- Get link
- Other Apps
Featured Post
Posted by
Maendeleo Vijijini
on
- Get link
- Other Apps
Jacques Issa Nundu (kulia) akiwa na Abubakar Kassongo Mpinda enzi ya uhai wao.
Jacques Issa Nundu (alizaliwa Julai 23,
1954 Uvira, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo) alikuwa mwanamuziki raia wa Congo
aliyejizolea umaarufu mkubwa akiwa nchini Tanzania ambako aliishi hadi mauti
yalipomfika Jumamosi Oktoba 25, 2014 na kuzikwa mjini Moshi, Kilimanjaro.
Maisha yake ya awali
Jacques
(Jackson) Issa Nundu alizaliwa katika Kijiji cha Nundu huko Uvira katika Jimbo
la Kivu, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo akiwa mtoto wa Chifu Sadi Issa Nundu.
Ndiyo maana hata wakati akiwa nchini Tanzania alikuwa akiitwa Prince Jacques
Issa Nundu.
Issa Nundu
alijaaliwa sauti nzuri na alikuwa mtunzi na mwimbaji mahiri ingawa taaluma
aliyoisomea ilikuwa ni ufamasia ambapo alipata kufanya kazi katika Hospitali ya
Uvira kama Mfamasia.
Akiwa katika hospitali hiyo alikuwa akifanya kazi asubuhi
hadi mchana, ambapo usiku alikuwa akienda kupiga muziki katika bendi ya Bavy
National akiwa na mpiga solo Dekula Kahanga Vumbi ambako alijizolea umaarufu
mkubwa kutokana na sauti yake murua.
Wakati huo
alikuwa na uwezo wa kukariri kisha kuimba nyimbo za wanamuziki wakongwe
mbalimbali zikiwemo za akina Dk. Nico Kasanda wa African Jazz.
Issa Nundu
aliitumikia bendi ya Bavy National kati yam waka 1981 hadi 1983 ambapo
aliondoka Uvira na kwenda Tanzania akiongozana na mtunzi na mwimbaji Kyanga
Songa ambaye pamoja na kila mmoja kujiunga na bendi tofauti, lakini walikutana tena
katika bendi ya Marquis du Zaire mwaka 1986 kabla Issa Nundu hajahamia MK.
Group mwaka 1990.
Akiwa
jijini Dar es Salaam, Issa Nundu alipigia bendi za Orchestra Makassy, Orchestra
Super Matimila, Maquis du Zaire, MK. Group, Bana Marquis, Super Kamanyola ya jijini Mwanza na La
Capitale ‘Wazee Sugu’ ambayo aliitumikia hadi alipoanza kuugua na mauti
kumkuta.
Alipokuwa
katika bendi ya Makassy alikutana na waimbaji mahiri akiwemo Mbombo wa
Mbomboka, Mzee Kitenzogu Makassy na Maliki Star na wengine wengi.
Wakati alipojiunga
na Marquis du Zaire, wakati huo ikipiga katika ukumbi wa White House-Ubungo,
alikuwa na miamba ya uimbaji akina Mutombo Lufungula ‘Audax’, Mbuya Makonga
‘Adios’, Mukumbule Lolembo ‘Parashi’, Kabeya Badu, Kalala Mbwebwe, mapacha
Kassalo Kyanga na Kyanga Songa, Kiniki Kieto, Abubakar Kasongo Mpinda
‘Clayton’, Mbombo wa Mbomboka, Kikumbi Mwanza Mpango ‘King Kiki’, Tshimanga Kalala
Assosa, Masiya Radi ‘Dikubakuba’, Rahma Shaari, Anna Mwaole na Mary Mwanjelwa.
Akiwa
Marquis aliimba peke yake wimbo wa Sikutegemea,
ambao aliuimba kwa sauti yenye simanzi mno.
Lakini pia alitunga wimbo wa Marusu
uliorekodiwa studio za Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) mwaka 1989, ambapo
solo limekung’utwa na Dekula Kahanga Vumbi.
Alipokwenda
katika bendi ya MK Group iliyokuwa ikipiga muziki katika Hoteli ya New Africa,
Issa Nundu alikutana na waimbaji mahiri akiwemo kiongozi wa bendi hiyo
Aboubakar Kasongo Mpinda ‘Clayton’, Kapaya Vivi na wengine wengi.
Nundu
alijiunga na Bana Marquis iliyokuwa inaongozwa na Tshimanga Kalala Assosa mwaka
1994 akiwa pamoja na Anna Mwaole na Aboubakar Kasongo Mpinda ‘Clayton’. Baadaye
yeye na Mukumbule Lulembo ‘Parashi’ na Anna Mwaole walikwenda jijini Mwanza na
kujiunga na bendi ya Super Kamanyola.
Mauti
Issa Nundu
alifariki alfajiri ya Jumamosi Oktoba 25, 2014 katika Hospitali ya KCMC mjini Moshi
alikokuwa amelazwa kutokana na kusumbuliwa na tatizo la kusinyaa kwa ubongo.
Mwanamuziki
huyo aliamua kurudi kwao Congo lakini alipofika Kigoma alizidiwa na kulazwa
huko kabla ya kuhamishiwa KCMC Moshi kwa matibabu zaidi. Alizikwa Jumanne
Oktoba 28, 2014 mjini Moshi ambapo baba yake Said Issa Nundu alihudhuria
mazishi hayo. Aliacha mjane na watoto kadhaa.
Comments
Post a Comment