- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Mbunge wa Kilolo, Venance Mwamoto, akiwa katika Kijiji cha Mhanga, Kata ya Kimala, akionyesha Wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro inayopakana na Wilaya Kilolo.
Na Daniel Mbega, Kilolo
WANANCHI wa
Wilaya ya Kilolo mkoani Iringa wanalia hawana ardhi. Na wataikosa kwa miaka 100
ijayo, au pengine milele, kwani hata vizazi vyao havitakuwa na kumbukumbu kama
wazazi wao waliwahi kumiliki ardhi.
Kwa sasa hawana
hata ardhi ya akiba, inapotokea kuna mradi wa jamii, hata wa kujenga zahanati,
lazima serikali za vijiji zinunue eneo kwa wananchi wengine wenye ziada.
Si kwamba
hawakuwa na ardhi, walikuwa nayo. Lakini ile ardhi ambayo mababu zao, akiwemo
Chifu Mkwavinyika Munyigumba, waliipigania isitwaliwe na wakeng’e (Wazungu), sasa wameiuza kwa wawekezaji wa Kampuni ya New
Forests kutoka Uingereza, kwa bei ya karibu na bure.
Kilio chao
hakiwezi kusikika, kwani waligawa ardhi hiyo kwa hiari wala hawakushikiwa
bakora. Ufukara na ujinga wa kutojua thamani ya ardhi ndivyo vilivyowaponza,
jambo ambalo hata viongozi wao wanakiri.
MaendeleoVijijini inafahamu kwamba, zaidi ya hekta 8,000
(takriban ekari 20,000) zimetwaliwa na New Forests Company (NFC) kwa ajili ya
kupanda miti aina ya Misindano na Mikaratusi.
Ilikuwa hivi:
Kampuni ya New Forests ilikuwa na fedha za kuwekeza … wananchi walikuwa na
ardhi. Wawili hao wakaingia ‘mkataba’ lakini wananchi wamepoteza – wamemeza
chambo, ndoano imewakaba.
Vijiji vingi
katika Kata za Idete, Ukwega na Dabaga ambako kampuni hiyo imewekeza havina
tena ardhi ya ziada kwa kizazi cha sasa na hata kijacho. Wawekezaji hao
wamepata hatimiliki kwa karne nzima, miaka 99. Kizazi cha sasa hakitakuwepo na
kijacho hakitajua pa kuanzia.
“Ujinga na
umaskini ndio umewafanya wananchi wauze ardhi, hawakupewa elimu kuhusu thamani
ya ardhi, walipoona fedha, na baada ya kushawishiwa na viongozi wa serikali za
vijiji, wakaamua kuuza kwa bei ya kutupa. Hekta moja waliuza kwa kati ya Shs.
50,000 na 100,000 tu,” alisema Mejusi Mgeveke, Diwani wa zamani wa Kata ya
Kimala wakati alipoongea na mtandao wa MaendeleoVijijini.
NFC iliomba
kibali cha uwekezaji Tanzania kupanda hekta 20,000 za miti. Mpaka sasa imepata
jumla ya hekta 8,000 tu wilayani Kilolo, bado inaendelea kutafuta ardhi katika
maeneo hayo ya Nyanda za Juu Kusini na safari hii wanaelekea Wilaya ya Mufindi
na mkoani Njombe.
Maeneo ambako
NFC imepata ardhi ni katika vijiji vya Lukosi ambako kuna hekta 2,270.4 (Shamba
Namba 972), Kising’a hekta 3,851.53 (Shamba Namba 973), Ipalamwa hekta 62.4
(Shamba Namba 974), Ndengisivili hekta 121.5 (Shamba Namba 975), Ukwega hekta
94.6 (Shamba Namba 976), Isele hekta 1,215 (mpango wa mwaka 2013), Idete hekta
50 na eneo jingine bado ‘wanalifukuzia’ katika Kijiji cha Makungu kwenye Kata
ya Ukwega.
Tangu imeanza
uwekezaji wa kilimo hicho cha miti kwa ajili ya matumizi ya viwandani mwaka
2010, kampuni hiyo kutoka Uingereza imetumia kiasi cha Dola 110 milioni
(takriban Shs. 176 milioni).
