua. Bomba zilizoharibika hazifanyiwi matengenezo
na badala yake zimekuwa mapambo wakati zingeweza kutengenezwa na maji
yakapatikana. Kwa ujumla hakuna ufuatiliaji yakinifu wa masuala ya maji.
“Yalishaletwa
hadi mabomba hapa na yakaunganishwa kabisa lakini ghafla tu tukaona yanatolewa
sasa sijui tatizo lilikuwa nini na mpaka leo kimya tumeshafuatilia tumechoka,”
anasema Rashid Kihombo mkazi wa kijiji cha Lihagule wilaya ya Ludewa.
Kuna
umuhimu mkubwa wa kuwekwa miundombinu ya uhakika ya upatikanaji wa maji hasa
katika maeneo ya vijijini kwenye vituo vya utoaji wa huduma za afya ili
kuwahakikishia wakazi wa maeneo ya vijijini uhakika na ustawi wa afya zao
kupitia huduma ya uhakika ya maji safi na salama.
Imeandaliwa
na www.maendeleovijijini.blogspot.com.
+255 656 331974.
Comments
Post a Comment