Kampuni
imekwishapatiwa hatimiliki kwa mashamba ya Lukosi na Ukwega kwa muda wa miaka
99. Bado inasubiri hatimiliki kwa mashamba yaliyobaki.
Lengo lake
jingine ni kuvuna hewa ya ukaa (Carbon Dioxide), ambayo kwa muda sasa imekuwa
ikihitajika katika nchi nyingi za Ulaya Magharibi katika harakati za Umoja wa
Mataifa kupunguza joto kutokana na ufyekaji wa misitu pamoja na mabadiliko ya
tabianchi.
Lakini wakati
taarifa za NFC zinasema kwamba mpaka sasa wamepata takriban hekta 8,000, Diwani
wa Kata ya Kimala, Mejusi Mgeveke, anasema eneo lililochukuliwa na wawekezaji
hao ni hekta 13,000 (ekari 33,500) likihusisha vijiji vyote vilivyotajwa.
Taratibu zilizotumika
Uchunguzi
uliofanywa na MaendeleoVijijini
umebaini kwamba, utaratibu uliotumika kupata ardhi hiyo haukuwa wazi katika
maeneo mengi.
“Walipokuja
wawekezaji kuomba ardhi miaka mitano iliyopita wananchi walielezwa kwenye
mikutano ya hadhara, wakaridhia, wataalamu wakaja kupima na kuthaminiwa.
Wananchi wakalipwa fidia,” alisema Aridi Sanga, Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha
Magome katika Kata ya Dabaga.
Maelezo yake yaliungwa
mkono na Diwani wa zamani wa Kata hiyo, Amin Tengelakwi, ambaye anasema wakati
walipokuja NFC katika maeneo hayo wananchi walishirikishwa na wakaridhia
wenyewe kutoa maeneo hayo.
“Ardhi
iliyotolewa ipo eneo la Wotamasiwa, ambalo ni la kijiji na la watu binafsi,
lakini kwa miaka mingi lilikuwa halitumiwi.
“Waliokuwa
wakipanda miti kwenye maeneo hayo ilikuwa ikiungua tu kwa vile wanajijiji wa
Kiwalamo walikuwa wakianzisha moto wakati wa kuandaa mashamba, hivyo serikali
ikaona ni vyema wakampatia mwekezaji,” alisema Tengelakwi na kuongeza kwamba
fidia iliyotolewa na mwekezaji ilikuwa Shs. 100,000 kwa hekta.
Tengelakwi alisema,
uhusiano baina ya wananchi na mwekezaji ni mzuri. “… amesaidia kujenga nyumba
ya mganga katika zahanati ya Magome na ameahidi kujenga vyumba viwili vya
madarasa na matundu manne ya vyoo kwenye Shule ya Msingi Kidabaga.”
Lakini si diwani
huyo wala mtendaji anayejua wapi mihutasari ya mikutano hiyo ya wananchi ilipo
hasa baada ya uongozi wa zamani wa Kata na Kijiji cha Kidabaga kutimuliwa mwaka
2012 kutokana na kutumia mabavu kuwachapa viboko wananchi.
Katika vijiji
vya Kimala, Idete, Magome, Kising’a, Makungu na Ipalamwa, hakuna kumbukumbu
zozote za kuonyesha mihutasari ya vikao hivyo wala makubaliano baina ya vijiji
na wawekezaji zaidi ya makubaliano ya mdomo kwamba wawekezaji wangetoa misaada
kwa huduma za jamii.
Tofauti na
wawekezaji wengine wa kilimo cha miti ambao wameandikishana na wanavijiji
kwamba watatoa asilimia 10 ya mapato yao kusaidia shughuli za maendeleo, NFC
yenyewe haikufanya hivyo.
Kaimu Ofisa
Mtendaji wa Kata ya Idete, Anderson Kitule, alisema hakuna mikataba yoyote ya
maandishi baina ya wananchi na mwekezaji, hivyo hawajui hata nini ambacho
wanajamii wanaouzunguka mradi watanufaika na uwekezaji huo.
“Tumejengewa tu
bweni la wasichana katika shule ya sekondari ya Madege na wawekezaji hawa ambao
pia wamejenga matundu ya vyoo na kutoa vitanda, magodoro, mablanketi kwa ajili
ya bweni hilo,” alisema.
Bruno Hakimu
Kauku, aliyekuwa Diwani wa Kata ya Idete, ambayo vijiji vyake vya Kiwalamo na
Idete vimetoa ardhi kwa mwekezaji, anasema hakuna nyaraka zozote kuonyesha
mchakato mzima wa utoaji ardhi katika kata hiyo.
Malipo ya fidia
Utaratibu wa
malipo ya fidia kwa wananchi nao haukuwiana na thamani halisi ya ardhi na wala
haukuwiana kutoka eneo moja na lingine. Mahali pengine fidia ilikuwa Shs.
100,000, lakini kwingine wakalipwa 25,000 kwa hekta.
“Wawekezaji
walipokuja walichukua ardhi kubwa, fidia ilikuwa ndogo, lakini kutokana na
uelewa mdogo tulikwenda hivyo hivyo,” alisema Mgeveke, Diwani wa Kata ya
Kimala.
Kwa sasa,
anasema, wananchi wameshtuka, wametambua thamani ya ardhi, lakini hawana ardhi
ya ziada.
Atilio Msigala,
Mwenyekiti wa aliyepita wa Kijiji cha Kising’a katika Kata ya Ukwega, anasema
malipo ya fidia kwa wananchi waliotoa ardhi yalikuwa madogo na yalichelewa
tangu ardhi yao ilipofanyiwa tathmini mwaka 2005.
“Kijiji hakina
eneo, wananchi ndio waliowapa ardhi NFC, lakini fidia ilikuwa ndogo, ardhi
ilithaminishwa mwaka 2005 kwa kiasi cha Shs. 25,000 kwa hekta, malipo ya kwanza
yalitolewa mwaka 2010, na yale ya mwisho yalitolewa mwaka 2011 ambapo hekta
moja ililipwa kwa Shs. 40,000,” alisema Msigala.
Kijiji cha
Kising’a kina eneo la hekta za mraba 8,884.58 na zilizotolewa kwa mwekezaji ni
hekta 3,851.53, ingawa mwenyekiti huyo anasema eneo lililotolewa ni hekta 4,500
ikiwa ni zaidi ya nusu ya eneo la kijiji.
Diwani wa Kata
ya Ukwega, Israel Mwilafi, ambaye ukoo wake walitoa hekta 400 (sawa na ekari
1,000), alisema walau wao ‘walilipwa vizuri’ mwaka 2011 kwa Shs. 40,000 kwa
ekari moja.
“Sisi tulilipwa
vizuri, ilikuwa Shs. 40,000 katika awamu ya pili tofauti na wale wa kwanza
ambao walilipwa Shs. 25,000,” alisema.
NFC wanasemaje?
Uongozi wa NFC tawi
la Tanzania, ulisema kwamba wao walifuata taratibu zote zinazotakiwa kupata
ardhi ambapo walifika kwenye serikali za vijiji na kupeleka maombi yao,
mikutano ikafanyika na mihutasari ikawasilishwa kwenye Kata, Halmashauri ya
Wilaya na baadaye Wizara ya Ardhi ambako wamepata hatimiliki na bado wanasubiri
nyingine.
“Hatujapora
ardhi, taratibu zote zilifuatwa baada ya kupewa kibali cha uwekezaji. Bila
taratibu hizi katu serikali haiwezi kutoa hatimiliki. Sisi hapa tunayo
mihutasari yote, kama vijiji havina basi ni juu yao wenyewe,” alifafanua mmoja
wa maofisa wa kampuni hiyo.
Hata hivyo, alikiri
kwamba hakuna makubaliano ya kimaandishi kuhusiana na kile ambacho wananchi
wanastahili kukipata kama gawiwo kutokana na faida watakayoingiza hapo baadaye.
Na katika kuendelea kuwa karibu na wananchi, kampuni hiyo inachangia huduma za jamii kama kujenga zahanati katika vijijini mbalimbali, ikiwemo Kiwalamo ambako wamekamilisha ujenzi wa zahanati iliyogharibu Shs. 44.7 milioni.
Jengo mojawapo la zahanati katika Kijiji cha Kiwalamo, Kata ya Idete wilayani Kilolo lililojengwa na kampuni ya New Forests.
Aliyekuwa Mkuu
wa Kitengo cha Mawasiliano katika Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya
Makazi, Abraham Nyantori, anasema kimsingi wawekezaji wanatakiwa kupitia kwenye
serikali za vijiji katika uombaji wa ardhi na wananchi washirikishwe kikamilifu
ili kuridhia.
“Kwa
kuwashirikisha wananchi maana yake tutakuwa tumeondoa migogoro ya ardhi,” anafafanua
na kuongeza kwamba ni vyema fidia nayo walau ikalingana na thamani ya ardhi.
Imeandaliwa
na www.maendeleovijijini.blogspot.com.
+255 656 331974.
Comments
Post a Comment